Mafunzo ya STEM yawezesha vijana Zanzibar kuongezea thamani zao la mwani
Je, ingekuwaje kama kila kijana kutoka visiwa vya Zanzibar nchini Tanzania angeweza kugeuza zao la mwani kuwa suluhisho la kiuchumi la kesho yake? Hilo ndilo lengo mradi wa shirika la kiraia la ProjeKt Inspire kupitia programu yake ya Girls in STEM, au Wasichana kwenye masomo ya Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati, unaoungwa mkono na Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF kwa ufadhili wa Canada.
Kupitia warsha wa siku tatu ya masomo ya STEM, wanafunzi wamejifunza kutumia masomo hayo kuongeza thamani ya zao la mwani na kuendeleza Uchumi wa buluu.
Kwanza utajiuliza Uchumi wa buluu ni nini? Huu ni uchumi utokanao na mazao ya baharini ambalo mwani ni mojawapo. Sasa tuendelee na video iliyoandaliwa na UNICEF inayoanza kwa kuwaonesha wanafunzi wakivuna mwani baharini kabla ya kurejea katika maabara kuuchakata na kutoa biopolima asilia. Hizi ni molekuli zinazofanana na plastiki.
Lengo kuu la mafunzo hayo ni kuwajengea vijana uwezo wa kutumia sayansi kutatua changamoto zinazowakabili wakulima wa mwani na kuongeza thamani ya zao hilo. Max George ni meneja wa Projekt Inspire, anaeleza umuhimu wa mradi huu.
"Mwani ni zao muhimu sana Zanzibar. Vijana wengi wanajishughulisha na kilimo hiki, lakini pia ni zao linalowanufaisha zaidi wanawake kwani wengi wa wanaolima mwani ni wanawake. Ndio maana tumeona umuhimu wa kuwafundisha vijana wetu, na asilimia kubwa ya washiriki wa kambi hii ni mabinti."
Kutokana na mafunzo hayo, wanafunzi walitumia utafiti na majaribio kubuni bidhaa mbalimbali zinazotokana na mwani, wakigeuza maarifa ya darasani kuwa majawabu ya changamoto za maisha ya kila siku. Aifat K. Mwalimu ni mwanafunzi wa Sayansi ambaye ni mshiriki wa mradi huu..
"Katika darasa letu la sayansi tumetengeneza bidhaa mbili kutokana na unga wa mwani. Tulitengeneza sabuni na shampoo. Hivyo tunaweza kujiita wajasiriamali na wanasayansi kwa sababu tumegundua namna ya kutengeneza bidhaa zinazoweza kutumika majumbani na katika jamii."
Mbali na kutengeneza bidhaa, baadhi ya washiriki walibuni majawabu ya kidijitali ya kuwasaidia wakulima wa mwani kupata taarifa muhimu na masoko kwa urahisi zaidi. Sofia S. Suleiman ni mwanafunzi wa teknolojia, anaeleza jinsi wanavyotumia akili mnemba kuendesha shughuli za utafiti wa kilimo cha mwani.
"Tumebahatika kutengeneza programu tunayoiita Seaweed Farming Chatbot App, ambayo inalenga kuwasaidia wakulima wa mwani kupata taarifa za kilimo, kuboresha uzalishaji wao, pamoja na kupata masoko na wateja."
Changamoto ya ukaushaji wa mwani baada ya mavuno pia lilipata jawabu kupitia ubunifu wa kiteknolojia ulioanzishwa na wanafunzi hao. Ilham F. Bakari, Mwanafunzi wa uhandisi anaeleza zaidi.
"Tumeona wakulima wa mwani wanapata changamoto kubwa baada ya kuvuna kwa sababu hali ya hewa hubadilika mara kwa mara. Kwa hiyo tumetengeneza kifaa kinachoitwa Smart seaweed dry Machine kitakachosaidia kukausha mwani kwa ufanisi."
Washiriki wengine walitumia maarifa ya hisabati na uchambuzi wa takwimu kubaini vipindi vinavyofaa zaidi kwa kilimo cha mwani ili kuongeza uzalishaji mwaka mzima kama anavyoeleza Mwanafunzi huyu wa somo la hisabati Raudhat J. Said..
“Katika miezi 12 ya mwaka, kila mwezi una hali ya hewa tofauti. Kwa hiyo, tumetumia hisabati ili kubaini ni mwezi gani kati ya miezi hiyo unafaa zaidi kwa ajili ya kulima na kuvuna zao la mwani."
Kupitia mradi huu, vijana wamejifunza kufikiri kwa ubunifu, kufanya kazi kwa ushirikiano na kutumia sayansi kutatua changamoto za jamii.