Muhtasari wa Habari 31 Desemba 2024
Muhtasari wa Habari 31 Desemba 2024
Amani na Usalama
Msumbiji hali bado ni tete watu waendelea kufungasha virago, Gaza mfumo wa afya wazidi kupata pigo na Mkuu wa WHO atoa wito katika ujumbe wa mwaka mpya
Vurugu baada ya uchaguzi nchini Msumbiji zimewalazimisha maelfu ya watu kuyahama makazi yao na wengine kukimbilia nchi jirani limeeleza leo Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi UNHCR. UNHCR inaeleza kuwa Serikali ya Malawi imeripoti kuwapokea watu 2,000 waliovuka na kuingia nchini humo katika wiki iliyopita. Na katika nchi jirani ya Eswatini, watu wengine 1,000 wamesili. Miongoni mwa waliowasili ni wakimbizi na waomba hifadhi raia wa mataifa mbalimbali ambao wamekuwa wakiishi Msumbiji.
Ripoti iliyochapishwa leo na Ofisi ya Haki za Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa imeweka wazi kuwa mtindo wa Israel wa mashambulizi mabaya karibu na dhidi ya hospitali katika Gaza, yamesukuma mfumo wa afya kwenye ukingo wa kuelekea kuporomoka kabisa, hali ambayo imekuja na athari mbaya kwa Wapalestina kukosa uwezo wa kupata huduma za afya na matibabu.
Mkurugenzi Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni (WHO) Dkt.Tedros Adhanom Ghebreyesus kupitia ujumbe wa mwisho wa mwaka amesisitiza kwamba "amani ni, na daima itakuwa, dawa bora kwa afya na ustawi wa watu wote, kila mahali." Pia Tedros ametaja baadhi ya mafanikio ya mwaka uliopita kuwa ni pamoja na “kutokomeza malaria na magonjwa mengine yaliyosahaulika katika nchi nyingi, na kwamba sasa nchi 17 za Afrika zinatumia chanjo mpya ya malaria.