Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

China na Urusi zapinga rasimu ya azimio ya kufanikisha safari mlango wa baharí wa Hormuz

Picha kubwa ya chumba cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ikionyesha wawakilishi wameketi kuzunguka meza kubwa ya duara, na wanachama kadhaa wakiinua mikono yao kupiga kura.
Picha ya UN/Manuel Elías Mkutano wa Baraza la Usalama: Wajumbe kuhusu rasimu ya azimio linaloongozwa na Bahrain la Mlango wa Hormuz

China na Urusi zapinga rasimu ya azimio ya kufanikisha safari mlango wa baharí wa Hormuz

Amani na Usalama

Rasimu ya Azimio iliyowasilishwa mbele ya wajumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa lengo la kuchagiza nchi zinazotumia mlango wa bahari wa Hormuz kuchangia katika kuhakikisha usalama wa meli zenye bidhaa za kibiashara zinazotumia mlango huo, imegonga mwamba baada ya Urusi na China kuipinga kwa kutumia kura turufu licha ya kura 11 za ndio.

Bahrain ndiyo iliyowasilisha rasimu hiyo iliyokuwa inaungwa mkono na nchi za Ghuba ambazo ni Kuwait, Qatar, Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu, (UAE) pamoja na Jordan.

Mchanganuo wa kura unaonesha kuwa wajumbe 11 walipiga kura za ndio ambao ni  Bahrain, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, (DRC), Denmark, Ufaransa, Ugiriki, Latvia, Lberia, Panama, Somalia, Uingereza na Ufaransa.

Kura mbili za hapa ni kutoka Urusi na China ambazo zina kura turufa, ilhali wajumbe wawili amba oni Colombia na Pakistan hawakuonesha msimamo wowote.

Usalama  unaozungumzwa ni pamoja na kusindikiza meli za biashara huku rasimu iliitaka Iran iache mara moja mashambulizi dhidi ya vyombo vya baharini vya  kibiashara na jaribio lolote lile la kuzuia meli kupiga kambi kwa muda na vile vile kuacha kushambulia miundombinu ya kiraia, kama vile maji, mitambo ya kuondoa chumvi kwenye maji na mitambo ya mafuta na gesi.

Sababu ya Urusi kupiga kura ya Hapana

Mwakilishi wa Kudumu wa Urusi kwenye Umoja wa Mataifa Balozi Vassily Nebenzia, amesema wamepinga rasimu kwa kuwa “ilikuwa na mbinu yenye makosa ya kimsingi na hatari kuhusu hali katika eneo hilo.”
Amesema “rasimu  hiyo imemulika Iran kama chanzo pekee cha mvutano wa kikanda na kwamba mashambulizi haramu ya Marekani na Israel hayakutajwa kabisa.”
 
Akisisitiza kwamba athari za azimio hilo “ziko wazi kwetu”, amewakumbusha wajumbe wa Baraza kile ambacho “tafsiri isiyo na mipaka na iliyo pana” ya azimio 1973 (2011) ilisababisha nchini Libya.
 
Balozi Nebenzia amesema kuwa Urusi na China hivi karibuni zitapendekeza azimio mbadala, akiongeza “rasimu yetu itakuwa fupi, ya haki na yenye uwiano.”

Na China je?

Balozi Fu Cong, ambaye ni Mwakilishi wa Kudumu wa China kwenye Umoja wa Mataifa amesema “rasimu ya azimio ilishindwa kuwasilisha chanzo cha msingi na taswira kamili ya mgogoro kwa njia ya kina na yenye uwiano.”
 
Amesisitiza kuwa Baraza la Usalama halipaswi kukimbilia kupiga kura juu ya rasimu ya azimio wakati kuna wasiwasi mkubwa umeibuliwa na wanachama.
 
Ameeleza ni matumaini yake kwamba amani na utulivu vitarejeshwa na akathibitisha dhamira ya China ya kushughulikia hali hiyo ipasavyo kwa kushughulikia sababu zake za msingi.
 
Balozi Fu amesema, “vita hivi havikupaswa kamwe kutokea,” akilaumu Marekani na Israel kama wachochezi na kuwataka wasitishe kile alichokiita vitendo vya kijeshi visivyo halali.
 
Halikadhalika amesisitiza kwamba msimamo wa China ni wa lengo na wenye uwiano, na akaiomba Iran kusitisha mashambulizi yake.