Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mpira wa kikapu wabadilisha maisha ya vijana wa Yambio nchini Sudan Kusini

Kundi la wanaume wa Kiafrika wakiwa wamevaa sare za mpira wa kikapu na nguo za kawaida kwenye uwanja wa nje huko Yambio, wakiwa na ukuta wa simba wenye rangi nyingi nyuma.
Habari za UN Vijana wa timu ya mpira wa kikapu ya Yambio wakifurahia baada ya mechi na walinda amani wa UNMISS

Mpira wa kikapu wabadilisha maisha ya vijana wa Yambio nchini Sudan Kusini

Amani na Usalama

Kwa msaada wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini UNMISS, uwanja wa mpira wa kikapu mjini Yambio, jimboni Equatoria Magharibi umekuwa kituo cha matumaini na ushirikiano, ukileta pamoja vijana kutoka makabila na asili tofauti. 

Huko Yambio nchini Sudan Kusini katika kiwanja cha mpira wa kikapu inafanyika mechi kati ya walinda amani wa Umoja wa Mataifa wa ujumbe wa UN nchini humo UNMISS na vijana wa Yambio.

Vijana wanaonekana kufurahia baada ya mechi, wakicheza mziki. Kila aina ya shangwe inayotengenezwa hapa ina umuhimu mkubwa kwani inajenga maridhiano, inavunja tofauti zilizodumu kwa muda mrefu miongoni mwa wanajamii, na kujenga uhusiano mpya wa umoja na urafiki.

Sunge Emmanuel ni katibu Mkuu wa Chama cha Mpira wa Kikapu cha Equatoria Magharibi na anasema michezo inaunganisha jamii na kuwapa sababu ya kuishi. “Mara tu watu wanaotoka kwenye malezi tofauti na matabaka tofauti ya maisha wanapokutana na kuwasiliana, kuna mabadiliko ya kifikra yanatokea na badala ya kukaa tu bila ya kujishughulisha na jambo lolote angalau sisi tunajishughulisha katika shughuli chanya kama michezo.”

Kupitia chama cha mpira wa kikapu huko Equatoria Magharibi vijana wanajifunza kuhusu ushirikiano na kuponya nafsi zao kutokana na madhila mbalimbali waliyopitia na kuwa pamoja.

Silhouette za vijana wakicheza mpira wa kikapu kwenye uwanja wa nje chini ya anga la bluu, huku malori UN yakionekana nyuma.
Habari za UN UNMISS inatumia michezo kuponya majeraha ya zamani ya wanajamii na kujenga jamii hususan za vijana wenye mshikamano

Papy Christian, ni Afisa wa Masuala ya Kiraia wa UNMISS na anasema“Vijana wamekuwa wakitumika kama kichocheo cha migogoro, na wametumika kama ngao ya migogoro. Vijana hawa sasa wanayopaswa kuchukua jukumu katika kuleta amani, usalama, maendeleo, na utekelezaji wa ajenda ya Vijana pamoja na amani na Usalama ili kuwafanya wajisikie kuwa wao ni washirika muhimu wa amani.”

Kupitia shughuli kama hizi za michezo, UNMISS inawapa vijana uwezo wa kuwa viongozi wa amani katika jumuiya zao, wakikuza matumaini ya maisha bora ya baadaye.