SOFI: Njaa yapungua kidogo duniani, ukosefu wa usawa ukiongezeka
SOFI: Njaa yapungua kidogo duniani, ukosefu wa usawa ukiongezeka
Ripoti ya mashirika matano ya Umoja wa Mataifa iliyotolewa Jumatatu Julai 28, kuhusu Hali ya Upatikanaji wa Chakula na Lishe Duniani (SOFI) imekadiria kupungua kwa njaa duniani kote tangu 2022, ingawa kwa viwango visivyo sawa.
Ripoti hiyo hiyo kuu ya mwaka huu wa 2025, inakadiria kuwa asilimia 8.2 ya watu duniani, yaani watu milioni 673, walikumbwa na njaa mwaka 2024, ikilinganishwa na asilimia 8.5 mwaka 2023 na asilimia 8.7 mwaka 2022.
Mashirika hayo 5 ya UN ni; lile la Chakula na Kilimo, (FAO), Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), la kuhudumia watoto, (UNICEF), Mpango wa Chakula (WFP), na la Afya Duniani (WHO).
Hali yatofautiana kimaeneo
Amerika ya Kusini na Asia zilishuhudia maboresho, ambapo kiwango cha utapiamlo kilipungua kwa asilimia 1.2 barani Asia na asilimia 1 katika Amerika ya Kusini na Karibea ni kati ya 2022 na 2024.
Hata hivyo, asilimia 20 ya watu barani Afrika na asilimia 12.7 ya watu katika Asia ya Magharibi wanakumbwa na njaa, hali inayoonyesha ongezeko la polepole lakini la kuendelea.
Kati ya watu milioni 512 wanaotarajiwa kuwa na utapiamlo wa muda mrefu ifikapo 2030, takribani asilimia 60 watakuwa barani Afrika.
Mwelekeo wa Malengo ya Maendeleo Endelevu, SDGs
Takwimu hizi pamoja na tathmini ya ripoti kuhusu malengo ya lishe chini ya Ajenda ya Maendeleo Endelevu, zinaonesha changamoto kubwa ya kufanikisha lengo namba 1 la Kutokomeza Njaa.
Miongoni mwa viashiria vya lishe kwa watoto, kiwango cha watoto wadumavu wenye umri wa chini ya miaka mitano kilipungua kwa asilimia 3.2 kati ya 2012 na 2024, lakini kiwango cha watoto wenye uzito uliopitiliza au wenye uzito mdogo bado hakijabadilika sana.
Pia kulikuwa na ongezeko la upungufu wa damu miongoni mwa wanawake wenye umri wa miaka 15 hadi 49, pamoja na ongezeko la unene kupita kiasi kwa watu wazima.
Cha muhimu ni kwamba, ingawa ukosefu wa chakula kwa ujumla ulipungua kidogo kutoka 2023 hadi 2024, watu milioni 335 zaidi walikumbwa na ukosefu wa chakula mwaka 2024 ikilinganishwa na 2019, kabla ya janga la coronavirus">COVID-19, na watu milioni 683 zaidi kuliko mwaka 2015, wakati Ajenda ya Maendeleo Endelevu ilipozinduliwa.
Mfumuko wa bei wa chakula kipindi cha COVID-19
FAO, UNICEF, IFAD, WFP na WHO wamebainisha kuwa makadirio ya njaa na uhakika wa kupata chakula bado yako juu ya viwango vya kabla ya janga la COVID-19, kutokana na mchanganyiko wa hali mbaya: mfumuko wa bei uliosababishwa na COVID-19, vita vya Ukraine, na mishtuko ya hali ya hewa.
Akizungumza wakati wa utangulizi wa ripoti tarehe 22 Julai, Mchumi Mkuu wa FAO, Máximo Torero Cullen, alisisitiza kuwa sera za kifedha na za fedha wakati wa janga la COVID-19 ziliongeza mahitaji na kusababisha mfumuko wa bei.
Pamoja na vikwazo vya biashara ya chakula na bidhaa vilivyosababishwa na vita vya Ukraine na mishtuko ya tabianchi inayoendelea, mambo haya yalichochea mfumuko wa bei ya chakula kwa kiwango kikubwa, na kuzuia urejesho wa usalama wa chakula na lishe baada ya janga.
Hali hii iliathiri zaidi nchi zenye kipato cha chini na cha kati, ambapo mfumuko wa bei ya chakula ulizidi wastani wa kimataifa ambao tayari ulikuwa juu.
Matokeo yake, ingawa idadi ya watu wanaoweza kumudu mlo bora iliongezeka duniani kote kutoka mwaka 2019 hadi 2024 licha ya kupanda kwa bei, ilipungua katika nchi za kipato cha chini na cha kati, ambako bei zilipanda kwa kasi zaidi.
Mapendekezo na mahitaji ya ufadhili
Ripoti inapendekeza mchanganyiko wa sera ili kukabiliana na mfumuko wa bei ya chakula duniani. Hii ni pamoja na hatua za kifedha zilizolengwa kulinda walioathirika zaidi, sera za fedha za kuaminika na za uwazi ili kudhibiti mfumuko wa bei, na uwekezaji wa kimkakati katika mifumo ya chakula na kilimo.
Ripoti pamoja na viongozi wa mashirika hayo pia wamesisitiza kuwa ufadhili unahitajika kwa dharura ili kukabiliana na changamoto za kimataifa.
“Njaa bado ipo katika viwango vya kutisha, lakini ufadhili unaohitajika ili kupambana nayo unapungua,” amesisitiza Mkurugenzi Mtendaji wa WFP, Cindy McCain.
“Mwaka huu, upungufu wa ufadhili kwa hadi asilimia 40 unamaanisha kuwa mamilioni ya watu watapoteza msaada muhimu tunaotoa,” ameongeza.
Amekumbusha kuwa, “ingawa kupungua kidogo kwa viwango vya ukosefu wa chakula ni jambo la kutia moyo, kushindwa kuendelea kutoa msaada muhimu kwa watu walioko kwenye mahitaji ya dharura kutafuta mafanikio haya kwa haraka, na kusababisha hali ya kutoeleweka zaidi katika maeneo yaliyo hatarini duniani.”