Baraza la Usalama lalaani marufuku ya Taliban kwa wanawake kufanya kazi UN
Baraza la Usalama lalaani marufuku ya Taliban kwa wanawake kufanya kazi UN
Katika azimio la kihistoria, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa hii leo Alhamis limelaani uamuzi wa watawala wa Afghanistan wa kupiga marufuku wanawake raia kufanya kazi katika Umoja wa Mataifa, likiwataka viongozi wa Taliban "kubadili haraka" uamuzi wao.
Azimio hilo lililopitishwa kwa kauli moja na chombo hicho chenye wanachama 15, linataka "ushiriki kamili, sawa, wa maana na salama wa wanawake na wasichana nchini Afghanistan", na linahimiza nchi na mashirika yote yenye ushawishi kwa watawala wa kimsingi wa nchi hiyo, "kuhamasisha mabadiliko ya haraka" ya sera ambazo kwa hakika zimefuta wanawake katika maisha ya umma.
Tangu kundi la Taliban lilipotwaa madaraka Julai 2021, wakati vikosi vyake vilipoiangusha Serikali iliyochaguliwa kwa njia ya kidemokrasia, limerudisha nyuma haki nyingi za binadamu za wanawake na wasichana, ikiwa ni pamoja na kupiga marufuku kuhudhuria shule za sekondari na chuo kikuu, vikwazo vya harakati na kazi, na katika Desemba, amri ya kupiga marufuku raia wa kike kufanya kazi kutoka kwa mashirika yasiyo ya kiserikali.
Mapema mwezi huu Taliban iliongeza marufuku yao kwa wanawake wanaofanya kazi katika Umoja wa Mataifa.
Umoja wa Mataifa ulisisitiza "kulaani kwake bila shaka" kwa hatua hiyo mapema Aprili, ukibainisha kuwa inakiuka sheria za kimataifa, ikiwa ni pamoja na Mkataba wa Umoja wa Mataifa. Wafanyakazi wote wa Umoja wa Mataifa wameambiwa wasiripoti ofisini, isipokuwa kwa baadhi ya kazi muhimu, wakati uhakiki wa uendeshaji unafanywa, unaohitimishwa tarehe 5 Mei.
Takwimu za Umoja wa Mataifa zinaonesha kuwa watu milioni 28.3 nchini Afghanistan wanahitaji msaada mwaka huu, na kuifanya Afghanistan kuwa operesheni kubwa zaidi ya misaada duniani, huku Umoja wa Mataifa ukiomba dola bilioni 4.6 kufadhili kikamilifu juhudi za misaada mwaka huu. Mratibu wa Misaada ya Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa alionya mwezi huu kwamba Afghanistan pia ndiyo operesheni yenye ufadhili mdogo zaidi duniani, na chini ya asilimia tano ya ufadhili imeahidiwa kufikia sasa.
'Wasiwasi mkubwa'
Azimio la leo la Baraza la Usalama linaweka wazi "wasiwasi mkubwa" wa mabalozi juu ya marufuku ya wanawake kufanya kazi katika Umoja wa Mataifa, likisema kwamba - pamoja na mmomonyoko mwingine wa haki za msingi - "utaathiri vibaya na kwa kiasi kikubwa" shughuli za misaada za Umoja wa Mataifa nchini kote, " ikiwa ni pamoja na utoaji wa misaada ya kuokoa maisha na huduma za kimsingi kwa walio hatarini zaidi”.
Inasisitiza kuwa UNAMA, pia haitaweza kutekeleza majukumu yake ya kibinadamu hadi marufuku hiyo itakapomalizika. Azimio hilo linasisitiza kwamba marufuku hiyo “haijawahi kutokea katika historia ya Umoja wa Mataifa.”
Hali ‘mbaya’ za kiuchumi na kibinadamu
Azimio hilo pia linasisitiza haja ya dharura ya kuendelea kushughulikia "hali mbaya ya kiuchumi na kibinadamu" ya Afghanistan na kusaidia nchi kurejesha kujitegemea, kwa kutambua umuhimu wa kuruhusu Benki Kuu kutumia mali ambazo kwa sasa zimezuiliwa nje ya nchi, "kwa manufaa. ya watu wa Afghanistan."
Baraza liliunga mkono kuendelea kwa kazi ya UNAMA ikirejelea "msaada wake kamili", na kutoa wito kwa wote walio na uhusika nchini Afghanistan, ikiwa ni pamoja na mamlaka ya Taliban, "kuhakikisha usalama na uhuru wa kutembea wa Umoja wa Mataifa na wafanyakazi wanaohusika nchini kote. ”