Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Miaka 8 baada ya kufurushwa hali ya Warohingya inazidi kuzorota

Mfanyakazi wa kutoa misaada akiwa amevaa koti la mvua la rangi ya chungwa akitumia kipaza sauti katika kambi ya wakimbizi ya Rohingya iliyofurika huko Cox's Bazar, Bangladesh, wakati wa Kimbunga Mocha.
© UNICEF/Sultan Mahmud Mukut Kambi ya wakimbizi ya Rohingya huko Cox's Bazar inajiandaa kukabiliana na Kimbunga Mocha.

Miaka 8 baada ya kufurushwa hali ya Warohingya inazidi kuzorota

Haki za binadamu

Leo Agosti 25 ni miaka minane tangu kufurushwa kwa wingi watu wa Rohingya kuondoka katika Jimbo la Rakhine, Myanmar. 

Umoja wa Mataifa unatoa wito wa mshikamano wa kimataifa kuwasaidia kwani mateso kwa watu hao yanaendelea kuwa mabaya zaidi. Anold Kayanda na tarifa zaidi.
Myanmar (zamani ikiitwa Burma) ni nchi ya Kusini Mashariki mwa Asia yenye zaidi ya makabila 100, inayopakana na India, Bangladesh, China, Laos na Thailand.
Warohingya wanafurushwa na kuteswa kwasababu mbalimbali zikiwemo za kihistoria kwa madai kuwa walitoka Bangladesh ingawa wameishi vizazi na vizazi nchini Myanmar. 
Mama mmoja wa Rohingya anamlisha mtoto wake mwenye utapiamlo katika makao yake katika kambi ya wakimbizi huko Cox's Bazar, Bangladesh.
© UNICEF/Ilvy Njiokiktjien Msichana mwenye umri wa miaka miwili anayeugua utapiamlo akilishwa na mamake kwenye makazi yao huko Cox’s Bazar, Bangladesh.
Pia sababu ya imani yao kwa uislamu miongoni mwa sababu nyingine. Ni miaka minane sasa tangu ufurushwaji mkubwa wa jami hii kutoka jimbo la Rakhine pwani ya Magharibi mwa Myanmar. 
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres anaonya kuwa Warohingya na raia wengine bado wanakabiliwa na ukiukaji wa haki za binadamu na kufurushwa
Anaeleza wasiwasi wake kuhusu tarifa za kufukuzwa na kupunguzwa kwa nafasi za hifadhi katika ukanda huo, huku wakimbizi walioko Bangladesh wakikabiliana na upungufu mkubwa wa msaada wa chakula, elimu na huduma za afya.
Guterres anasisitiza tena wito wake wa kulindwa kwa raia wote kwa mujibu wa sheria za kimataifa na anataka mshikamano mkubwa wa kimataifa
Hata hivyo ana matumaini kuwa Mkutano wa Ngazi ya Juu kuhusu Rohingya utakaofanyika New York mwezi ujao utasaidia kupata suluhu za kudumu.
Watoto wakimbizi wa Rohingya katika kambi huko Aceh, Indonesia, wakipaka rangi bango kubwa la 'HOPE' lenye mjitolea wa UNHCR .
© UNHCR/Amanda Jufrian Watoto wa Rohingya hupaka rangi kwenye bango linalosomeka 'tumaini' kwenye tovuti ya watu waliofurushwa makwao nchini Indonesia.
Kwa upande wake, Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa, Volker Türk, anaeleza kuwa jeshi la Myanmar na Jeshi la Rakhine bado wanaendeleza uhalifu mkubwa dhidi ya Rohingya bila kuchukuliwa hatua, kinyume na sheria za kimataifa na maagizo ya Mahakama ya Kimataifa ya Haki na anatoa wito wa kukomesha matendo hayo ili kuvunja mzunguko wa vurugu