Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mscan yawezesha wajawazito waishio maeneo ya ndani zaidi Uganda kupata huduma za uchunguzi

Mwanamke mmoja nchini Uganda anapata uchunguzi wa ultrasound wakati wa programu ya afya ya uzazi inayoungwa mkono na WHO.
© WHO
Huduma ya ultrasound inayoungwa mkono na WHO kwa ajili ya afya ya mama nchini Uganda

Mscan yawezesha wajawazito waishio maeneo ya ndani zaidi Uganda kupata huduma za uchunguzi

Afya

Baada ya kuhitimu shahada ya udaktari nchini mwake Uganda, huko Afrika Mashariki, Daktari mmoja alibaini kuwa hiyo haitoshi, bali alienda mbali zaidi kubuni kifaa kinachosaidia wajawazito hasa wale wanaoishi maeneo ya ndani zaidi kufahamu hali ya afya ya watoto wao tumboni, na hivi sasa kifaa hicho kinaelekea kupata hakibunifu kupitia shirika la Umoja wa Mataifa la Hakibunifu, WIPO.

Katika simulizi hii iliyochapishwa katika ukurasa wa Youtube wa WIPO, ndani ya chumba cha daktari, muuguzi akitumia kifaa kidogo kuzunguka juu la tumbo la mjamzito ili kupata picha ya mtoto aliyemo tumboni ili kufahamu maendeleo yake. Kifaa kimeunganishwa kwenye kompyuta mpakato na ndiko muuguzi anatazama ili aweze kufahamu hali halisi.

Mbunifu wa kifaa hiki ni Daktari Prosper Hembisibwe ambaye pia ni Muasisi mwenza na Afisa Mtendaji Mkuu mwenza wa kampuni ya MScan iliyobuni kifaa hiki.

“Katika Mscan Uganda tunatengeneza mashine hizi za bei nafuu za kupata picha za ndani ya mwili au ultrasound na zinazobebeka, ambazo unachohitaji ni mama mjamzito popote alipo.”

Mfanyakazi mmoja wa afya nchini Uganda, akiwa amevaa blazer nyeusi na shati nyeupe ya polo na pini ya bendera ya Uganda, anasimama nje mbele ya jengo lenye miti kwenye mandhari.
© WHO
Daktari Prosper Hembisibwe ambaye pia ni Muasisi mwenza na Afisa Mtendaji Mkuu mwenza wa kampuni ya MScan iliyobuni kifaa cha Ultrasound kwa ajili ya afya ya uzazi nchini Uganda.

Je ni kwa nini waliamua kubuni kifaa hiki?

« Changamoto ni kwamba maeneo ya vijijini—hasa mikoani—tunajua kuwa vituo vingi vya afya nchini Uganda havijaunganishwa na umeme wa gridi, na mashine kubwa za kawaida ni nzito sana na ghali. Kwa hiyo Mscan iligundua kuwa tulihitaji kutengeneza kifaa kinachobebeka, kinachotumia nishati kidogo, na kinachoweza kukidhi hitaji hilo.”

Na ndoto yake ni nini?

“Ndoto yangu kwa Mscan ni kuwafikia kila mama mjamzito barani Afrika ili waweze kufurahia ujauzito wenye hali nzuri na wenye utu. Hakuna mama anayepaswa kufa, bila kujali hali yake ya kijamii na kiuchumi, wakati wa kuleta binadamu duniani.”

Na tayari manufaa ya kifaa hiki ni dhahiri.

“Nilipata fursa mwaka 2022 kumwona mjamzito ambaye mtoto wake alikuwa amejiviringisha kitovu mara tatu shingoni mwake. Tulishuhudia mtoto huyo akizaliwa. Mama huyo alikuwa amefanyiwa uchunguzi wa Mscan. Kwangu, hiyo ilikuwa moja ya nyakati zilizogusa moyo sana kwetu kama biashara yenye faida kijamii.”

Tayari MScan wameshapata kibali nchini Uganda na barani Afrika, na wameuza kifaa hicho kwa mataifa manne ya Afrika. Mwelekeo ni kusajili hakibunifu ya Mscan huko WIPO.

Kwa mujibu wa Dkt. Hembisibwe, kupitia ushirikiano na pashawa ya kazi yao wameweza kufikia wajawazito 13,000 ambao kamwe hawajawahi kupimwa kwa kutumia kifaa cha aina hiyo, na kutatua zaidi ya changamoto 1,600 za ujauzito.