Katibu Mkuu wa UN aomboleza kifo cha Rais wa zamani wa Zambia Edgar Lungu
Katibu Mkuu wa UN aomboleza kifo cha Rais wa zamani wa Zambia Edgar Lungu
Malengo ya Maendeleo Endelevu
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres leo ametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha aliyekuwa Rais wa Zambia, Edgar Chagwa Lungu, ambaye aliongoza taifa hilo la Afrika kuanzia mwaka 2015 hadi 2021.
Kupitia taarifa iliyotolewa na msemaji wake, Katibu Mkuu amemkumbuka Rais Lungu kama kiongozi aliyetoa mchango mkubwa katika diplomasia na kuanzisha miradi muhimu ya miundombinu wakati wa uongozi wake.
“Katibu Mkuu amepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha Rais wa zamani wa Zambia, Edgar Chagwa Lungu,” taarifa hiyo imesema. “Anatoa salamu za rambirambi kwa familia yake, Serikali na wananchi wa Zambia.”
Historia fupi ya Lungu
Edgar Lungu alizaliwa mwaka 1956 na alipata umaarufu kupitia taaluma ya sheria na siasa, akihudumu kama Waziri wa Sheria na Waziri wa Ulinzi kabla ya kuchukua nafasi ya urais mwaka 2015 kufuatia kifo cha Rais Michael Sata. Baadaye alichaguliwa kuwa Rais mwaka huo huo na tena mwaka 2016.
Wakati wa uongozi wake, Rais Lungu alipeleka mbele miradi ya maendeleo ya miundombinu, hususan katika sekta za barabara, nishati na afya.
Alijulikana pia kama kiongozi aliyesaidia kudumisha uhusiano wa kidiplomasia katika ukanda wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na Muungano wa Afrika.
Alichangia uchaguzi wa amani
Ingawa serikali yake ilikabiliwa na ukosoaji kuhusu kudhoofika kwa demokrasia na kuongezeka kwa deni la taifa, Lungu alisimamia uchaguzi wa amani mwaka 2021 uliosababisha kukabidhi madaraka kwa Rais wa sasa, Hakainde Hichilema.
Habari za kifo chake zimezua maombolezo na heshima kutoka kwa wananchi wa Zambia na viongozi wa bara zima la Afrika.
Taarifa ya Umoja wa Mataifa inaonesha namna mchango wa Rais Lungu ulivyoacha alama ya kudumu katika maendeleo ya Zambia na diplomasia ya kikanda.