Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Leo ni siku ya elimu duniani: Vijana ndio injini elimu wakati wa majanga

Wasichana watatu wenye tabasamu wakiwa na ishara kwa ajili ya kampeni ya 'Like Your Sister' shuleni wakipigania maeneo ya haki ya jinsia na yasiyo na vurugu katika shule.
© Informed Future Generations
Wasichana wakiendesha kampeni ya elimu jumuishi na utekelezaji wa usawa wa kijinsia katika elimu.

Leo ni siku ya elimu duniani: Vijana ndio injini elimu wakati wa majanga

Utamaduni na Elimu
  • Dunia itege sikio kusikiliza vijana wabunifu kwenye sekta ya elimu.
  • Tujenge mifumo ya elimu bunifu na jumuishi
  • Vijana si wapokeaji tu wa elimu bali ni wabunifu wa mustakabali wao

Leo dunia inaadhimisha siku ya elimu maudhui yakiwa uwezo wa vijana katika kuongoza mabadiliko ya mifumo ya kujifunza.

Jacques Kwibuka, mfanyakazi wa kujitolea wa UNICEF, anapiga makofi kwa shauku kwenye tukio la mtandao wa elimu.
© Vizazi vya Baadaye Vinavyojifunza
Jacques Kwibuka anashiriki katika tukio la mtandao wa UNICEF.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres pamoja na shirika la Education Cannot Wait linaloungwa mkono na Umoja wa Mataifa katika kutoa elimu kwenye maeneo yenye dharura wametoa ujumbe ukijikita kwenye uwezo huo wa vijana na ubunifu kwenye sekta ya elimu.

Akizungumzia kauli mbiu hiyo ya mwaka huu kupitia ujumbe wake uliochapishwa kwenye wavuti mahsusi wa siku hii, Katibu Mkuu Guterres amesisitiza umuhimu wa ulimwengu kutega sikio na kusikiliza kile ambacho vijana wenyewe wanahitaji ili kufanikiwa katika ulimwengu wa sasa.

"Tunahitaji hasa kusikiliza sauti za vijana wenyewe, na kufanyia kazi maombi yao ya kupata walimu wabobevu, ujuzi na mafunzo ya umahiri yanayoendana na ulimwengu unaobadilika, pamoja na usawa katika matumizi ya teknolojia," amesisitiza Guterres.

media:entermedia_image:41e615cd-cd8a-4f56-838e-752a3afc03da
© World Bank & ICAR
Wanafunzi wakitumia teknolojia katika mafunzo.

Kuelekea mifumo ya kibunifu

Guterres amemalizia kwa kutoa wito wa ushirikiano wa kimataifa katika kujenga mifumo ya elimu ambayo ni jumuishi, thabiti, na inayotumia ubunifu wa hali ya juu ili kuhakikisha hakuna kijana anayeachwa nyuma.

Soma ujumbe mzima wa Guterres hapa

Vijana si wapokeaji pekee wa elimu bali wabunifu

Kwa Education Cannot Wait, msisitizo mkubwa umewekwa kwenye umuhimu wa kuwashirikisha vijana sio tu kama wapokeaji wa elimu, bali kama wabunifu wa mustakabali wao.

Katika taarifa  iliyotolewa jijini New York, Marekani, (ECW), inasema kuwa vijana ni washirika muhimu na wenye nguvu katika kubuni mifumo ya elimu, hususan katika maeneo yanayokabiliwa na majanga na dharura.

Mtoto mchanga katika shati la bluu anakunywa kikombe kijani katika chumba cha darasa, akiwa amezungukwa na watoto wengine. Picha hii inachukua wakati kutoka kwa mpango wa maendeleo ya utoto wa mapema unaoungwa mkono na UNICEF katika Wilaya ya Burera, Rwanda.
© UNICEF/Habib Kanobana
Mtoto mdogo anahudhuria shule katika Wilaya ya Burera, Rwanda.

Uongozi wa vijana katika maamuzi

Ushiriki wa vijana unatajwa kuwa injini ya uvumbuzi na mabadiliko ya kijamii na ndio maana kupitia muundo wake wa uongozi, ECW inahakikisha vijana ikiwa ni pamoja na wale walioko kwenye kambi za wakimbizi, wanashiriki kikamilifu katika kufanya maamuzi, kupanga programu za elimu, na kuchangia mawazo ya kibunifu yanayosaidia kujenga mifumo ya elimu inayohimili dharura.

Kwa kina soma taarifa ya ECW hapa.