Ubunifu wa spika janja Kaya sasa kuanza kuingia sokoni mwakani
Kila uchao Umoja wa Mataifa unapigia chepuo ushiriki wa vijana katika kuleta mabadiliko katika dunia ya sasa na kuhakikisha mustakabali wa kizazi kijacho unakuwa bora. Umoja wa Mataifa ukitoa wito huo vijana nao wanaitikia kuhakikisha kuwa wanatumia stadi zao kubadilisha maisha ya jamii zao kwa kuzingatia malengo ya maendeleo endelevu, SDGs. Miongoni mwa vijana hao ni Isaya Yunge kutoka Tanzania ambaye ni mwanzilishi mwenza wa kampuni inayotengeneza spika janja, Smart Kaya. Akiwa hapa Umoja wa Mataifa hivi karibuni, Arnold Kayanda wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa alizungumza naye kutaka kufahamu mwelekeo wa spika hiyo ni upi hivi sasa katika kuhakikisha inaanza kusaidia walengwa na zaidi ya yote changamoto walizokumbana nazo. Ni kutokana na mazungumzo hayo basi tumekuandalia makala hii upate ufahamu zaidi.