Nyama ikiingia mezani, mikunde hunyanyapaliwa- FAO
Nyama ikiingia mezani, mikunde hunyanyapaliwa- FAO
Jamii ya mikunde! Wengi wanaitambua zaidi kama ni kunde zenyewe, na maharagwe lakini ni zaidi ya hiyo. Kuna choroko, mbaazi, dengu, njegere na kadha wa kadha ambapo kutokana na umuhimu wake sio tu kiuchumi bali pia katika lishe ya binadamu, kurutubisha udongo na pia kuhimili mabadiliko ya tabianchi, ndio maana Umoja wa Mataifa unapigia chepuo.
📍Njombe Tanzania
🧵🎥1/2: @FAOTanzania na @AgriConnect4
katika harakati za kuchagiza ulaji wa mikunde.
"𝗡𝘆𝗮𝗺𝗮 𝗶𝗸𝗶𝗶𝗻𝗴𝗶𝗮 𝗺𝗲𝘇𝗮𝗻𝗶, 𝗺𝗶𝗸𝘂𝗻𝗱𝗲 𝗶𝗻𝗮𝗻𝘆𝗮𝗻𝘆𝗮𝗽𝗮𝗹𝗶𝘄𝗮." @KabambalaJohn https://t.co/xPqPPyphR4
HabarizaUN
Mathalani nchini Tanzania, shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo, FAO linafadhili mradi wa AgriConnect ambao pamoja na mambo mengine unapatia wananchi; wanawake na wanaume stadi za mapishi sahihi ya jamii ya mikunde.
Tathmini ya ulaji wa mikunde Tanzania
Afisa lishe wa FAO nchini Tanzania Stella Kimambo amenukuliwa hivi karibuni huko mkoani Njombe nchini Tanzania akisema “vyakula vya jamii ya mikunde huondoka mezani pale nyama inapoonekana, vinanyanyapaliwa.”
Na kama hiyo haitoshi idadi kubwa ya watanzania hula zaidi maharage lakini mikunde kama vile mbaazi, dengu na choroko havipati nafasi mezani.
Ulaji uko chini lakini uuzaji mikunde nje ya nchi unashamiri
Bi. Kimambo anasema ingawa ulaji wa aina mbalimbali za mikunde uko chini, bado Tanzania ni mzalishaji muhimu wa mikunde na kwamba mwaka 2022 Tanzania iliuza nje ya nchi mazao ya jamii ya mikunde yenye thamani ya dola milioni 266 kutoka dola milioni 198 mwaka 2020. Takribani asilimia 85 ya mazao hayo yanaelekea India.
Magreth Natai afisa lishe kutoka Wizara ya kilimo Tanzania anaelezea juu ya umuhimu wa mazao jamii ya mikunde akisema mazao ya mikunde kama njegere, mbaazi, choroko, kunde ni mazao ambayo yana umuhimu mkubwa kilishe, kiuchumi na kimazingira kwa maana tunajua mikunde inarutubisha udongo.”
Hivyo amesema wataendelea kushirikisha wananchi kutambua umuhimu huo ikiwemo kwa lishe.
Harakati za kuchagiza ulaji wa mikunde
Ili kushamirisha ulaji wa mazao ya jamii ya mikunde hapa nchini, FAO inaunga mkono mradi wa AGRICONNECT, mradi unaochagiza sio tu kuongeza mnyororo wa thamani wa mazao hasa nyanda za juu za kusini mwa Tanzania ikiwemo mkoa wa Njombe, bali pia kuhakikisha kuna uhakika wa chakula na lishe.
Mashindano ya upishi wa mazao ya mikunde yalifanyika mkoani Njombe kusini mwa Tanzania tarehe 10 mwezi Februari mwaka huu wakati wa maadhimisho ya siku ya mikunde duniani.
Nilipika keki kwa kutumia ndizi na maharage
Esther Lukasi mpishi na mama lishe aliibuka mshindi wa pili na akihojiwa na John Kabambala wa Redio Washirika KidsTime FM nchini Tanzania amesema, alipatiwa zawadi ya mtungi wa gesi, vijiko vikubwa vya chakula pamoja na kisu.
“Nilipika mchanganyiko wa wali na choroko, pilau la maharage, ugali wa maharage au usuge, mboga za majani na keki kwa kutumia ndizi na maharage,” amesema Bi. Lukasi.
Kwa mshindi huyu wa pili, mashindano hayo yalikuwa kitu kikubwa kwake kwani hawajahi kupika vitu kama hivyo na kwamba “ninashukuru FAO kwani wamekuja kutupa mafundisho ambayo hatukufahamu hapa. Na nina furaha sana sikutegemea kushinda na nimefurahi kuwa nitaweza kupika chakula kwa urahisi nyumbani kwangu.”
Katika soko la kuu la nafaka na matunda mkoani Njombe, mazao yamesheheni lakini cha ajabu ni changamoto ya lishe miongoni mwa watoto.
Sara Mtibike mchuuzi hapa sokoni anasema changamoto ya lishe licha ya kuweko kwa vyakula ni kwamba “tumeondokana na asili, zamani wazee wetu walipika kande, maboga lakini sisi tunaona uvivu kupika kwa muda mrefu. Hivyo ni vema turejee asili ili watoto wetu waweze kuwa na lishe bora.”