Priyanka Chopra Jonas uso kwa uso na watoto walioathiriwa na ukame nchini Kenya
Priyanka Chopra Jonas uso kwa uso na watoto walioathiriwa na ukame nchini Kenya
Balozi mwema wa shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya Watoto UNICEF Priyanka Chopra Jonas amefanya ziara ya siku mbili nchini Kenya kujionea athari za ukame uliokumba pembe ya Afrika na kusababisha mamilioni ya Watoto kuugua utapiamlo mkali.
Taarifa iliyotolewa na UNICEF kutoka Nairobi Kenya na New York Marekani imeeleza kuwa katika ziara yake hiyo Priyanka alitembelea Kaunti ya Turkana ambayo ni moja kati ya Kaunti 15 nchini Kenya zilizoathiriwa zaidi ya ukame uliosababishwa na mvua kutonyesha katika kipindi cha misimu minne ya mvua mfululizo na kuwaacha zaidi ya watoto 900,000 wenye umri chini ya miaka mitano wakiteseka zaidi ambapo takwimu zilizotolewa na UNICEF zinaonesha mtoto mmoja kati ya watatu wanakabiliwa na utapiamlo mkali.
“Familia nyingi nilizokutana nazo wanaishi chini ya dola moja kwa siku na nyingine hazijakula kwa siku tatu” alisema Balozi huyo mwema wa UNICEF na kueleza hiyo ndio picha halisi ya athari za mabadiliko ya tabianchi na kushukuru UNICEF kwa juhudi zake za kusaidia watoto kwakuwapatia matibabu na vyakula vyenye virutubisho kwani wengi wao wana utapiamlo mkali.
Juhudi za UNICEF nchini kenya
UNICEF imeongeza juhudi za kutoa misaada kama vile kugawa maziwa yenye lishe na pia ni matibabu kwa watoto wenye utapiamlo katika vituo vya afya pamoja na kuisaidia serikali ya kenya kwenye kutambua na kutibu Watoto wenye utapiamlo hususani wale walioko katika mazingira magumu kufikika.
Kiujumla ukame uliosababishwa na kutonyesha mvua kwa misimu minne umewaacha watoto milioni 1.4 katika uhaba mkubwa wa chakula chenye lishe, maji safi, huduma za afya, elimu na kuishi katika mazingira yenye migogoro na hata sasa inakadiriwa msimu wa tano utakuja bila mvua na kufanya hali kuzidi kuwa mbaya kwa Watoto hao na familia zao na hawatakuwa na namna nyingine zaidi ya kutegemea misaada ya kibinadamu kama sehemu kubwa ya kuwawezesha kuishi.
Kaimu mwakilishi mkaazi wa UNICEF nchini Kenya Jean Lokenga aliambatana na Balozi mwema Priyanka Chopra Jonas katika kaunti ya Turkana ambapo alimweleza namna UNICEF inavyofanya kazi bila kuchoka kwakushirikiana na serikali ya Kenya na wadau wengine kupunguza vifo vya watoto waishio katika mazingira magumu.
“Hali hii mbaya inaweza ikaongezeka zaidi katika msimu ujao wa mvua, mahitaji muhimu kama vile chakula cha ambacho pia ni matibabu kwa Watoto wenye utapiamlo kinazidi kupungua kwasababu hatuna ufadhili wakutosha. Kenya na eneo lote la ukanda huu tuna uhitaji wa haraka kwa ajili ya kuongeza huduma zetu za usaidizi” Lokenga alimueleza Balozi mwema Chopra Jonas.
Alimshukuru pia kwa ziara yake hiyo kwani aliamini kuwa uwepo wake hapo utachangia kuonesha hali hali na kujenga uelewa kwa dunia juu ya changamoto zinazowakabili Watoto wa Pembe ya Afrika
Aliyoshuhudia katika Kaunti ya Turkana
Mtoto Keeza
Katika kituo cha kutibu Watoto wenye utapiamlo kilichopo katika hospitali ya Lodwar mjini Lodwar ambacho Watoto wenye utapiamlo mkali wamelazwa hapo Chopra Jonas na mtoto Keeza mwenye umri wa miaka miwili aliyelazwa kutokana na kuugua utapiamlo mkali.
Kutokana na mwili wake kutokuwa na uwezo wa kinga madhubuti mtoto Keeza pia amepata maambukizi ya ugonjwa wa Malaria, nimonia na uvimbe. Shukran kwa muhudumu wa afya aliyekuwa akitembelea familia za mashinani katika Kijiji cha Nakwemekwi mtoto huyo aliweza kukimbizwa hospitali hapo ili kupatiwa huduma na sasa amelazwa akiendelea na matibabu.
Akiwa na huzuni kwa hali aliyomkuta nayo Keeza Chopra Jonas alisema “Hali halisi ni kuwa kuna Watoto wengi kama Keeza na hawapati matibabu yanayohitajika. Watoto ambao hawana kinga Madhubuti tayari wanazidi kuathirika na kukosa lishe na hawawezi kupambana na magonjwa, hii inamaanisha wapo hatarini kufa kutokana na magonjwa hayo na njaa, hali hii inatia huruma lakini inaweza kuzuilika isipokuwa tu ni lazimia tuchukue hatua sasa ili kuokoa mamilioni ya Watoto ambao wamesukuwa katika ukingo wa kifo.”
Kijiji cha sopel
Katikati ya kaunti ya Turkana Bi. Chopra Jonas alikutana na wananchi waathiriwa wa ukame, wengi wa wanakijiji hicho ambao ni wafugaji wameyahama makazi yao kwani hakuna maji ya kunywesha mifugo pamoja na wao wenyewe.
Wananchi hao wamejengewa kisima cha maji kinachotumia nishati ya jua na sasa maji yanayopatikana nayawatosha wananchi wa kijiji hicho pamoja na shule na zahanati ya eneo hilo.
Katika eneo zila la pembe ya Afrika UNICEF inatoa kifurushi cha dharura kwa kila familia ambacho kina vifaa muhimu vya kuwawezesha kutibu maji wanayochota ili waweze kupata maji safi na salama ya kunywa na matumizi mengine ya nyumbani.
Familia hizo zilizoathika pia zinapatiwa fedha taslimu kwa ajili ya mahitaji muhimu kama vile gharama za matibabu na kuwalinda watoto ili wasiache shule na kuongia katika ndoa za utotoni.
Mama Hanna Moru
“Nimekutana na mama mmoja jina lake Hanna Moru na nimependa namna alivyo na moyo wa ushujaha katikati ya madhila haya ya ukame unaowakabili” alisema Bi. Chopra Jonas nakusimulia mazungumzo yao “aliniambia jinsi ambavyo ameweza kubaki kijijini kwake sababu tu kuna chanzo cha maji ambacho kinahudumia familia yake. Mtoto wa Hanna mwenye umri wa miaka 143 aitwaye Celine sasa anaweza kwenda shule, na mtoto mwingine mdogo wa Hanna anapata chanjo na anapokea chakula cha lishe ambacho pia ni matibabu ya utapiamlo wanachopewa kwenye zahanati kijiji hapo.”
UNICEF inatoa wito kwa serikali, sekta binafsi, na watu binafsi kusaidia kwa kutoa msaada wa haraka wa kifedha kwa ajili ya kukabiliana na ukame ukaokabili nchi zilizoko katika Pembe ya Afrika. Kadiri hali inavyoendelea kuzorota ndio mahitaji yanazidi kuongezeka hivyo UNICEF nayo inahitaji kupanua huduma zake na kuhakikisha wanawafikia wote wenye uhitaji .