Pfizer yahitaji -70℃, AstraZeneca 2 °C hadi 8 °C sasa ipi inafaa wapi na kwa nini?
Pfizer yahitaji -70℃, AstraZeneca 2 °C hadi 8 °C sasa ipi inafaa wapi na kwa nini?
Ugonjwa wa virusi vya Corona au COVID-19 ulitangazwa na shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni, WHO kuwa janga la afya ya umma duniani tarehe 30 mwezi Januari mwaka 2020.
Ili kudhibiti kuenea kwa maambukizi WHO mpaka sasa imeshaidhinisha aina 6 za kwa ajili ya matumizi ya dharura ya chanjo dhidi ya coronavirus">COVID-19.
Chanjo hizo ni Pfizer/BioNTech, AstraZeneca/Oxford moja ikitengenezwa na Korea Kusini na ile inayotengenezwa na taasisi ya Serum nchini India, Moderna, Johnson & Johnson, Sinovac na Sinopharm. Chanjo hizo ni miongoni mwa chanjo zaidi ya 200 ambazo ziko kwenye utafiti ili kukabili Corona.
Ubaridi wa kuhifadhi chanjo unatofautiana
Mwongozo wa WHO unaonesha kuwa kila chanjo iliyoidhinishwa kwa matumizi ya dharura ina masharti yake hasa katika uhifadhi na utumiaji ili iweze kuwa na ufanisi. Mathalani Pfizer inahitaji ubaridi wa nyuzi joto hasi 70 katika kipimo cha selsiyasi (-70℃). Halikadhalika lazima chanjo iwe imeganda, na iwapo itayeyuka na kuganda tena basi ufanisi wake unapungua. Kiwango hicho cha ubaridi cha uhifadhi ni changamoto kwa nchi nyingi za kipato cha chini na kati ambazo hazina miundombinu ya majokofu ya kuhifadhi na kusambaza chanjo.
AstraZeneca kwa upande wake inahitaji ubaridi wa kati ya nyuzi joto 2 hadi 8 katika kipimo cha selsiyasi ( +2 °C hadi 8 °C,) kiwango ambacho ni sawa na chanjo za kawaida ambazo hutolewa katika nchi za kipato cha chini na kati. Na chanjo hizi hazihitajiki kuwa zimeganda barafu wakati anapatiwa mhusika.
Wataalamu wanasema kuwa chanjo kama Pfizer na Moderna zinazotumia teknolojia ya kuchochea seli ya mwili kuzalisha protini ili kuongeza kinga ya mwili dhidi ya virusi na hivyo zikipata joto au baridi kupitiliza zinaharibika na kama ilivyo kwa samaki, chanjo iliyoharibika lazima itupwe na WHO haitaki hata dozi moja ya chanjo itupwe. Hivyo lazima nchi kuzingatia mifumo na masharti ya uhifadhi wa kila chanjo.
Matumizi yako vipi?
Kwa chanjo ya Pfizer, iwapo haijachanganywa na imehifadhiwa katika nyuzi joto hasi 90 hadi hasi 60 (-90 °C hadi -60 °C) inaweza kutunzwa kwa miezi 6 tangu itengenezwe. Lakini ikiwa kwenye nyuzi joto 2 hadi 8 inaweza kutumika ndani ya siku 5 tu,na joto likipanda zaidi na kuwa nyuzi joto 30 inapaswa iwe imetumika ndani ya saa 2. Na iwapo itachanganywa na iko katika nyuzi joto 2 hadi 30 basi lazima itumike ndani ya saa 6.
Kwa upande wa AstraZeneca kichupa cha chanjo ambacho hakijafunguliwa na kimehifadhiwa katika nyuzi joto kati ya 2 hadi 8 (2 °C hadi 8 °C ) kinaweza kutumika hadi miezi 6. Kile ambacho kimeshafunguliwa lakini kiko katika ubaridi wa kati ya nyuzijoto 2 hadi 25 katika kipimo cha selsiyasi (2 °C hadi 25 °) kinaweza kutumika ndani ya saa 6 tu.
Kwa nini chanjo hizo zimeorodheshwa kwa matumizi ya dharura?
WHO inasema ni kwa kuzingatia mazingira ya janga la Corona, chanjo zinaweza zisiwe zimekidhi vigezo vya awali vya kuidhinishwa moja kwa moja, na hivyo basi jopo linazipitia na kuidhinisha ziwe kwenye orodha ya matumizi ya dharura ili kuchagiza mchakato wa upatikanaji wake na matumizi ya dawa ambazo bado hazijapatiwa leseni lakini zinahitajika katika dharura ya kitabibu ili kulinda afya ya umma.
Nchi za Afrika zilizochukua Pfizer
Mwezi Februari mwaka huu kampuni ya Pfizer-BioNTech iliridhia mataifa manne ya Afrika ambayo ni Cabo Verde, Rwanda, Afrika Kusini na Tunisia kupokea chanjo yake ya Pfizer. Kwa mujibu wa WHO kanda ya Afrika, Katika kuwasilisha ombi za chanjo hiyo ya Pfizer, nchi zilitakiwa kuwasilisha maombi ambapo nchi 13 ziliwasilisha na maombi yao kufanyiwa tathmini ikiwemo kiwango cha cha vifo kutokana na COVID-19 na uwezo wa kuhifadhi chanjo hizo katika joto la -70°C.
Wito wa WHO kwa nchi zinazochukua chanjo
Nchi lazima ziwe na mkakati wa kitaifa wa utoaji wa chanjo na wakati huo huo mkakati huo ujumuishe uimarishaji wa mnyororo wa kupokea, kuhifadhi na kusambaza chanjo hizo na usimamizi wake n ahata vifaa vinavyotakiwa kama mabomba ya sindano, majokofu na makasha ya kutupia sindano zilizotumika. Usambazaji huo ufikie hadi maeneo ya ndani kabisa ya nchi ili kila mtu anayehitaji kupata chanjo apatiwe.