Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Lenacapavir: Dawa mpya ya kujikinga na VVU yawapa matumaini vijana Afrika Kusini

Mtu aliyevaa glavu za bluu huandaa sindano yenye chupa katika mazingira ya kimatibabu.
© UNAIDS Muuguzi aliyevaa glavu zinazotumika mara moja akiandaa sindano na dawa ya lenacapavir ya chanjo ya kudungwa dhidi ya VVU katika kliniki tembezi nchini Afrika Kusini.

Lenacapavir: Dawa mpya ya kujikinga na VVU yawapa matumaini vijana Afrika Kusini

Afya

Kwa mara ya kwanza, mtu anaweza kujikinga na Virusi Vya Ukimwi, VVU, kwa sindano moja tu kila baada ya miezi sita  bila kumeza kidonge kila siku. Dawa hiyo iitwayo Lenacapavir.

Dawa hii imeonesha ufanisi wa zaidi ya asilimia 96 katika kuzuia maambukizi, sasa imeanza kutolewa katika nchi tisa barani Afrika, ikiwemo Afrika Kusini, nchi yenye idadi kubwa zaidi duniani ya watu wanaoishi na VVU. Lakini je, dawa hii itawafikia wote wanaoihitaji? 

Katika kijiji cha Philippi, viungani mwa jiji la Cape Town nchini Afrika Kusini. Picha zilizopigwa kutoka juu zinaonesha chini nyumba za mabati zikiwa zimesongamana, na katikati ya eneo la maegesho ya magari, kliniki tembezi zimepangwa. Nje ya mlango kuna bango lililoandikwa, "FAST PrEP – usichelewe, jikinge leo."

Mfanyakazi wa afya mwanamke mweusi mwenye nywele zilizosokotwa na sare ya bluu akiwa na epauleti za rangi ya hudhurungi akizungumza katika mazingira ya kliniki, huku mabango ya taarifa za kimatibabu yakiwa ukutani nyuma yake.
© UNAIDS Zimasa Zwide, muuguzi katika Kliniki tembezi ya Kijiji cha Philippi nchini Afrika Kusini, anazungumzia umuhimu wa VVU na chanjo.

Ndani ya kliniki hiyo, muuguzi amevaa glavu, akiandaa sindano. Kwenye meza kando yake kuna kijitabu cha kinga, vipeperushi na kisanduku cha dawa.

Muuguzi Zimasa Zwide, anayefanya kazi katika kliniki hiyo tembezi ya Philippi, anaeleza kwa nini kinga hii ya VVU ni muhimu hasa kwa wasichana na wanawake vijana.

"Kuna wimbi kubwa la ukatili wa kijinsia, ambapo wanawake vijana wanashambuliwa, na wengi wao wanajikuta katika hatari ya maambukizi kupitia ubakaji. Kwa hiyo tunawahimiza wajikinge muda wote, ili hata kama mtu akibakwa, angalau kwa upande wa VVU awe salama zaidi."

Mratibu wa Mawasiliano wa Taasisi ya Afya ya Desmond Tutu, Mbali Jonas, anasema jamii imepokea habari hii kwa shauku kubwa kwani, "Kuna furaha kubwa sana ndani ya jamii. Sindano hii ya LEN imetambulika kama mabadiliko makubwa katika kukabiliana na janga la VVU, hasa kwa vijana, kwa sababu inakupa usiri.Unapata sindano mbili kwa mwaka, na umemaliza."

Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa akizungumza jukwaani wakati wa hafla ya UNAIDS.
© UNAIDS Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa akizungumza katika hafla ya UNAIDS iliyoandaliwa kwa ajili ya kuzindua chanjo ya kwanza dhidi ya HIV, lenacapavir.

Nje ya kliniki, kundi la vijana limekaa kwenye mkutano wa elimu ya afya na kinga dhidi ya VVU, mkutano ukiongozwa na Sive Mphambaniso. 

Wanawake wanne wananyoosha mikono, wawili kati yao ni miongoni mwa waliokwisha kupata Lenacapavir (dawa ya muda mrefu ya kuzuia na kutibu maambukizi ya VVU). 

