Wanawake viongozi ni chachu ya mabadiliko chanya kwenye jamii
Wanawake viongozi ni chachu ya mabadiliko chanya kwenye jamii
Hii leo kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa kandoni mwa mjadala mkuu wa Baraza Kuu, Wanawake wakuu viongozi wa nchi na serikali wamezungumzia nafasi muhimu ya uongozi wa wanawake kwenye kutatua changamoto zinazokabili dunia hivi sasa sambamba na kujenga mustakabali endelevu.
Taarifa iliyotolewa leo jiijni New York, Marekani na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kushughulikia masuala ya wanawake, UN Women, imesema wanawake hao wakuu wa nchi na serikali wamekutana kupitia jukwaa jipya la wanawake viongozi la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, UNGA, jukwaa lililoanzishwa mwaka jana wakati wa #UNGA76.
Mkutano wao ukiwa na maudhui, Majawabu ya mabadiliko kutoka kwa wanawake viongozi kwa changamoto za sasa zinazohusiana, umeonesha kuwa ushiriki kamilifu na fanisi wa wanawake kwenye siasa na kupitia maamuzi ni muhimu kushughulikia vipaumbele vya dunia kwa ufanisi na ujumuishi.
Waliohudhuria ni pamoja na Rais Novák of Hungary, Waziri Mkuu wa Bangladesh Sheikh Hasina, Waziri Mkuu wa Iceland Katrín Jakobsdóttir, WAziri Mkuu wa Samoa, Fiamē Naomi Mataʻafa na WAziri Mkuu wa Uganda Robinah Nabbanja, halikadhalika WAziri Mkuu wa Aruba Evelyn Wever-Croes of Aruba. Wengine ni Waziri Mkuu wa St. Maarten Silveria E. Jacobs na Waziri Mkuu wa zaman iwa New Zealand Helen Clark.
Tukio liliandaliwa na Ofisi ya Rais wa Baraza Kuu la UN pamoja na ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kushughulikia masual ya wanawake, UN Women kwa ushirikiano na Baraza la wanawake viongozi, CWWL.
Wanawake wakiongozi huleta mabadiliko - Kőrösi
Akizungumza kwenye tukio hilo, Rais wa UNGA77 Csaba Kőrösi, amesema uongozi wa wanawake huleta mabadiliko. Viongozi wanawake tulio nao hii leo hapa ni Ushahidi hai wa hoja hiyo. Utawala jumuishi unaweza kusababisha sera ambazo zinaweka mazingira ya mabadiliko chanya katika kipindi kirefu,
Amesema kwa kujumuisha maoni ya wanawake kutoka makundi mbalimbali hasa katika ngazi ya juu, serikali zinaweza kuumba na kulenga kwa ufanisi majawabu kwa wale wenye uhitaji.
Katika nchi 193 wanachama wa Umoja wa MAtaifa, ni nchi na serikali 28 tu ndio zinaongozwa na wanawake - Ripoti ya UN
Bi. Sima Bahous, Mkurugenzi Mtendaji wa UN Women, amesema pindi wanawake wengi zaidi wanaongoza kwenye Nyanja za kisiasa na umma, kila mtu ananufaika hasa kwenye majanga. Kizazi kipya cha watoto wa kike kinaona mustakabali wao bora. Elimu, afya, malezi ya watoto na ukatili dhidi ya wanawake vinamulikwa zaidi na vinapata majawabu.”
Majanga yamedhihirisha nafasi chanya ya wanawake viongozi
Majanga ya hivi karibuni duniani kama vile COVID-19, mabadiliko ya tabianchi na mizozo , yamedhihirisha mabadiliko chanya yanayokuweko pindi wanawake wanashiriki kwenye maamuzi iwe kwenye mabunge au ofisi za umma.
Kipimo cha ufuatiliaji wa masuala ya jinsia, Gender Response Tracker kinaonesha kuwa serikali zenye uwakilishi mkubwa wa wanawake kwenye mabunge zilipitisha sera zinazozingatia masuala ya jinsia kukabili COVID-19, ikiwemo sera zinazolenga moja kwa moja kuimarisha usalama wa wanawake kiuchumi.
Kwa kasi ya sasa, usawa wa kijinsia bungeni kufikiwa 2062
Katika nchi 193 wanachama wa Umoja wa MAtaifa, ni nchi na serikali 28 tu ndio zinaongozwa na wanawake.
Kwa mujibu wa ripoti ya Umoja wa Mataifa, kwa kasi ya sasa ya maendeleo, uwakilishi sawa bungeni hautafikiwa hadi mwaka 2062.
Bi. Katrín Jakobsdóttir, Waziri Mkuu wa Iceland na Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Viongozi duniani amesema, ni imani yake thabiti k uwa dunia inahitaji wanawake wengi zaidi viongozi na viongozi kutoka pande mbalimbali na uzoefu tofauti wa maisha.”