Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

FAO : Njaa yaongezeka duniani, watu milioni 266 wakikabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula

Mtoto mdogo mwenye ngozi nyeusi anapimwa kwa ajili ya utapiamlo katika kliniki ya lishe inayoungwa mkono na UNICEF huko Juba, Sudan Kusini. Mikono ya mfanyakazi wa afya inaonyeshwa ikifunga mkanda wa rangi za MUAC (Mid-Upper Arm Circumference) kuzunguka mkono wa juu wa mtoto ili kutathmini hali yake ya lishe.
© UNICEF/Mark Naftali Mfanyakazi wa afya anamchunguza mtoto kuthibitisha utapiamlo kati ya watoto kufuatia njaa kali.

FAO : Njaa yaongezeka duniani, watu milioni 266 wakikabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula

Msaada wa Kibinadamu

Ripoti mpya ya kimataifa ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo FAO iliyotolewa leo 24 Aprili 2026 imebaini kuongezeka kwa mgogoro wa njaa duniani, huku zaidi ya watu milioni 266 katika nchi na maeneo 47 wakikabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula.

Ripoti hiyo ya Kimataifa kuhusu Migogoro ya Chakula (GRFC) iliyozinduliwa lmjini Roma Italia inaonyesha kuwa mwaka 2025 ulishuhudia viwango vya pili vya juu zaidi vya njaa kali kuwahi kurekodiwa, jambo linaloashiria hali mbaya na ya muda mrefu.

Mgogoro mkubwa na wa muda mrefu

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kiwango cha njaa si kikubwa tu bali pia kinaongezeka kwa ukali na kudumu kwa muda mrefu.

“Tuna hali ambapo jumla ya watu milioni 266 katika nchi na maeneo 47 wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula. Lakini kinachotutia wasiwasi zaidi ni kiwango cha ukali na muda mrefu wa hali hii,” amesema Rein Paulsen, Mkurugenzi wa Ofisi ya Dharura na Mnepo wa FAO.

Ripoti inaonesha kuwa karibu nusu ya maeneo yenye migogoro ya chakula pia yanakabiliwa na matatizo ya lishe, yanayosababishwa na mchanganyiko wa lishe duni, magonjwa, na kuporomoka kwa huduma muhimu.

Familia moja ya wahamiaji kutoka Myanmar wanakimbilia ndani ya hema la muda huko Sagaing kufuatia tetemeko la ardhi la Machi 2025. Mwanamke wa Asia na msichana mdogo wanaonyeshwa wakiandaa mboga kwenye godoro ndani ya makao yaliyojaa fujo.
© WFP/Htet Oo Linn Huko Myanmar, kuongezeka kwa bei hasa kunaathiri maeneo ya mbali yaliyopigwa na migogoro na kuathiri sana nchi ambayo bado inajaribu kutokea baada ya tetemeko la ardhi la mwaka jana.

Watoto waathirika zaidi wa utapiamlo unaoongezeka

Ripoti inaonesha hali mbaya kwa watoto, ambapo watoto milioni 35.5 walikumbwa na utapiamlo mkali mwaka 2025 pekee karibu milioni 10 kati yao wakiwa katika hali mbaya zaidi ya utapiamlo inayohatarisha maisha.

Katika maeneo yaliyoathirika zaidi kama Gaza, Myanmar, Sudan Kusini, Sudan, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC migogoro iliyojikutanisha imewasukuma watu karibu na hatari kubwa ya vifo, hasa kwa walio katika mazingira hatarishi zaidi.

Uhaba wa takwimu waficha ukubwa halisi wa tatizo

Licha ya takwimu hizi za kutisha, FAO inaonya kuwa hali halisi inaweza kuwa mbaya zaidi kutokana na mapungufu ya ukusanyaji wa takwimu.

“Hatuoni maboresho katika hali ya uhaba wa chakula. Tunachoshuhudia ni mapengo ya takwimu,” ameeleza Paulsen.

“Pale ambapo kuna upungufu wa takwimu, hatuwezi kuelewa kikamilifu mahitaji na hali hii itadhoofisha juhudi zetu za pamoja za kuboresha uhakika wa chakula.”

Shirika hilo linasisitiza kuwa takwimu sahihi ni muhimu ili kupanga na kutekeleza hatua madhubuti za kukabiliana na tatizo hili.

Baa la njaa lathibitishwa Gaza na Sudan

Katika mojawapo ya matokeo ya kutisha zaidi, ripoti imethibitisha kuwepo kwa baa la njaa katika maeneo mawili Gaza na Sudan ndani ya mwaka mmoja, jambo ambalo halijawahi kushuhudiwa mara nyingi.

“Baa la njaa limethibitishwa katika maeneo mawili tofauti, Ukanda wa Gaza na Sudan na hii ni hali ya kutia wasiwasi mkubwa. Baa la njaa linahusiana moja kwa moja na migogoro,” ameonya Paulsen.

Mapigano yanayoendelea, mabadiliko ya tabianchi na hali tete ya uchumi wa dunia vinaendelea kuzidisha tatizo hili.

Mtoto anayesumbuliwa na utapiamlo mkali anashikiliwa na mtu mzima.
UN News Mtoto mdogo Misk Al-Madhoun anaugua utapiamlo mkali.

Upungufu wa ufadhili watishia juhudi za kukabili migogoro

Ripoti pia inaonesha kuwa kupungua kwa ufadhili wa kibinadamu kunadhoofisha juhudi za kukabiliana na njaa. FAO inasisitiza kuwa mchanganyiko wa misaada ya chakula na kusaidia uzalishaji wa kilimo ni njia yenye ufanisi zaidi.

“Tunapoziunganisha njia hizi ipasavyo, matokeo chanya katika uhakika wa chakula yanaweza kuwa mara 17 zaidi kuliko kutoa msaada wa chakula pekee,” amesema Paulsen.

Wakati mahitaji yakiongezeka na rasilimali zikipungua, FAO inatoa wito wa hatua za haraka na za pamoja ili kuzuia hali isizidi kuwa mbaya na kuimarisha mifumo ya chakula duniani.