Ni wakati wa sauti zetu vijana zisikilizwe kwa vitendo: Mwanaharakati Dkt.Owusu
Ni wakati wa sauti zetu vijana zisikilizwe kwa vitendo: Mwanaharakati Dkt.Owusu
Katika Mkutano wa Vijana wa Umoja wa Mataifa unaofanyika kandoni mwa mjadala mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa UNGA80 unaoendelea hapa New York, viongozi vijana kutoka duniani kote wanataka uwakilishi mkubwa katika maamuzi ya kimataifa.
Miongoni mwao ni daktari wa tiba na mwanaharakati wa kijamii wa vijana wa Uingereza na Ghana, Dkt. Khadija Owusu ambaye amezungumza na Flora Nducha wa Idhaa hii ya Kiswahili.
Owusu, ambaye pia ni mwanzilishi na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Akaya inayowakilisha wasichana wa zama hizi, anasema vijana hawapaswi kuzungumziwa tu, bali wajumuishwe moja kwa moja katika kuandaa Suluhu za changamoto zinazoihusu dunia wakiwemo na wao "Mara nyingi tunazungumza kuwa tunataka ushiriki zaidi wa vijana wakati umefika wa kuacha kuzungumza tu kuhusu kuhitaji vijana wengi, bali tuwe na vijana wengi."
Niko hapa kuwakilisha maelfu ya wasichana
Anasema ushiriki wake katika mkutano huu wa ngazi ya juu wa vijana si wa kibinafsi tu, bali unaakisi sauti za wasichana na vijana wengi wanaosaidiwa na taasisi yake ya Akaya.
"Niko hapa kuwakilisha si mimi peke yangu, si Uingereza tu, na si Ghana tu, bali Taasisi ya Akaya, na wasichana na vijana wengi tunaowahudumia nchini kote."
Owusu anaamini vijana wa Kiafrika, hususan wasichana, wanapaswa kupata nafasi kubwa zaidi katika jmaukwaa ya kimataifa kama Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa ili kupaza sauti zao.
"Bado tunahitaji kuona vijana zaidi kama sisi kwenye vyumba vya mikutano, Waafrika zaidi, vijana zaidi wa Kiafrika na wasichana wa Kiafrika kwenye vyumba vya mijadala, wakishiriki majadiliano kwa sababu tunaleta mabadiliko halisi."
Owusu anasema ujumbe wake kwa vijana barani Afrika ni kubeba vipaji vyao, wajiamini, na kuendeleza ndoto zao kwani kila kitu kinawezekana.