Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wafanyabiashara wa Afrika Mashariki wakutana kwenye maonesho jijini Mwanza Tanzania

Bidhaa zilizotengenezwa kwa mikono
Evarist Mapesa/ UN NEWS Kiswahili
Bidhaa zilizotengenezwa kwa mikono

Wafanyabiashara wa Afrika Mashariki wakutana kwenye maonesho jijini Mwanza Tanzania

Ukuaji wa Kiuchumi

Lengo namba 17 la Malengo ya Maendeleo Endelevu ya umoja wa mataifa katika kipengele kinachozungumzia biashara linahimiza biashara huria na utandawazi unavyoweza kuleta manufaa na kuzitaka nchi kujiunga kwa kupamoja ili kupata manufaa kutoka kwanye mifumo ya biashara kwa pande zote.

Na hicho ndicho kinachofanyika hapa jijini Mwanza ambapo wafanyabiashara kutoka mataifa ya afrika mashariki ambayo ni kenya Uganda, Rwanda, Burundi, Sudan kusini na wenyeji Tanzania wanakutana Kwenye maonesho yenye lengo la kupanua wigo wa bidhaa zao.

Maonesho haya yanatajwa kuwarahisishia wafanyabiashara hawa kutanua wigo wa bidhaa zao katika nchi wanachama wa jumuiya ya afrika mashariki.

Ojok James Onono ni afisa Habari wa Chuo kikuu cha Gulu kutoka nchini Uganda ambacho kinajihusisha na utafiti Pamoja na utenegenezaji wa dawa asilia, anasema wamekuja katika maonesho haya ili watu wajifunze kile wanachokifanya.

“Maonesho haya ni muhimu kwetu kwasababu ni jukwaa tunalolitumia kukutana na watu na kuwaonesha nini tunachokifanya, kama mtu atapenda kuja kujifunza namna ya kutengeneza dawa kwa kutumia mitishamba anaweza kuja kwetu Uganda”alisema Onono.

“Matarajio yetu ni kwamba watu watakuja kujifunza kuhusu dawa mbalimbali za tiba asilia tulizonazo, kuwa na mtandao,na kupata watu wengi Zaidi watakaoshirikiana na chuo”,alisema Onono.

Maoenesho ya wafanyabiashara mkoani Mwanza
Evarist Mapesa / UN News Kiswahili
Maoenesho ya wafanyabiashara mkoani Mwanza

Maonesho haya yanatoa fursa kwa wafanyabiashara na wajasiriamali kujitangaza, kuongeza mtandao wa biashara,kuongeza ubora wa bidhaa na kuboresha teknolojia, kutafuta wabia wapya wa kibiashara pamoja na kufanya utafiti wa masoko.

Prisca Lanyero ni mjasiriamali kutoka Uganda anayejishughulisha na utengenezaji wa mikoba, bangili za mikononi, vikapu Pamoja na ushonaji wa mabegi, anasema wajasiliamali waliowengi katika ukanda huu wa afrika mashariki wanapenda kufanya biashara zinazovuka mipaka kutoka katika mataifa yao Kwenda nchi Jirani ili kujipanua kibiashara, lakini suala hilo huwa ni gumu kutokana na mitaji yao kuwa midogo.

“Watu wanaogopa kufanya bishara kwasababu hawana mitaji,wanatamani kuja lakini hawana mitaji, hilo ndilo tatizo,Katika maonesho haya nategemea kupata kiasi kikubwa cha fedha,na biashara yangu itakua kubwa na Kupaa juu Zaidi”,alisema Lanyero.

Baadhi ya watu wamekuwa wakiogopa kuanzisha biashara wakihofia kuwa watapata hasara ama kufirisika kabisa, hivyo kuwaweka katika hatari ya mstari mwekundu wa kudumbukia katika umaskini uliopindukia kutokana na kwamba miongoni mwao huishi chini ya dola moja kwa siku.

Lakini Tadei Ng’uto kutoka nchini Tanzania anatoa neno kwa wananchi wanaoishi katika nchi za jumuiya ya afrika mashariki “kuanzisha biashara siyo jambo la kuogopa, na hao ambao wanaogopa kitu kimoja wapo wanachotakiwa wakifanye ni kuvaa ujasiri kiasi cha kwamba  kutaka kufanya kile alichokuwa nacho kiweze kuwa kikubwa Zaidi ya hivyo alivyo”,alisema Ng’uto.

“awe na kiu ya kutaka kutanuka kibiashara na utoaji wa huduma kwa watu wa ndani na nje ya nchi, kwahiyo kikubwa Zaidi lazima pia usimamie maono yako ambayo ulikuwa umejiwekea tangu mwanzani”,aliongeza Ng’uto.

Haya ni maonesho ya 17 kufanyika katika nchi wanachama wa jumuiya hii ya afrika mashariki ambapo mataifa ya Tanzania,kenya Uganda, Rwanda, Burundi na sudan kusin yamekuwa wakihudhuria kila mwaka.

Maonesho ya biashara afrika mashariki yalianza rasmi august 26 na yanatarajiwa kufungwa September 04,2022 huku yakibebwa na kaulimbiu inayosema Lugha ya Kiswahili nguzo mahsusi katika kukuza na kuendeleza biashara,viwanda na kilimo afrika.