Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Chuja:

Habari Mpya

Hapa na pale

Shirika la UM juu ya Matumizi ya Amani ya Nishati ya Nyuklia (IAEA) limetangaza leo kuwa linahitajia kupokea kutoka Iran taarifa zaidi, na ruhusa ya kuchunguza kiwanda cha fueli ya kusafishia madini ya yuraniamu, ambacho kinajengwa sasa hivi na Iran. Marc Vidricaire, msemaji wa IAEA aliripoti kwamba kwenye barua iliotumiwa taasisi yao na Iran, mnamo tarehe 21 Septemba 2009, ilielezwa kwamba Iran inajenga kiwanda kipya cha kutengenezea nishati na taarifa zaidi juu ya kadhia hiyo, zitatumiwa IAEA "katika muda mwafaka na kwa wakati upasao." Vidricaire alisema "IAEA imeiomba Iran kuwapatia, haraka iwezekanavyo, taarifa maalumu kuhusu ujenzi huu na kuwapatia wataalamu wa IAEA ruhusa ya kuzuru na kufanya ukaguzi wa kiwanda ili kuthibitisha kama ni salama kufanya shughuli zake." Aliongeza kusema Iran imeiarifu IAEA kwamba hakuna vifaa vya kinyuklia kwenye jengo la kiwanda kipya.

Hapa na pale

"Matatizo makubwa yataukabili ulimwengu mzima ikiwa tutashindwa kuusuluhisha mzozo wa Usomali". Onyo hili lilitolewa na Naibu KM juu ya Masuala ya Kisiasa, B. Lynn Pascoe alipohutubia wiki hiii mkutano wa Kundi la Kimataifa la Mawasiliano juu ya Usomali (ICGS). Alisema taasisi za mpito ziliopo nchini kwa sasa hivi ndizo zenye fursa ya kurudisha tena hali ya utulivu na amani Usomali, hali ambayo haijawahi kushuhudiwa tangu 1991. Aliongeza kwa kusema ni muhimu kwa jamii ya kimataifa kufadhilia misaada hakika, na yenye maana, kwa Serikali ya Mpito Usomali ili ipate uwezo wa kuimarisha vyema utawala wake. Msaada wa kimataifa vile vile utaisaidia Serikali kuanzisha taasisi zitakazoshughulikia mahitaji ya umma na baadaye kuzalisha natija za amani. Pascoe aligutusha kwamba mashambulio ya wiki iliopita mjini Mogadishu kwenye Makao Makuu ya vikosi vya ulinzi amani vya Umoja wa Afrika, AMISOM, yanathibitisha dhahiri kuwepo haja kuu ya kujumuisha jumuiya ya kimataifa katika kuisaidia Serikali ya Mpito kudhibiti bora utawala nchini.

UNRWA inaadhimisha miaka 60

Viongozi wa kitaifa na mawaziri wa vyeo vya juu kutoka sehemu mbalimbali za dunia walikusanyika leo hii kwenye Makao Makuu ya UM mjini New York kuhishimu mchango wa Shirika la UM Linalofarajia Wahamiaji wa KiFalastina katika Mashariki ya Karibu (UNRWA) kuhudumia kihali umma wa KiFalastina, shirika ambalo leo limetimiza miaka 60 tangu kubuniwa.

Hapa na pale

Raisi Barack Obama wa Marekani alipohutubia Baraza Kuu la UM aliwaambia wajumbe wa kimataifa kwamba taifa lake lipo tayari kuanzisha mlango mpya kwenye uhusiano wa kimataifa na nchi wanachama. Aliyataka mataifa yajihusishe kwenye awamu yenye lengo la kukidhi masilahi ya pamoja ya umma wote wa dunia, na kwenye mazingira ambapo mataifa yatahishimiana. Aliutaka ulimwengu kuongeza juhudi zao, mara mbili zaidi, zitakazohakikisha UM utatumiwa kama ni kipengele muhimu cha kuendeleza masilahi ya pamoja ya umma wote wa ulimwengu. Alisisitiza kwamba ukubwa wa matatizo yalioukabili ulimwengu sasa hivi, bila shaka yanahitajia mchango wa Mataifa Wanachama yote, mchango utakaoipa taasisi ya UM maana hakika ya jina lake, kama ni taasisi inayosimamia masilahi ya Mataifa Yalioungana. Alisema mwelekeo huo ndio Marekani ungelipendelea kuuona unatumiwa kuendeleza uhusiano wa kimataifa katika siku za baadaye - hali itakayokuwa ya amani na yenye ustawi, ambayo walimwengu wote wanaweza kuifikia, tukitambua kwamba kila taifa lina haki na dhamana ya kutekeleza majukumu hayo. Makubaliano haya, alitilia mkazo, ndio yenye uwezo wa kuyafikia malengo yanayoridhisha katika uhusiano wa kimataifa.