Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu wa Haiti wanaomba mambo matatu - Edem Wosornu

Edem Wosornu, Mkurugenzi wa Operesheni na Utetezi katika shirika la Umoja wa Mataifa la kutoa misaada ya dharura OCHA akiwa na watoto katika mji mkuu wa Haiti, Port-au-Prince.
UNICEF/ Herold Joseph
Edem Wosornu, Mkurugenzi wa Operesheni na Utetezi katika shirika la Umoja wa Mataifa la kutoa misaada ya dharura OCHA akiwa na watoto katika mji mkuu wa Haiti, Port-au-Prince.

Watu wa Haiti wanaomba mambo matatu - Edem Wosornu

Msaada wa Kibinadamu

Wakati wa ziara ya siku nne nchini Haiti hivi karibuni, Mkurugenzi wa Uendeshaji na Utetezi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuratibu Misaada ya Dharura (OCHA), Edem Wosornu ametembelea maeneo kadhaa ya miradi ya misaada ya kibinadamu na kukutana na jamii zilizoathirika, mamlaka za Haiti, pamoja na washirika wa kitaifa, kimataifa na wa ndani, kujadili janga la kibinadamu nchini humo pamoja na mikakati zaidi ya misaada ya dharura.

Akieleza hali aliyoikuta Bi Wosornu anasema, “Watu wa Haiti wanaomba mambo matatu. Wanaomba amani, wanaomba ghasia za magenge zikome, wanaomba kurejeshewa nchi yao.”

Ziara hiyo inakuja wakati ambapo Haiti inakabiliwa na mgogoro ambao umezidi kuwa mbaya zaidi tangu Machi mwaka huu kukiwa na vurugu mpya katika mji mkuu, Port-au-Prince. Kwa mujibu wa OCHA, zaidi ya watu 578,000 kwa sasa wamekimbia makazi yao nchini Haiti, na zaidi ya shule 900 zimefungwa tangu Januari mwaka huu yaani zaidi ya nusu mwaka.

Anaeleza alichozungumza na watoto akisema, "Watoto nilioshirikiana nao huko Gonaives, huko Les Cayes lakini pia huko Port-au-Prince, wanaomba kuweza kurejea shuleni. Watoto niliokutana nao wanataka kuwa madaktari, wanataka kuwa wanasheria, wanataka kuwa walimu, wanataka kuwa wauguzi. Watu wa Haiti wamechoshwa na ghasia. Watu wa Haiti wanataka kurejea katika maisha yao.”

Emile Macier, mkuu wa shule ya Joseph Bernard des Frères ya mjini Port-au-Prince kwa masikitiko anaeleza, “Maelfu ya wanafunzi wananyimwa masomo. Nani anajua, labda magenge yamewachukua. Nia yangu kubwa ni kwamba tutafute sehemu nyingine ya kuwahifadhi waliofurushwa ili shule ifanye kazi. Hatuwezi kufunga shule. Je, itakuwaje kwa watoto? Huwezi kujua magenge yamewawajiri wangapi? Huweze kujua wasichana wangapi walibakwa na kupata mimba. Hatujui.”

Kwa upande wa afya nako hali ni tete kama alivyojionea Mkurugenzi wa Uendeshaji na Utetezi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuratibu Misaada ya Dharura (OCHA), Edem Wosornu,

“Tunatakiwa kuhakikisha kuwa vituo vya afya vya nchi hii vina uwezo wa kuwasaidia wananchi. Tunahitaji kuhakikisha kuwa miundombinu ya elimu ina uwezo wa kusaidia watu. Suluhu za muda mrefu zinahitajika za haraka na za muda mfupi.

Bi Wosornu anaeleza kwamba, Bi Wosornu anaeleza kwamba, "Watu milioni 1.6 kati ya watu milioni 5 ambao wana uhaba wa chakula katika nchi hii wanahitaji sana usaidizi. Nchi inayozalisha maembe na ndizi na viazi vikuu na ndizi na nchi ambayo ina udongo halisi, wenye rutuba na wenye rutuba haipaswi kuwa na uhaba wa chakula. Vurugu lazima zikome ili kuruhusu watu kurudi kwenye mashamba yao, ili waweze kuishi maisha yao.

Ni nini kifanyike? Wosornu anaeleza, "Wadau wa misaada ya kibinadamu ni sehemu ya suluhisho, lakini pia tunahitaji washirika wa maendeleo kwa mbinu za muda mrefu. Tunahitaji suluhu za pamoja, sio tu kutoka kwa sehemu moja ya mwavuli wa usaidizi, lakini kutoka kwa nyanja zote tofauti za mambo.”