Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNMISS imelaani vikali mashambulizi mapya kwenye kambi ya wakimbizi wa ndani Adidiang Upper Nile

Walinda amani wa Ethiopia wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa huko Sudan Kusini (UNMISS) wakisindikiza kikundi cha wanawake nje ya eneo linalosimamiwa na Umoja wa Mataifa na hivyo kuwawekea mazingira salama ambapo wanaweza kutafuta kuni bila kuwa katika hatari
UNMISS\Nektarios Markogiannis
Walinda amani wa Ethiopia wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa huko Sudan Kusini (UNMISS) wakisindikiza kikundi cha wanawake nje ya eneo linalosimamiwa na Umoja wa Mataifa na hivyo kuwawekea mazingira salama ambapo wanaweza kutafuta kuni bila kuwa katika hatari ya kushambuliwa. (Picha ya Machi 28, 2017)

UNMISS imelaani vikali mashambulizi mapya kwenye kambi ya wakimbizi wa ndani Adidiang Upper Nile

Amani na Usalama

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Sudan Kusini UNMISS, umelaani mashambulizi mapya na ghasia zinazofanywa na watu wenye silaha, zinazolenga wakimbizi wa ndani wanaotafuta hifadhi katika eneo la kisiwa cha Adidiang, kilichoko takriban kilomita 40 kusini mwa mji mkuu wa jimbo la Upper Nile wa Malakal.

Kwa mujibu wa taarifa ya UNMIS iliyotolewa leo baadhi ya taarifa za waathirika zinaonyesha kuwa idadi kadhaa ya raia waliokimbia wanaweza kuwa walikufa maji katika Mto Nile. 

Takriban raia 5,000 walikimbilia eneo hilo mwezi uliopita, kufuatia mapigano makali kati ya makundi hasimu yenye silaha huko Tonga, magharibi zaidi yam ji wa Malakal.

Shambulio la hivi punde pia limezua mapigano makali kati ya makundi na jamii tofauti za wakimbizi wa ndani  katika eneo la ulinzi wa raia la UNMISS (POC) ambapo wafanyakazi wa UNMISS walijibu haraka kurejesha utulivu na kutoa ulinzi thabiti kwenye eneo hilo.

UNMISS inatoa wito kwa washambuliaji kusitisha mapigano mara moja na kujiepusha kuwadhuru raia walio hatarini na wakimbizi wa ndani. 

Ujumbe huo pia unatoa wito kwa mamlaka za serikali na kitaifa kuingilia kati haraka ili kupunguza hali hiyo na kulinda maisha ya raia.

Walinda amani wa Umoja wa Mataifa wametumwa kwendfa kuokoa raia wanaozama majini na kutoa ulinzi kwa watu walioathirika. 

UNMISS inawashirikisha wadau wote wanaohusika, ikiwa ni pamoja pande zinzokinzana, mamlaka, na jumuiya za mitaa ili kuwezesha kuchukuliwa hatua za pamoja kwa wakati muafaka.