Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ripoti ya IOM: Uhamiaji unachochea uchumi na maendeleo, lakini mafanikio yako hatarini

Mwanamke kutoka Amerika ya Kusini, amevaa mkoba na mifuko, anatembea nje huku milima ikiwa nyuma yake.
© IOM Watu wanaendelea kuhama katika muktadha wa kimataifa unaozidi kutokuwa na uhakika.

Ripoti ya IOM: Uhamiaji unachochea uchumi na maendeleo, lakini mafanikio yako hatarini

Wahamiaji na Wakimbizi

Ripoti mpya ya Shirika laUmoja wa Mataifa la Uhamiaji (IOM) inaonesha kuwa upatikanaji wa njia salama, za mpangilio na za kawaida za uhamiaji unaendelea kuchangia ukuaji wa uchumi, maendeleo na utulivu duniani. 

Matokeo hayo yalitolewa wakati wa Wiki ya Jukwaa la Mapitio ya Uhamiaji ya Kimataifa (IMRF) mjini New York, yakionesha uhamiaji kama kichocheo kikuu cha maendeleo ya dunia.

Ripoti ya “Ya dunia ya uhamiaji 2026” inaonya kuwa kupunguza njia halali za uhamiaji hakuzuii watu kuhama, bali huwasukuma kutumia njia zisizo rasmi na hatarishi zaidi. 

Hali hiyo huongeza hatari kwa wahamiaji, huongeza gharama kwa mataifa na kupunguza manufaa makubwa ya kiuchumi na kijamii ya uhamiaji.

Uhamiaji bado ni nguvu kubwa ya kiuchumi duniani

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kufikia katikati ya mwaka 2024 kulikuwa na wahamiaji wa kimataifa takribani milioni 304, sawa na asilimia 3.7 ya watu duniani. 

Idadi ya wafanyakazi wahamiaji pia imeongezeka kwa zaidi ya milioni 30 kati ya mwaka 2013 na 2022, ikionesha nafasi kubwa ya uhamiaji katika soko la ajira la kimataifa.

Ripoti imeongeza kuwa mchango wa kifedha kutoka kwa wahamiaji bado ni tegemeo kubwa kwa nchi nyingi. 

Fedha zinazotumwa nyumbani zilitarajiwa kufikia takribani dola bilioni 905 mwaka 2024, ikiwa ni pamoja na dola bilioni 685 kwenda nchi zenye kipato cha chini na cha kati kiasi kinachozidi misaada rasmi ya maendeleo na uwekezaji wa moja kwa moja wa kigeni kwa pamoja.

Mfanyakazi wa misaada wa IOM anapiga magoti kuzungumza na wanawake wawili waliohamishwa wakiwa wamevaa hijabi kwenye mlango wa ofisi ya uwanja wa IOM katika kambi ya wakimbizi nchini Sudan.
© IOM Mfanyakazi wa Shirika la Kimataifa la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji atoa msaada kwa mwanamke nchini Sudan.

Tofauti za fursa za uhamiaji na ongezeko la wakimbizi

IOM inaonya kuwa fursa za uhamiaji bado hazilingani, ambapo watu kutoka nchi tajiri wana upatikanaji mkubwa wa njia halali, huku wale kutoka nchi maskini wakikabiliwa na vizuizi zaidi. 

Wakati huohuo, ripoti imebainisha kuwa idadi ya watu waliokimbia makazi yao imefikia viwango vya juu, ikiwa zaidi ya milioni 120 kufikia mwisho wa 2024 kutokana na migogoro, athari za mazingira na udhaifu wa kimuundo.

Wito wa ushirikiano na mifumo bora ya uhamiaji

“Duniani kote, uhamiaji unasaidia ajira, ukuaji wa uchumi, utulivu na mshikamano wa kijamii,” amesema Mkurugenzi Mkuu wa IOM Amy Pope. Amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya nchi husababisha usimamizi bora wa uhamiaji na matokeo mazuri zaidi. 

Ripoti inatoa wito wa kupanua njia salama za uhamiaji, kupunguza gharama za kutuma fedha, kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kutumia sera zenye ushahidi ili kuhakikisha uhamiaji unaendelea kunufaisha watu na uchumi.