Wanajadiliana kwa sauti, wakiulizana maswali. Lakini Mphambaniso anasema bado kuna pengo kubwa la uelewa."Ninapokwenda kwenye jamii, nikiwaeleza watu mambo haya, wengine wanashangaa sana. Naamini hawana taarifa za kutosha kama inavyopaswa. Kwa sababu baadhi ya watu wanajihusisha na ngono bila kujua kinachoweza kutokea, wala madhara ya ngono zisizo salama. Na njia zote hizi tulizo nazo, wengi wao hawazijui."

Hapa ndipo penye changamoto. Afrika Kusini ina watu milioni nane wanaoishi na VVU, na kila mwaka bado kunakuwa na maambukizi mapya yanayofikia takriban laki moja na sabini elfu. Lakini dozi zilizopo kwa sasa ni laki nne na hamsini elfu tu.

Mkurugenzi wa Kituo cha VVU cha Desmond Tutu, Profesa Linda-Gail Bekker, anasema hilo linaibua swali zito kwani "Hili linaibua swali kubwa. Hii ni nchi ambayo watu milioni nane wanaishi na VVU. Bado tunaona maambukizi mapya yapatayo laki moja na themanini elfu kila mwaka. Tunahitaji kuifikisha kinga hii kwa watu wengi zaidi ya laki nne na hamsini elfu. Kwa hiyo, itabidi tuwe wachaguzi kuhusu nani apate Lenacapavir."

Anaendelea akisema kwamba, "Ni ile hali ya hatua ya mwisho  tunapoanza kulizima janga hili, ni lazima uwafikishie kinga watu wengi zaidi na zaidi. Na hilo linazua swali kubwa la uendelevu. Kwa maoni yangu, njia pekee ya kuweza kufanya hivi ni kama tutapata bei nafuu kabisa, inayoweza kuenea, na yenye tija."
Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa akizungumza kwenye jukwaa wakati wa hafla ya hadhara ya chanjo ya kuzuia VVU ya Lenacapavir.
© UNAIDS Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa akizungumza katika hafla ya hadhara ya UNAIDS wakati wa uzinduzi wa chanjo ya VVU ya Lenacapavir.

Tunahamia mji wa Secunda, jimbo la Mpumalanga. Umati umejaa nje ya kliniki, ukisubiri kuwasili kwa Rais wa Afrika Kusini na Waziri wa Afya, kwa ajili ya uzinduzi rasmi wa Lenacapavir. Rais Cyril Ramaphosa anapanda jukwaani na kusema, "Usalama wa afya hauwezi tena kutenganishwa na maendeleo ya kiuchumi. Uwezo wa kubuni, kutengeneza na kusambaza dawa ni jambo la msingi kwa mamlaka yetu, ustahimilivu wetu na ustawi wetu. Kwa hiyo tuwe wazi  Lenacapavir si suluhisho la kila kitu. Ni silaha moja zaidi yenye nguvu katika ghala letu."

Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Gilead Sciences inayotengeneza dawa hiyo, Daniel O'Day, anasema kasi ya kuifikisha dawa hii barani Afrika haijawahi kushuhudiwa.

"Lenacapavir ni dawa mpya ya kwanza ya aina yake ya VVU kufika nchi za Afrika zilizoko kusini mwa Jangwa la Sahara katika mwaka ule ule ilipoidhinishwa Marekani. Hili halijawahi kufanyika. Na hili ni jambo ambalo sisi Gilead tulidhamiria kulifikia mara tu tulipojua ufanisi wa Lenacapavir katika kutokomeza VVU."

Mwakilishi wa UNAIDS nchini Afrika Kusini, Alankar Malviya, anasisitiza kuwa dawa hii ni sehemu tu ya mkakati mpana kwa kuwa "Inatupatia mojawapo ya njia bora zaidi za kuwalinda vijana dhidi ya maambukizi mapya. Lakini kwa kuwa itatolewa kwa awamu, ni muhimu kutambua kuwa hii ni sehemu ya zana nyingi tulizo nazo za kuzuia maambukizi mapya, sambamba na kondomu, vidonge vya kujikinga na njia nyingine, ili kufikia lengo la kutokomeza Ukimwi ifikapo mwaka 2030."

Video inahitimisha kwa picha ya Rais akiwa na Waziri wa Afya wakiinua masanduku ya dawa ya Lenacapavir juu, huku umati ukishangilia. Matumaini ni makubwa lakini swali la bei, uzalishaji na usambazaji bado liko wazi.