Hatua ya Marekani kujiondoa kwenye mashirika ya UN yamaanisha nini kwa tabianchi, biashara na maendeleo?
Hatua ya Marekani kujiondoa kwenye mashirika ya UN yamaanisha nini kwa tabianchi, biashara na maendeleo?
Mashirika na vyombo husika ni pamoja na:
- UNFPA, UNCTAD, ITC na ICTRs, UN Women
- Mikataba ya kimataifa ukiwemo UNFCCC wa mabadiliko ya tabianchi
- Na baasdhi ya Ofisi za Wawakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa UN
Hatua ya wiki hii ya Marekani ya kutangaza kujiondoa katika vyombo kadhaa vya Umoja wa Mataifa inalenga miradi na mipango inayojikita katika maeneo kadhaa lukuki, ikiwemo janga la tabianchi, biashara, jinsia na maendeleo.
Pindi msemaji wa Umoja wa Mataifa Stéphane alipozungumza na waandishi wa habari Alhamisi jijini New York, Marekani kufuatia tangazo la Marekani, alisisitiza kuwa Shirika litaendelea kutelekeza majukumu yake kwa azma ile ile.
Tangazo la Jumatano la Marekani linaeleza kuwa serikali ya Marekani “inasitisha ushiriki wake katika au ufadhili kwenye vyombo hivyo kwa kadri inavyoruhusiwa kisheria.”
Vyombo kadhaa vilivyoorodheshwa kwenye taarifa hiyo hufadhiliwa kimsingi au kiasi kwa bajeti ya kawaida ya Umoja wa Mataifa, ikimaanisha kwamba ufadhili utaguswa na tangazo hilo la Marekani, ijapokuwa ufadhili mkuu utaendelea.
Hata hivyo, Ikulu ya Marekani inaeleza kuwa tathmini yake ya ufadhili kwa mashirika ya kimataifa inaendelea na kwa sasa haiku dhahiri madhara ya tangazo la sasa yatakuwa ni kwa kiasi gani.
Hapa tunakuwekea bayana mchanganuo wa vyombo 31 vya Umoja wa Mataifa vilivyotajwa kwenye tangazo hilo la Marekani, na mchango wa vyombo hivyo katika maisha ya watu, jamii na mataifa kwa ujumla.
Masula ya Afrika
- Ofisi ya Mshauri Maalum wa Masuala ya Afrika: Hupatia ushauri bora bara la Afrika, na kuhakikisha mipango ya Umoja wa Mataifa kwenye bara hilo inaendana na mahitaji ya wananchi
- Jukwaa la Kudumu la Watu wenye Asili ya Afrika: Hulenga kuboresha usalama, ubora wa maisha na maendeleo ya watu wenye asili ya Afrika, na hushauri Baraza la UN la Haki za Binadamu.
Tabianchi na Mazingira
- Programu ya Pamoja ya UN ya Kupunguza Hewa Chafuzi kutokana na Ukataji Misitu katika nchi zinazoendelea (UN-REDD): Hutoa ushauri wa kiufundi, miongozo ya kisera na ufadhili kwa ajili ya usimamizi endelevu wa misitu
- Shirika la UN kuhusu Masuala ya Nishati (UN Energy; Huratibu kazi za mashirika 30 ya Umoja wa Mataifa na ya kimataifa ili kusongesha upatikanaji rahisi wa nishati ya uhakika, nafuu na ya kisasa kwa watu wote.
- Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (UNFCCC) ; Mkataba huu ambao huandaa mikutano ya viongozi ya nchi wanachama wa mkataba huo (COPs) ni msingi katika kuwezesha ushirikiano wa kimataifa na kuhakikisha uwazi na uwajibikaji katika kutatua janga la tabianchi.
- UN na Bahari (UN Oceans); Huimarisha uratibu wa UN juu ya masuala ya bahari kama vile uhifadhi wa anuai ya bahari, kusongesha matumizi endelevu ya bahari na usimamizi bora wa bahari duniani
- UN na Maji (UN Water): Huratibu masuala ya maji na huduma za kujisafi na kusongesha usimamizi endelevu wa rasilimali za maji
Uratibu
- Mfumo wa UN wa Bodi Kuu Tendaji za Uratibu; Huleta pamoja wakuu wa mashirika ya UN ili kuhakikisha hatua za pamoja juu ya changamoto za dunia na kuhakikisha utekelezaji fanisi wa majukumu ya UN
Maendeleo
- Shirika la Umoja wa Mataifa la Makazi ya Binadamu (UN Habitat): Husongesha miji na majiji endelevu, na hutoa ushauri wa kiufundi na kisera ili kuboresha mazingira ya kuishi na kupunguza umaskini wa mijini
Elimu na Mafunzo
- Chuo cha UN cha Mafunzo na Utafiti (UNITAR): Hutoa mafunzo na kujengea uwezo watu mmoja mmoja, mashirika nan chi, (hususan mataifa yanayoendelea) kwenye maeneo kama vile diplomasia, maendeleo endelevu, mabadiliko ya tabianchi na usimamizi wa majanga
- Chuo cha UN cha Mafunzo kwa Watumishi: Hupatia watumishi wa UN mafunzo, na huduma za ushauri ili kuhakikisha nguvu kazi ina uwezo, inaendana na mazingira na inafanya kazi kwa ushirikiano
- Chuo Kikuu cha UN: Tanuru la fikra la UN na hutoa mafunzo ya shahada za juu, hufanya tafiti na hutoa miongozo ya kisera kwenye masuala muhimu ya dunia
- Education Cannot Wait: Mfuko wa Umoja wa Mataifa uliojikita katika kufadhili elimu kwenye maeneo yenye dharura na majanga yaliyodumu muda mrefu, ili kuhakikisha watoto na vijana walioathiriwa vibaya na majanga, ukimbizi na wanapata elimu bora na kwa usalama
Jinsia
- Shirika la Umoja wa Mataifa la Masuala ya Wanawake (UN Women): Hufanya kazi kutokomeza ubaguzi dhidi ya wanawake na wasichana, husongesha usawa wa jinsia na kujengea uwezo wanawake duniani kote
Afya
- NShirika la UN la Idadi ya Watu (UNFPA) : Husongesha afya na haki za uzazi kwa wote, na kukuza usawa wa kijinsia na hukusanya takwimu za idadi ya watu kwa ajili ya maendeleo, ikisaidia kupunguza vifo vya akina mama na kupanua upatikanaji wa huduma za uzazi wa mpango.
