IFAD - Kilimo chazaa matunda Rwanda: wakulima wadogo wajikwamua
IFAD - Kilimo chazaa matunda Rwanda: wakulima wadogo wajikwamua
Katika kijiji kimoja nchini Rwanda, ndoto ya muda mrefu ya Chantal Uwizeyimana imegeuka kuwa njia ya kujikwamua kiuchumi. Kupitia mradi wa STARLIT unaotekelezwa na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Kilimo – IFAD, wakulima wadogo kama Chantal wamepata mafunzo, pembejeo na maarifa ya kubadili kilimo kuwa chanzo cha mapato ya uhakika. Sasa si tu kwamba mavuno yameongezeka, bali pia maisha yamebadilika kwa namna isiyotarajiwa.
Naam ni Chantal Uwizeyimana huyu, mkazi wa Rwanda, akisimulia safari yake ya matumaini. Kwa zaidi ya miaka 20, alikuwa na ndoto ya kuwa na cherehanj, lakini maisha ya kilimo duni yalikuwa kikwazo kwake na familia yake waliokuwa wakitegemea kwa kuuza mahindi kwa bei ya chini.
“Kabla ya mradi wa STARLIT, ilikuwa vigumu sana kupata mazao ya kutosha kwa sababu hatukuwa na stadi sahihi za kilimo.”
Kupitia mradi STARLIT, ulioanzishwa na IFAD na wadau wengine Chantal na wanaushirika wengine walipata mafunzo ya kilimo bora. Kiongozi wa ushirika wao, ClaudeTwagiramungu, alipelekwa Kenya kujifunza mbinu bora kutoka kwa wakulima wa huko.
Claude Twagiramungu
“Mwanzo hatukujua lolote kuhusu biashara ya kilimo biashara lakini kule Kenya tulifundishwa kwa kina kuhusu faida zake. Niliporejea, niliwafundisha wanachama wenzangu yote niliyopata,”anasema Claude, ambaye pia ni mjasiriamali.
Kwa wale ambao hawakuweza kusafiri, mafunzo yalitolewa kupitia simu za kiganjani. Mavuno yao sasa yameongezeka mara tatu. Mradi huu unalenga wakulima wadogo 2,800 nchini Rwanda na Kenya – nusu yao wakiwa wanawake. Chantal anasema kwa furaha..
“Sasa tunaweza kulipa bima ya afya, karo za shule za watoto wetu na mahitaji ya msingi.”.
Na hatimaye, baada ya miaka 20 ya kusubiri, Chantal amefanikiwa kununua cherehani ya kushonea nguo , na sasa anapata kipato cha ziada
“Lengo langu sasa ni kununua cherehani ya umeme ili kuongeza ubunifu wangu. Pia natamani kununua ng’ombe wa maziwa ili kuendelea kuboresha maisha yangu.”