Mkuu wa misaada wa UN aishutumu Israel kwa kuendelea kuzuia misaada Gaza
Mkuu wa misaada wa UN aishutumu Israel kwa kuendelea kuzuia misaada Gaza
Mratibu wa misaada ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa Tom Fletcher leo ametoa wito wa kuondoa vizuizi vya misaada mara moja Gaza, aonya kuhusu mateso yanayoendelea kwa raia miezi mwili tangu kuanza kwa vizuizi hiyo Gaza.
Katika taarifa yake afisa mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura OCHA amesema vizuizi hivyo vya makusudi vya Israel dhidi ya misaada vinagharimu maisha ya raia na vinakiuka sheria za kimataifa.
Katika taarifa nzito Tom Fletcher, amezitaka mamlaka za Israel “kuondoa kizuizi hiki cha kikatili cha misaada na kuruhusu msaada unaookoa maisha kuingia katika eneo hilo lililozingirwa nakukaliwa kimabavu”.
Kuzuia misaada kunakatili maisha
Fletcher amesema kwamba miezi miwili iliyopita, Israel ilifanya “uamuzi wa makusudi kuzuia misaada yote ya kibinadamu kuingia Gaza, na hivyo kusimamisha juhudi za Umoja wa Mataifa za kuwasaidia walionusurika kutokana na mashambulizi ya kijeshi”.
Aongeza kuwa Israel imekuwa “wazi kwa uthubutu kuhusu nia yake ya kuishinikiza Hamas”, lakini alisisitiza kuwa mbinu kama hizo hazikubaliki chini ya sheria za kimataifa na zinaowaathiri zaidi ni raia wasio na hatia.
Ameonya kwamba “Kuzuia misaada kunawanyima raia chakula, kunawaacha bila huduma za msingi za afya, kunawavua utu na matumaini na kunaweka katika adhabu ya pamoja isiyo na huruma”.
Ameendelea kusisitiza kwamba “Kuzuia misaada kunaua.”
Misaada haipaswi kuwa kadi ya masharti
Akiendelea kukemea utekaji nyara, Fletcher amesisitiza kwamba Hamas lazima iwaachilia mateka wote sasa, huku akisisitiza kuwa misaada ya kibinadamu haiwezi kutumika kama chombo cha shinikizo katika mazungumzo ya kisiasa au kijeshi.
Pia Fletcher amesema “Sheria za kimataifa ziko wazi, kama nguvu inayokalia, Israel lazima iruhusu msaada wa kibinadamu kuingia Gaza,” akiongeza kuwa “Misaada inayookoa na maisha ya raia, havipaswi kamwe kuwa kadi ya masharti.”
Mapendekezo ya Israel hayafikii kiwango cha chini cha msaada
Fletcher pia amekosoa mapendekezo ya hivi karibuni kutoka kwa mamlaka za Israel, akisema hayafikii “kiwango cha chini cha msaada wa kibinadamu unaozingatia misingi ya kanuni.”
Amesisitiza msimamo wa usawa na uhuru wa harakati za misaada ya kibinadamu, na kuongeza kuwa timu za Umoja wa Mataifa ziko tayari kuokoa maisha “licha ya hatari kubwa zilizopo.”
Hatutakata tamaa
Katika hitimisho lenye hisia la taarifa yake Fletcher amewaomba radhi raia wa Gaza kwa kushindwa kwa jumuiya ya kimataifa kumaliza kizuizi hicho.
Amesema “Kwa raia waliobaki bila ulinzi, hakuna ombi la msamaha linaloweza kutosha kutimiza lengo hilo” akiongeza kuwa “Lakini kwa kweli naomba radhi kwamba tumeshindwa kuishawishi jumuiya ya kimataifa kuzuia dhuluma hii. Hatutakata tamaa, hata kama dunia imewapa kila sababu ya kukata tamaa na sisi.”
Shinikizo la kimataifa laanza kuongezeka
Taarifa hiyo inaongeza sauti katika ukosoaji unaoongezeka duniani kote dhidi ya hatua za Israel huko Gaza katikati ya janga la kibinadamu linalozidi kuongezeka.
Makundi ya haki za binadamu yameonya kuhusu njaa, magonjwa, na kuanguka kwa mifumo ya afya katika eneo hilo lenye msongamano mkubwa.
Juhudi za kidiplomasia za kufanikisha kusitisha mapigano na kupata fursa ya upatikanaji wa misaada hadi sasa hazijazaa matunda, huku mzozo ukiendelea kuingia mwezi wa saba.