Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

DRC: Kinachotakiwa ni sitisho la mapigano bila masharti yoyote

Bintou Keita (kwenye skrini) Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa UN nchini DRC na pia Mkuu wa MONUSCO akihutubia Baraza la Usalama la UN 27 Machi 2025 jijini New York, Marekani
UN Photo/Manuel Elías
Bintou Keita (kwenye skrini) Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa UN nchini DRC na pia Mkuu wa MONUSCO akihutubia Baraza la Usalama la UN 27 Machi 2025 jijini New York, Marekani

DRC: Kinachotakiwa ni sitisho la mapigano bila masharti yoyote

Amani na Usalama
  • Sitisho la mapigano ni muarobaini
  • Balozi Ngay asema hakuna askari wa Rwanda aliyeondoka DRC
  • Waziri Nduhungirehe asema mikakati ya Rwanda kujilinda kwa sasa itasalia pale pale

Mapigano yakizidi kushamiri huko mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC tangu mwezi Januari mwaka huu, Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Mataifa nchini humo Bintou Keita ameliambia Baraza la Usalama kuwa juhudi zote zielekezwe kwenye sitisho la mapigano lisilo na masharti yoyote.

Bintou Keita akihutubia ikiwa ni moja ya vikao vinavyofanyika kila baada ya miezi mitatu kueleza Baraza juu ya hali ya amani na usalama DRC, amesema ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulindaa amani nchini humo ambao yeye pia anauongoza, “umejizatiti kusaidia harakati za kikanda za kuleta amani kwenye taifa hilo la Maziwa Makuu.

"MONUSCO iko tayari kutumia uwezo wake wote kutekeleza sitisho la mapigano linaloweza kupatikana,” amesema hayo kwenye mkutano huo uliohudhuriwa pia na Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda Olivier Nduhungirehe.

Msuluhishi wa AU ateuliwe mapema kuratibu michakato ya amani ya kikanda

Ameweka bayana hata hivyo kwamba “licha ya juhudi muhimu za kikanda na kimataifa, sitisho la mapigano lisilo na masharti yoyote lililoitishwa na viongozi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, EAC, Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika, SADC, Muungano wa Afrika, AU na Baraza la Usalama kupitia azimio namba 2773, na vile vile hivi karibuni huko Qatar, hadi sasa hakuna kilichopatikana.

Watu wanaokimbia ghasia mashariki mwa DR Congo eneo la Bukavu, wakisubiri kuvuka mpaka wa Gatumba na kuingia Burundi.
© UNHCR/Bernard Ntwari
Watu wanaokimbia ghasia mashariki mwa DR Congo eneo la Bukavu, wakisubiri kuvuka mpaka wa Gatumba na kuingia Burundi.

"Ni vema pande zote kuheshimu ahadi zao za kunyamazisha silaha na kusaka Suluhu kwa njia ya amani,” amesema hayo huku akishukuru harakati za Rais wa Angola ambaye ni Mwenyekiti wa AU, João Lourenço, "kwa kusaka bila kuchoka harakati za kurejesha mazungumzo kati ya DRC na Rwanda.”

Amesihi kuteuliwa haraka kwa Msuluhishi wa AU atakayeteuliwa na viongozi wa EAC na SADC, kwa lengo la kuunganisha michakato ya amani kwa kutumia msingi wa michakato ya Luanda na Nairobi.

Bi. Keita amesema ni matumaini yake kuwa Baraza la Usalama ambalo lina jukumu la kusimamia amani na usalama duniani, litawajibisha kila upande kwa mujibu wa azimio namba 2773 ambalo pamoja na mambo mengine linaweka mwongozo wa mchakato wa kisiasa na amani nchini humo.
 
Amesema MONUSCO, ambao ni ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini DRC, uko tayari kusaidia usimamizi na utekelezaji wa sitisho la mapigano kwa sababu hoja hilo ni moja ya mambo yaliyopitishwa na mkutano wa pamoja wa viongozi wa Jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki, EAC na ile ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika, SADC.

Guterres kuandikia barua Baraza la Usalama kuhusu uondokaji wa MONUSCO

Alipoulizwa kuhusu mchakato wa MONUSCO kuondoka kwenye majimbo ya Ituri na Kivu Kaskazini, Bi. Keita ambaye anaongoza pia ujumbe huo amesema, “nadhani hebu tueleweke. Bado kuna mchakato wa kuondoka unaendelea. Tulikubaliana mwaka jana kuanzia Septemba hadi Desemba kwamba kuna mbinu mpya itakayoandaliwa. Na vigezo ni kwamba hatutaondoka jimbo kwa jimbo, bali tutaangalia kila jimbo ni wapi kuna hatari na ambako raia wanahitaji kulindwa zaidi ambao ndio msingi wa jukumu letu.”
 
