Kamati ya UM ya Kuondosha Ubaguzi Dhidi ya Wanawake (CEDAW) ambayo inakutana wiki hii kwenye Makao Makuu ya UM mjini New York, imeanza shughuli za kusailia namna nchi wanachama zinavyotekeleza mikataba ya kimataifa ya kukomesha ubaguzi wa kijinsiya. Kamati hii ya CEDAW imetimia miaka 30 katika mwaka huu. Mwenyekiti wa Kamati ya Kuondosha Ubaguzi Dhidi ya Wanawake, Naela Mohammed Gabr wa kutoka Misri, Ijumatano aliwaambia waandishi habari wa Makao Makuu kwamba miongoni mwa masuala muhimu wanayoyazingatia kwenye kikao cha safari hii ni pamoja na ile mada inayohusu taathira za mizozo ya fedha iliopamba duniani karibuni na namna inavyochafua huduma za kimsingi za jamii. Vile vile alisema Kamati inasailia mada zinazohusu mishahara wanaopatiwa wanawake kwenye mazingira ya mizozo ya kifedha kimataifa, pamoja na tatizo la kuzidi kwa ukosefu wa kazi miongoni mwa wanawake." Kwa mujibu wa taarifa za UM Kamati ya CEDAW hutumia taratibu mbalimbali za kuhamasisha nchi wanachama kutekeleza mapendekezo yake ya kukomesha ubaguzi wa kijinsiya, mathakan, Kamati mara nyingi huchapisha rasmi ukiukaji wa haki za wanawake katika taifa fulani, fafanuzi ambazo baadaye huutumiwa Ofisi ya Kamisheni wa UM juu ya Haki za Binadamu iliopo Geneva. Ofisi ya haki za Binadamu hujumuisha matokeo ya uchunguzi wa Kamati ya CEDAW kwenye ule Mradi wa Mapitio ya Jumla kuhusu namna haki za binadamau zinavyotekelezwa katika Mataifa Wanachama 192 wa UM. Mapitio haya hufanyiwa kila taifa, mara moja katika kila miaka minne. Kwenye mkutano wa wiki hii wataalamu 22 wa Kamati ya CEDAW wanafanyia mapitio juu ya hali za wanawake katika mataifa ya Azerbaijan, Bhutan, Denmark, Guinea-Bissau, Laos, Ujapani, Liberia na pia Uspeni, Uswiss, Timor-Leste na Tuvalu.