Sheria ya Kimataifa
- Kamisheni ya Kimataifa ya Sheria: Husimamia uendelezaji na urasimishaji wa sheria za kimataifa kwa kuandaa vyombo vya kisheria na kufafanua kanuni; kukuza utawala wa sheria, na kuunga mkono mahusiano ya amani baina ya mataifa.
- Mfumo wa Kimataifa wa Masalia ya Mahakama za Kimataifa za Uhalifu : Hutekeleza majukumu muhimu ya Mahakama za Kimataifa za zamani za makosa ya uhalifu za Rwanda na Yugoslavia, hukamilisha kesi zinazoendelea, hulinda mashahidi na kuhifadhi kumbukumbu, kuhakikisha uwajibikaji kwa uhalifu mkubwa wa kimataifa.
Kupunguza mizozo na ghasia
- Ofisi ya Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu kuhusu Watoto kwenye Mizozo: Huongoza utetezi wa kimataifa na ufuatiliaji ili kulinda watoto wanaoathiriwa vibaya na migogoro ya kivita.
- Ofisi ya Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu kuhusu Ukatili dhidi ya Watoto: Hufanya utetezi wa kimataifa ili kuzuia na kuondoa aina zote za ukatili na ghasia dhidi ya watoto.
- Ofisi ya Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Ukatili wa Kingono kwenye Mizozo: Inangoza juhudi za Umoja wa Mataifa za kuzuia na kuchukua hatua dhidi ya unyanyasaji wa kingono kwenye mizozo kwa kutetea manusura, kushirikiana na serikali na makundi yaliyojihami ili kumaliza ukiukwaji, na kukuza uwajibikaji.
- Kamisheni ya Ulinzi wa Amani: Inasaidia juhudi za amani katika nchi zinazotoka kwenye migogoro kwa kuratibu rasilimali, kutoa ushauri wa kimkakati, na kukuza ushirikiano.
- Mfuko wa Ujenzi wa Amani : Inatoa ufadhili wa kulingana na mazingira kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa amani ili kuzuia kurejea kwa vurugu na kuanzisha uthabiti na maendeleo ya muda mrefu.
- Ofisi ya Umoja wa Mataifa wa Muungano wa Ustaarabu (UNOAC) : Inakuza mazungumzo na ushirikiano kati ya mataifa, tamaduni, na dini ili kupambana na mgawanyiko na itikadi kali.
- Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Msajili wa Silaha za kizamani: Hukaribisha nchi wanachama kuripoti kila mwaka kuhusu uagizaji, usafirishaji na umiliki ya silaha kuu za kizamani, ikipunguza hatari ya migogoro ya kivita kupitia uwazi zaidi katika uhamishaji wa silaha.
Biashara na Uchumi
- Idara ya Masuala ya Uchumi na Kijamii: Huandaa na kuchanganua takwimu za kiuchumi, kijamii na kimazingira, ikisaidia mataifa kushughulikia changamoto za maendeleo zinazohitaji haraka.
- EKamisheni za kiuchumi kwa Afrika, Amerika ya Kusini na Karibea , Asia na Pasifiki na Asia Magharibi: Kamisheni hizi za kikanda hutoa miongozo ya sera, hufanya iwe rahisi mazungumzo kati ya serikali na kujenga uwezo kwa ajili ya maendeleo endelevu na jumuishi.
- Kituo cha Kimataifa cha Biashara (ITC) : Hujengea uwezo biashara ndogo na za kati katika nchi zinazoendelea kiuchumi na zile zilizo kwenye mpito kupitia biashara na uelewa wa masoko, msaada wa kiufundi na ujenzi wa uwezo.
- Shirika la Umoja wa Mataifa la Biashara na Maendeleo, (UNCTAD): Inasaidia nchi zinazoendelea kujiunganisha na uchumi wa dunia kwa kutoa utafiti, uchambuzi wa sera, na msaada wa kiufundi kuhusu biashara, uwekezaji, fedha, na teknolojia.