Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

China yataka mshikamano huku ikiahidi msaada zaidi kwa UN

Waziri Mkuu wa China Li Qiang akihutubia Mjadala wa UNGA80
UN Photo/Loey Felipe Waziri Mkuu wa China Li Qiang akihutubia Mjadala wa UNGA80

China yataka mshikamano huku ikiahidi msaada zaidi kwa UN

Amani na Usalama

Waziri Mkuu wa China, Li Qiang, leo aonya katika Mjadala Mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwamba dunia imeingia katika kipindi kipya cha mizozo na mabadiliko, huku sera za upande mmoja na mtazamo wa vita baridi zikirejea.

“Baada ya miaka 80 ya kanuni na mpangilio wa kimataifa, mfumo wa kimataifa umeharibiwa mara kwa mara,” amesema Li . Amesisitiza kuwa China inaendelea kujizatiti kudumisha hadhi na mamlaka ya Umoja wa Mataifa na kufuata mpangilio wa kimataifa unaotegemea sheria.

Li ametaja mafundisho ambayo ubinadamu umemeyapata katika kipindi cha miongo minane iliyopita, ikiwa ni pamoja na thamani ya amani, mshikamano, na haki. Ameongeza kuwa “Amani na maendeleo ni matamanio makuu ya pamoja ya watu wote,” akikumbusha jinsi ushirikiano wa kimataifa wakati wa vita vya upinzani na dharura zilizofuata ulivyochochea maendeleo.

Ameonya kwamba kuacha haki na usawa kunaweza kusababisha dunia kurudi katika machafuko na ukatili.

Kazi ya China kukuza amani na maendeleo

Akizungumzia migogoro ya kimataifa na dharura za kibinadamu, Li amesema, “China iko tayari kushirikiana na pande zote kuchukua hatua zinazoratibiwa na zenye ufanisi ili kutatua matatizo halisi na kukuza amani na maendeleo zaidi duniani.”

Ametaja michango ya China kama mchangiaji wa pili kwa ukubwa wa operesheni za amani za Umoja wa Mataifa na kusisitiza usuluhishi wake katika migogoro, ikiwemo ya Ukraine na mgogoro wa Palestina-Israeli unaoendelea.

Li alisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kiuchumi unaonufaisha pande zote na mazungumzo ya kitamaduni. “China imekuwa mstari wa mbele katika kukuza maendeleo ya pamoja ya dunia,” amesema, akionyesha ukuaji thabiti wa uchumi wa China na jukumu lake katika mpango wa Belt and Road Initiative.

Ameendelea kusema kuwa China itatekeleza miradi ya kitamaduni na tamaduni kwa nchi zinazoendelea ili kukuza uelewano na mazungumzo kati ya tamaduni mbalimbali.

Changamoto za dunia na utawala wa dunia

Kuhusu changamoto zinazojitokeza, Li ametaka suluhisho la pamoja katika mabadiliko ya tabianchi, hatari za kiteknolojia, na maendeleo endelevu. “China imekuwa mshiriki anayehusika katika kushughulikia changamoto za kimataifa,” amesema, akionyesha mipango kama Mpango wa Kimataifa wa Udhibiti wa Akili Mnemba AI na mfumo wa nishati mbadala unaoongoza dunia.

Ametangaza ushirikiano mpya na Umoja wa Mataifa kusaidia maendeleo ya Kusini-Kusini na malengo ya maendeleo endelevu, ikiwemo mchango wa bajeti wa dola milioni 10.