Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Manusura wa ukatili wa kingono wahitaji msaada wa kivitendo si ahadi – Ripoti

Manusura wa ubakaji Naima Said Ali na Batuulo Harun Amin wakishikana mikono katika ofisi za Chama cha Malezi ya Wanawake na Watoto wa Somalia huko Mogadishu.
UN Photo/Fardowsa Hussein Waathirika wa ubakaji wakiwa nje ya chama cha haki za wanawake huko Mogadishu, Somalia.

Manusura wa ukatili wa kingono wahitaji msaada wa kivitendo si ahadi – Ripoti

Amani na Usalama

Ripoti mpya ya Umoja wa Mataifa imebaini ongezeko kubwa la visa vya ukatili wa kingono unaohusiana na migogoro, na kutoa wito wa kuimarishwa kwa huduma za kusaidia manusura.

Kwa mujibu wa Ripoti hiyo ya 16 ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Ukatili wa Kingono kwenye maeneo yenye mizozo iliyotolewa leo jijini New York, Marekani, zaidi ya manusura 4,600 waliripotiwa kufanyiwa ukatili huo mwaka 2024 — ikiwa ni ongezeko la asilimia 25 ikilinganishwa na mwaka uliotangulia.

ikiwa ina kurasa 34, ripoti hiyo inahusisha nchi 21 ambazo taarifa zake zimethibitishwa na Umoja wa Mataifa na inaonesha kuwa ukatili ulifanywa na vikundi vya kiserikali na visivyo vya kiserikali, kama mbinu ya vita, mateso, ugaidi na ukandamizaji wa kisiasa.

Mwanamke na mwanamume wamekaa nje ya hema katika kambi ya watu waliokimbia makazi yao, huku mtoto akiwa karibu.
© UNFPA/Junior Mayindu Manusura wa unyanyasaji wa kingono nchini DR Congo wanapona kwa usaidizi wa wafanyakazi wa mstari wa mbele wa UNFPA.

DRC, Sudan Kusini, Somalia na Haiti zaongoza

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Haiti, Jamhuri ya Afrika ya Kati (CAR), Somalia na Sudan Kusini zinaongoza kwa kuwa na matukio mengi zaidi ya ukatili wa kingono kwenye maeneo yenye mizozo.

Waliokumbwa na visa hivyo ni pamoja na wanawake, wasichana, wanaume, wavulana, pamoja na watu wa mwelekeo tofauti wa kijinsia, jamii za wachache na watu wenye ulemavu.

Umri wa manusura ni kuanzia mwaka mmoja hadi miaka 75, na ripoti inasema, “asilimia 92 ya manusura wote 4,600 ni wanawake.”

Ripoti pia inafichua kuwa ukatili wa kingono ulienea kwenye maeneo watu wanakoshikiliwa kizuizini, ukifanywa kama njia ya mateso, udhalilishaji na kupata taarifa.

Vikundi vya waasi vilitumia ukatili huo kama njia ya kutawala maeneo, rasilimali na kuendeleza itikadi kali. Pia, upatikanaji mkubwa wa silaha ndogo ndogo uliendelea kuchochea vitendo hivi.

Mwanamke wa Haiti aliyevaa kitambaa chekundu kichwani na fulana yenye mistari akishika kichwa chake mkononi kama ishara ya huzuni.
© PAHO/WHO/David Lorens Mentor Mnusurika wa ubakaji amepumzika kwenye kituo cha wakimbizi wa ndani huko Port-au-Prince.

Kauli ya Bi. Patten

Pramila Patten, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu kuhusu Ukatili wa Kingono kwenye mizozo, amenukuliwa kwenye taarifa hiyo akisema kuwa ukosefu wa upatikanaji wa huduma za afya na msaada wa kisaikolojia unawaacha manusura wengi kwenye hatari kubwa, hasa ndani ya saa 72 za baada ya kukumbwa na ukatili ambapo matibabu ya haraka ya ukatili wa kingono huhitajika zaidi.

Nini kifanyike?

Ripoti inashauri kuongeza ufadhili kupitia Mfuko wa Pamoja wa Umoja wa Mataifa wa Kushughulikia Ukatili wa Kingono kwenye mizozo, pamoja na kutumwa kwa washauri wa ulinzi wa wanawake katika maeneo ya migogoro.

Ripoti ina kiambatanisho kilichotaja kwa mara ya kwanza jumla ya pande 63 za kiserikali na zisizo za kiserikali zinazohusishwa na mifumo ya ubakaji na ukatili mwingine wa kingono, kutokana na ushahidi uliothibitishwa na Umoja wa Mataifa.

Baadhi yao, Hamas wa eneo la Palestina linalokaliwa na Israeli,  RED Tabara nchini DRC, na mashirika kadhaa ya usalama nchini Libya.

Ripoti kwa mara ya kwanza pia imeweka "orodha ya tahadhari", ikielekeza lawama kwa vikosi vya Israeli na Urusi kwa madai ya ukatili wa kingono kwenye maeneo ya korokoroni, huku ikieleza kuwa kukosekana kwa upatikanaji wa waangalizi wa Umoja wa Mataifa kunakwamisha uthibitishaji wa kina.

Mwanamke wa Kisomali aliyevaa hijabu ya zambarau anafunika mdomo wake kwa mkono wake, uso wake ukifichwa na kivuli.
UN Photo/Fardowsa Hussein Kufikia Machi 2021, ubakaji na jaribio la ubakaji ndizo zilizoripotiwa mara kwa mara za ukatili wa kingono nchini Somalia.

Wito wa Guterres

Katibu Mkuu wa UN Antonio Guterres ametoa wito kwa pande zote katika migogoro kuhakikisha kuwa hatua madhubuti za kuzuia ukatili wa kingono zinawekwa, ikiwa ni pamoja na kutoa maagizo wazi ya kupiga marufuku ukiukaji huo, kuwawajibisha wahusika na kuruhusu Umoja wa Mataifa kutoa huduma muhimu.

Na kwa Patten, "hatupaswi kuwapa manusura maneno ya matumaini pekee, bali maisha ya utu na hatua thabiti za kukomesha uhalifu huu.”