Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Chuja:

Habari Mpya

Hapa na pale

Mjumbe Binafsi wa KM kwa Sahara ya Magharibi, Christopher Ross, anaelekea kwenye eneo husika kwa ushauri, baada ya kukutana na KM, wajumbe wa Baraza la Usalama na wawakilishi wa makundi husika – yaani, Chama cha Ukombozi wa Sahara Magharibi (Frente Polisario) na Morocco. Ross ataanza ziara yake ya mashauriano kesho Ijumatano katika mji wa Rabat, Morocco. Hii itakuwa ni ziara ya awali kwenye eneo, baada ya kushika rasmi wadhifa wa Mjumbe Binafsi wa KM.

Baraza Kuu litazingatia marekibisho ya mfumo wa BU

Wiki hii, mnamo tarehe 19 Februari, wawakilishi wa Mataifa Wanachama wa Baraza Kuu watakusanyika kwenye Makao Makuu ya UM kujadiliana juu ya ile rai ya kuleta marekibisho kwenye mfumo wa Baraza la Usalama, kwa lengo la kuhakikisha kazi za taasisi hii ya kimataifa zitawakilisha, kwa usawa, na kwa haki matakwa na mahitaji hakika ya wanachama wote wa UM, yatakayolingana na hali halisi ilivyo kwenye uhusiano wa kimataifa wa karne ya ishirini na moja.

Mshindi wa Tunzo ya Haki za Binadamu, kutokea JKK, azungumzia uokoaji afya ya wasibiwa na uhalifu wa nguvu wa kijinsia

Makala yetu maalumu, kwa leo, itazingatia juhudi za daktari mmoja shujaa, kutokea Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (JKK), aliyehamasishwa kiutu na kizalendo, kujishirikisha kwenye huduma za kufufua afya ya wale wanawake, na watoto wa kike, waliosibiwa na mateso ya jinai ya kunajisiwa kimabavu na kihorera, kutokana na mazingira ya vurugu kwenye eneo la mashariki ya JKK.

Hapa na pale

KM Ban Ki-moon ameripotiwa kushtushwa, kwa shambulio la kujitoa mhanga dhidi ya wachaMngu wa KiShia, liliotukia Ijumaa karibu na Baghdad. Kadhalika, KM alisema ameshtushwa na mashambulio mengine kama hayo yaliotukia majuzi Iraq ambayo yalisababisha darzeni za vifo na kujeruhi raia kadha wa kadha, ikijumlisha fungu kubwa la watoto wadogo na wanawake. KM alisisitiza hakuna sera ulimwenguni inayohalalisha vitendo hivi, si ya kidini wala kisiasa, na alikumbusha walimwengu wanawajibika, pote walipo, kulaani kwa lugha nzito kabisa makosa kama haya ya jinai kuu dhidi ya wanadamu. KM aliusihi umma wa Iraq kupinga kabisa jaribio katili linalotaka kuchochea fujo za kiitikadi nchini mwao, na aliwataka viongozi wa Iraq kuungana pamoja, kwa moyo wa kuhishimiana na uelewano wa kizalendo, kama walivyofanya wakati walipokwenda kupiga kura karibuni kwenye uchaguzi wa majimbo, uchaguzi ambao ulifanyika mwezi uliopita bila fujo.