Muhtasari wa habari: Polio nchini Malawi na Msumbiji, Mauaji Gaza, Nishati safi ya kupikia Afrika
Kufuatia tathmini za kina nchini Malawi na Msumbiji, Timu huru ya Tathmini ya Kukabiliana na Mlipuko wa Polio (OBRA) leo Mei 14 imependekeza kufikia ukomo wa mlipuko wa virusi vya polio aina ya 1 (WPV1) nchini Malawi na Msumbiji, kuashiria hatua muhimu katika mapambano dhidi ya polio katika eneo la Afrika.
Kisa cha mwisho cha WPV1 katika Kanda ya Afrika, kilichohusishwa na aina hiyo ya polio kiliripotiwa katika Jimbo la Tete la Msumbiji mnamo Agosti 2022. Jumla ya wagonjwa tisa waligunduliwa nchini Msumbiji na nchi jirani ya Malawi, ambapo mlipuko huo ulitangazwa Februari 2022. Hatua ilichukuliwa haraka na zaidi ya watoto milioni 50 wamechanjwa dhidi ya virusi hivyo katika nchi 5 za kusini mwa Afrika.
Mauaji Gaza
Huko Gaza Wapalestina zaidi waliouawa kutokana na mashambulizi ya kijeshi ya Israel wakiendelea kutambuliwa na mamlaka ya afya ya eneo hilo, wasaidizi wa kibinadamu wa Umoja wa Mataifa wameeleza tena kwamba kwa hakika katika ya watu 35 ambao wameshauawa, idadi kubwa ya wanawake na watoto. Christian Lindmeier, msemaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani (WHO), amesema idadi hata inaweza kuwa kubwa zaidi kila mwili utakapopatikana na kinachohitajika ni usitishaji mapigano sasa ili kuweza kuipata miili ya watu waliofariki."
Nishati safi ya kupikia
Na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kwa njia ya video leo amewaeleza viongozi wa kimataifa jijini Paris Ufaransa kwamba “Tunahitaji hatua ya haraka ili kumpa kila mtu, kila mahali ufikiaji wa nishati safi ya kupikia.” Guterres amewasisitiza viongozi hao wanaoshiriki Mkutano kuhusu nishati safi ya kupikia barani Afrika kwamba, “Tunacho kichocheo cha mafanikio: Ramani yetu ya Kimataifa ya Ubadilikaji ulio wa haki na jumuishi kuelekea nishati safi ya kupikia.” Na hivyo akawasihi wote kuiweka hiyo “katika vitendo.”