Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Vifo na uharibifu wa kimbunga Kenneth Comoro na Msumbiji vimenishtua:Guterres

Wilaya ya Macomia jimboni Cabo Delgado nchini Msumbiji limeathirika vibaya na kimbunga Kenneth kilichotua Msumbiji Aprili 25, 2019
OCHA/Saviano Abreu
Wilaya ya Macomia jimboni Cabo Delgado nchini Msumbiji limeathirika vibaya na kimbunga Kenneth kilichotua Msumbiji Aprili 25, 2019

Vifo na uharibifu wa kimbunga Kenneth Comoro na Msumbiji vimenishtua:Guterres

Msaada wa Kibinadamu

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema ripoti za vifo na uharibifu mkubwa uliosababishwa na kimbunga Kenneth nchini Msumbiji na Comoro zimemshtua na kutoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kuongeza msaada wa fedha kukabiliana na mahitaji ya dharura na ya muda mrefu ya waathirika.

Katika taarifa iliyotolewa na msemaji wake hii leo Guterres amesema kimbunga Kenneth kimekuja wiki sita tu baada ya kimbunga kingine kikubwa Idai kilichosambaratisha maisha ya mamilioni ya watu Msumbiji, Malawi na Zimbabwe.

Kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura OCHA hadi sasa watu watato wametripotiwa kupoteza maisha nchini Msumbiji na watatu nchini Comoro.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres
UN
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres

Pia kimbunga hicho kimesababisha uharibifu mkubwa ikiwemo kuharibi asilimia 90 ya nyumba kwenye jimbo la Cabo Delgado nchini Msumbiji, kuezua mapaa ya nyumba, kubomoa madaraja na kuharibu miundombonu mingine ikiwemo nguzo za umeme Comoro na Msumbiji. Na mafuriko zaidi yanatarajiwa Msumbiji.

Katibu Mkuu Guterres ametuma salamu za rambirambi na mshikamano kwa familia za walioathirika, serikali na watu wa Msumbiji na Comoro.

Ameongeza kuwa Umoja wa Mataifa na washirika wa kibinadamu wanazisaidia mamlaka katika kutathmini mahitaji na kutoa msaada.

Katibu Mkuu ametoa ombi kwa jumuiya ya kimataifa kuongeza rasilimali fedha ambazo zinahitajika haraka ili kushughulikia mahitaji ya dharura, ya muda mfupi na ya muda mrefu.

Katibu Mkuu anatarajiwa kuzuru hivi karibuni nchini Msumbiji kufuatia ombi maalum la Rais Filippe Nyusi wa nchi hiyo.