Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Asante Kenya kwa kutupa utaifa sasa hofu hatuna tena:Washona 

Branjimeni Mshawa Ndooro, mmoja wa watu wa jamii ya Washona waliopiga kura kwa mara ya kwanza katika uchaguzi mkuu wa Kenya mwaka 2022 baada ya kupatiwa uraia mwaka 2021.
UNIC Nairobi/Abdikarim Haji
Branjimeni Mshawa Ndooro, mmoja wa watu wa jamii ya Washona waliopiga kura kwa mara ya kwanza katika uchaguzi mkuu wa Kenya mwaka 2022 baada ya kupatiwa uraia mwaka 2021.

Asante Kenya kwa kutupa utaifa sasa hofu hatuna tena:Washona 

Haki za binadamu

 Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR lilipitisha azimio la kumaliza tatizo la watu wasiokuwa na utaifa ifikapo mwaka 2024. Miaka 2 kabla ya lengo hilo kutimizwa, Kenya imepiga hatua katika harakati za kuwatambua rasmi na kuwapa utaifa Washona walio na asili ya Zimbabwe.

UNHCR imekuwa mstari wa mbele kuiunga mkono Kenya kupitia kampeni yake ya kimataifa ya #IBelong kampeni ya kumaliza tatizo la kutokuwa na utaifa iliyozinduliwa miaka michache iliyopita.

 

 

Kabila la washona kutoka Zimbabwe ambao hivi sasa wamepatiwa utaifa nchini Kenya, ndio wamefanikiwa kupiga kura kwa mara ya kwanza katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu tangu kutambulika rasmi na serikali. Washona waliingia Kenya miaka 1960 wakieneza dini halikadhalika kufanya kazi kama vijakazi wa Waingereza.

 

 

Tangu watambuliwe rasmi mwaka jana wa 2021, wameweza kupokea vitambulisho na hata hati za kuzaliwa kwa baadhi yao.

 

Mwanamke huyu wa Kishona ni mmoja wa watu wasio na utaifa nchini Kenya
© UNHCR/Anthony Karumba
Mwanamke huyu wa Kishona ni mmoja wa watu wasio na utaifa nchini Kenya

 

UNHCR inapinga hali ya kukosa utaifa

 

 

Hatua ya washona kupatiwa utaifa wa Kenya inaenda sanjari na kampeni ya shirika la Umoja wa Mataifa la Wakimbizi UNHCR ya kuondoa hali ya kutokuwa na utaifa ifikapo mwaka 2024.

 

Kampeni ilianza mwaka 2014 na inaunga mkono azimio la kupunguza idadi ya watu wasiokuwa na utaifa duniani azimio ambalo lililopitishwa mwaka 1961 kwenye kongamano la UNHCR mjini New York Marekani na kuanza kutekelezwa rasmi mwaka 1975.

 

 

Tangu jamii ya Washona kuanza kupatiwa utaifa wa Kenya takribani washona 5000 waliomba na kupokea vitambulisho rasmi vya Kenya. Wengine wapatao 1600 ambao hawakuwa na uraia walipokea hati za kuwatambua kisheria.

 

Marian Mungani alizaliwa Kenya na anaamini kuwa,” Sasa maisha ya wanangu yatabadilika sio kama ilivyokuwa kwangu mimi.Watoto wangu watasoma vizuri na kupata mambo mazuri zaidi maishani.Mimi nilizaliwa hapa lakini sikuweza kusoma.”

 

 

Mwaka 2019 Kenya iliitambua jamii ya Washona na kuifanya kuwa kabila la 45 lililo na watu wasiopungua Elfu 4.

 

Faida Gawasa ni mmoja ya wakongwe wa jamii hiyo iliyowasili miaka ya 1960 na akielezea hisia zake tangu wapate sauti ya kuwa Wakenya anasema kabla ya kupata hati za uraia, Washona wamekuwa wakiishi katika hali yenye changamoto kwani hawakuweza kutimiza vigezo vya kufanya biashara halali au hata kupata elimu kamili.

 

Mwanamke, ambaye wazazi wake wanatokea Zimbabwe amekuwa mtu wa kwanza asiyekuwa na utaifa kwenda chuo kikuu nchini Kenya.
© UNHCR/Anthony Karumba
Mwanamke, ambaye wazazi wake wanatokea Zimbabwe amekuwa mtu wa kwanza asiyekuwa na utaifa kwenda chuo kikuu nchini Kenya.

 

Robert Mungani anaunga mkono hilo akisema,”Awali sikuweza kuwa na uhuru wa hata kununua kadi ya simu.Nililazimika kuomba usaidizi kwa wengine kabla ya kupata kitambulisho rasmi.Kwa sasa natembea bila hofu ya kushikwa na ninaweza kufanya nikitakacho kwani niko huru.”

 

 

Watoto wa Kishona walishindwa kufanya mitihani ya kitaifa kwa kukosa hati za kuzaliwa ijapokuwa ni wazaliwa wa Kenya. Jacob Thamini alipata tabu alipojitahidi kumaliza shule na kwa mtazamo wake anasema ,”Sasa nitasoma vizuri na kuweza kujipangia maisha.Nilitatizika awali lakini kuna nuru ya yajayo mbele ya safari.Niliweza kupiga kura na kuwachagua niwatakao.Nafurahi sana.”

 

 

Madhila ya kutokuwa na utraifa

 

 

Washona walishindwa kutembea na kuwa huru kwa kukosa hati muhimu za uraia. Walipowasili Kenya walikuwa na hati za kusafiria za Uingereza.

 

Baada ya Kenya kupata uhuru mwaka 1963 walipewa nafasi kusajiliwa kuwa wakenya lakini wengi wao waliipoteza fursa hiyo baada ya kupitwa na wakati.

 

Hilo liliwafanya kukosa utaifa kwani hawakutambulika Zimbabwe, Kenya au hata Uingereza.

 

Jamii ya Washona aghalabu wanapatikana Githurai,Kinoo,Kiambaa, Hurligham katika kaunti za Nairobi na Kiambu na hata nje ya maeneo ya pwani.

 

Na uamuzi wa Kenya kuwapatia uraia umebadilidi maisha yao na vizazi vyao vijavyo.