Amesema kulikuwa kufanyike kikao cha Utatu cha mchakato wa Luanda unaoongozwa na Rais Joao Lorenzo wa Angola ukileta pamoja Rais Felix  Tshisekedi wa DRC na Paul Kagame wa Rwanda lakini haukufanyika, na baadaye kuanzia Januari mapigano yakaanza na hali ya usalama imeendelea kudorora.
 
Hivyo hatukuweza kukaa na mamlaka kujadili huo mpango mpya wa kuondoka Ituri na Kivu Kaskazini.
“Sasa tunaenda kufanya hivyo kupitia barua itakayoandikwa na Katibu Mkuu kwenda kwa Baraza la Usalama, ambayo ilikuwa iwasilishwe ifikapo mwishoni mwa mwezi huu kuelezea uhalisia huo. Hatujapata fursa ya kuzungumza na kupanga upya mbinu ya kuondoka, na wakati huu si sahihi kwa MONUSCO kuondoka Kivu Kaskazini,” amesema Bi. Keita.

MONUSCO inatekeleza wajibu wake kule ambako M23 inashikilia

Kuhusu ulinzi wa raia, Mkuu huyo wa MONUSCO amesema sasa hivi kuna changamoto kubwa kutokana na waasi wa M23 ambao wametwaa Goma jimboni Kivu Kaskazini na Bukavu jimboni Kivu Kusini, wameweka vizuizi vingi njiani kwa hiyo inakuwa vigumu kuendesha doria zilizooeleka. “Na zaidi ya hapo tunatakiwa kutoa taarifa saa 48 kabla ya kuendesha doria au kupita kwenye maeneo kufikisha misaada ya kiutu. Hii yote inaleta mkwamo. Lakini kila mtu aelewe kuwa bado tunatekeleza majukumu yetu kwenye maeneo yanayodhibitiwa na M23.”

Madhara ya Marekani kuondoa ufadhili

Amemulika pia jinsi hatua ya Marekani kuondoa ufadhili kwenye mashirika ya kiutu akisema asilimia 70 ya ufadhili wa ombi la usaidizi kwa DRC inatolewana Marekani.
“Hivyo unaweza kufikiria hii ina maana gani. Inabidi uchague nani anapata msaada wakati huu ambapo wahitaji ni wengi. Kwa hiyo kwangu mimi nikitazama muda wa sasa, muda wa kati na muda ujao.”

Hakuna askari wa Rwanda aliyeondoka DRC – Balozi Ngay

Zénon Mukongo Ngay, Mwakilishi wa Kudumu wa DRC kwenye Umoja wa Mataifa, alipatiwa fursa ya kuhutubia wajumbe wa Baraza ambapo amesema “utekelezaji wa azimio namba 2773 la mwaka 2025 unasalia kuwa kipaumbele.”

Amesema “hadi leo hii, hakuna askari wa Rwanda ameondoka kutoka ardhi ya DRC, hakuna wapiganaji wa M23/AFC walioondoka kutoka Goma au Bukavu, au eneo lolote linalodhibitiwa na waasi hao na hakuna utawala wowote sambamba na ule wa serikali ambao umevunjwa,” akizungumzia waasi wa M23 ambao wameunda utawala wao kwenye mji wa Goma na kuteua Gavana wao, hali iliyosababisha DRC kuhamishia makao makuu ya jimbo la Kivu Kaskazini kwenda mji wa Beni.

Mikakati yetu ya kujilinda itasalia palepale kwa sasa – Waziri Nduhungirehe

Kwa upande wake, Bwana Nduhungirehe, ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda ameeleza Baraza kuwa, “kilicho dhahiri kwetu Rwanda ni kwamba mikakati ya kujilinda ambayo tumeiweka itaendelea kusalia, hadi pale kuna mfumo wa uhakika wa muda mrefu wenye hakikisho la usalama, kwenye mpaka wetu na DRC.”

Kisha Waziri huyo wa Mambo ya Nje wa Rwanda alizungumza na waandishi wa habari nje ya ukumbi wa Baraza na kusema kuwa “ni juu ya ukanda wetu na Afrika kutuongoza kwenye mchakato wa kutusongesha mbele.”