Idadi ya wagonjwa wa saratani duniani kuongezeka maradufu ifikapo 2050
Idadi ya wagonjwa wa saratani duniani kuongezeka maradufu ifikapo 2050
Kasi ya hatua dhidi ya saratani inabidi iongezeke haraka hivi sasa kwani idadi ya wagonjwa wa saratani inatarajiwa kuongezeka maradufu miaka 24 ijayo, limesema shirika la Umoja wa Mataifa la Afya duniani, WHO.
Kupitia ripoti ya Hali ya Saratani duniani ya mwaka 2026, iliyotolewa leo Geneva, Uswisi, WHO na shirika lake tanzu la utafiti wa saratani, (IARC), wanasema kwa sasa duniani kila mwaka kuna wagonjwa wapya milioni 20.6 na takribani vifo milioni 10.
Huduma za saratani bado hazijafikiwa kwa usawa
Kuna tofauti kubwa baina ya nchi:
- Katika upatikanaji wa kinga,
- Uchunguzi wa mapema,
- Matibabu na huduma za uangalizi.
- Asilimia 87 ya wanawake wenye saratani ya titi katika nchi zenye kipato cha juu huishi angalau miaka mitano baada ya kugunduliwa na ugonjwa huo
- Katika nchi za kipato cha chini ni wanaoishi baada ya kubaini ni asilimia 42
- Nchi zilizojumuisha saratani kwenye huduma za afya kwa wote ni chini ya theluthi moja.
Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus, amesema tofauti hizo si jambo lisiloepukika bali ni matokeo ya maamuzi ya sera, akisisitiza kuwa kila mtu anapaswa kuwa na fursa sawa ya kupata huduma za saratani bila kujali mahali alipozaliwa au kipato chake.
Unyanyapaa ni 'mwiba' asema manusura wa saratani ya titi
Abigael Hartz mkazi wa Ireland lakini anatokea Nigeria anasimulia alichoshuhudia alipotembelea hospitali moja ya kupima saratani Nigeria. “Wagonjwa wengi niliokutana nao walikuwa tayari katika hatua za mwisho za ugonjwa. Baada ya kufanyiwa upasuaji wa kuondolewa matiti yote mawili, mimi nilikabiliwa na changamoto ya kujikubali kutokana na mabadiliko ya mwili wangu. Hata hivyo, nilijua kwamba upasuaji huo ulikuwa umenipa nafasi bora zaidi ya kuendelea kuishi. Lakini nilikutana na wanawake wanne ambao walichagua kufa badala ya tiba ya kuondolewa titi. Hayo ndio matokeo ya kutisha ya unyanyapaa. Nilitambua kwamba sikuweza kuendelea kubaki pembeni nikitazama tu. Ndiyo maana mwaka 2016 nilishirikiana kuanzisha Bricon Foundation, ili kuwasaidia watu wanaoishi na saratani pamoja na familia zao.”
Kinga na uwekezaji vinaweza kupunguza mzigo wa saratani
- Wagonjwa 4 kati ya 10 wanahusishwa na vihatarishi vinavyoweza kuzuilika
- Matumizi ya tumbaku na pombe
- Unene kupita kiasi
- Kutofanya mazoezi ya mwili
- Maambukzi ya virusi vya papilomo, (HPV), homa ya ini aina B na C.
Ingawa matumizi ya tumbaku yamepungua kwa asilimia 27 tangu mwaka 2010 na nchi nyingi zimeanzisha mipango ya kitaifa ya kudhibiti saratani, WHO inasema maendeleo hayo bado hayajatosha kutokana na upungufu wa dawa muhimu na huduma katika nchi zenye kipato cha chini.
Nini kifanyike?
- Serikali ziunganishe huduma za saratani katika huduma za afya kwa wote,
- Kuongeza uwekezaji katika kinga, matibabu na utafiti,
- Kuwashirikisha watu wanaoishi na saratani katika kupanga sera ili kupunguza mzigo wa ugonjwa huo kwa vizazi vya sasa na vijavyo.