Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baada ya zaidi ya nusu karne ya kutokuwa na utaifa, Washona wapiga kura kwa mara ya kwanza Kenya

Branjimeni Mshawa Ndooro, mmoja wa watu wa jamii ya Washona waliopiga kura kwa mara ya kwanza katika uchaguzi mkuu wa Kenya mwaka 2022 baada ya kupatiwa uraia mwaka 2021.
UNIC Nairobi/Abdikarim Haji
Branjimeni Mshawa Ndooro, mmoja wa watu wa jamii ya Washona waliopiga kura kwa mara ya kwanza katika uchaguzi mkuu wa Kenya mwaka 2022 baada ya kupatiwa uraia mwaka 2021.

Baada ya zaidi ya nusu karne ya kutokuwa na utaifa, Washona wapiga kura kwa mara ya kwanza Kenya

Haki za binadamu

Wakati raia wengine wa Kenya wakisubiri historia ya kumshuhudia Rais wa 5 wa nchi hiyo ya Afrika Mashariki, watu jamii ya Shona waliowasili Kenya mwanzoni mwa miaka ya 1960 wakitokea Zimbabwe wakieneza dini na wakiwa vijakazi wa waingereza hatimaye wameonja moja ya faida za uraia kwa kupiga kura kwa mara ya kwanza kwani tangu Kenya ilipopata uhuru mwaka 1963.

Watu hao walisalia bila utaifa hadi mwaka jana 2021 serikali ya Kenya ilipowapatia uraia kwa kuzingatia kampeni ya hivi karibuni ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR ya kutokomeza tatizo la ukosefu wa utaifa ifikapo mwaka 2024. Mzee huyu wa makamo, Branjimeni Mshawa Ndooro ni miongoni mwa waliopiga kura kwa mara ya kwanza, anasema, mimi ni mmoja wa watu wa jamii ya washona ambao walipewa uraia juzi na serikali, nimeweza kupiga kura ili na sisi tuweze kujiunga na wale wengine ambao ni Wakenya." 
 
Miaka mitatu iliyopita, serikali ya Kenya kwa kushirikiana na UNHCR na wadau wengine, iliwapatia vyeti vya kuzaliwa zaidi ya watoto 600 wa asili ya jamii ya Shona na hivyo wakawa raia wa Kenya huku wazazi wao ambao wakisalia bila utaifa hadi mwaka 2021 akiwemo Mzee Ndooro  anasema, "tunaweza kusema wengi tumezaliwa hapa. Hizi shida tulikuja kuzijua wakati wazazi wetu waliofariki dunia, tulipokuwa sasa sisi tumezaa watoto na ikahitajika watoto huko shuleni wajiandikishe wapate vyeti vya kuzaliwa. Hapo ndipo tulipoanza kukutana na shida. Lakini kwa wito mwema, wale wenzetu Wakenya kule mashinani waliweza kutusaidia mapaka serikali, Umoja wa Mataifa na Kamisheni ya haki za binadamu ya Kenya walipoingia. Tunamshukuru Rais Uhuru Kenyatta kwa huruma zake, Mungu alimgusa roho hii shughuli ikafanikishwa ili na sisi tujisikie kama wanadamu, kama wananchi wale wengine. Tumeonja utamu wa kuwa raia."
Historia ya Washona Kenya

Washona walifika Kenya mwaka wa 1960 na kuishi kama watu wasio na utaifa kwa karibu miongo sita hadi, Julai 28, 2021, walipotambuliwa kama kabila la 45 la Kenya. Wakiwa na stakabadhi zote zinazohitajika, walijiandikisha kupiga kura, na hatimaye, Jumanne, Agosti 9, 2022 Washona, waliotoka Zimbabwe, walipiga kura kwa mara ya kwanza kama raia wa Kenya.  

"Ilikuwa safari ndefu kwetu kama watu. Bila cheti cha kuzaliwa na kitambulisho cha kitaifa, si rahisi kufanya kazi katika nchi. Tunashukuru sana Serikali ya Kenya kwa kututambua kama jamii," anasema Benjamin Muregerera, kiongozi wa Jumuiya ya Washona. Alikua raia kamili wa Kenya wakati Rais Uhuru Kenyatta alipowatambua kama kabila la 45 ya nchi hiyo.  

Washona walifika Kenya kutoka Zimbabwe kama wamishonari wa Kikristo katika miaka ya 1960. Walibeba pasipoti za Uingereza na walisajiliwa kama raia wa Uingereza.  

Baada ya uhuru wa Kenya mwaka wa 1964, Washona walikuwa na nafasi ya miaka miwili kusajiliwa kama Wakenya, jambo ambalo wengi walikosa. Pia, hawakuweza kujiandikisha walikotoka kwa sababu hawakuwa tena raia wa nchi walikozaliwa, hivyo kuwafanya wasiwe na utaifa.  

Kutokuwa na utaifa sio utambulisho mzurikuishi nao. Kimsingi, inakataza mtu kupata kile ambacho raia wanakichukulia kuwa haki za kuzaliwa. Ukosefu wa kitambulisho cha kitaifa, hati moja muhimu zaidi ambayo raia yeyote lazima awe nayo ili kupata huduma, ni kilema kikubwa.  Alipoulizwa ni changamoto zipi walizokabiliana nazo kabla ya Utambulisho Muregerera, anayefahamika kwa jina la 'Mhofu' (jina la ukoo) alisema karibu kila biashara inahitaji kitambulisho cha taifa ambacho Jamii yake haikuwa nacho. Ilikuwa vigumu kwa Jamii iliposimamishwa na polisi kwa sababu hawakuwa na kitambulisho cha taifa. Baadhi walikamatwa kwa kukosa vitambulisho, na jaribio la kuwafukuza nchini lilisaidia kukutana na Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR ambalo liliwasaidia kutatua hali yao ya kutokuwa na utaifa hadi kutambuliwa kwao mwaka 2021.  

Wanachama wa Jamii ya Washona waliweza tu kuhudhuria shule hadi shule ya upili (sekondari) lakini walipata changamoto za kuingia katika elimu ya juu ambapo hati za utambulisho ni za lazima. Kutambuliwa kwa Jamii yao kama sehemu ya Kenya sasa kumeondoa mkwamo huo.    

Kanisa la The Gospel of God Church yaani Kanisa la Injili ya Mungu ni kanisa la wamisionari la watu wa Shona ambalo Baba Joanne alianzisha. Bwana. Muregerera, aliyezaliwa nchini Kenya, ni kizazi cha kwanza cha Washona, na anafurahi kuwa amebeba kitambulisho cha kitaifa ambacho kina jina la baba yake, anasema, "siwezi kukuambia jinsi mimi na jamii yangu tunavyojisikia.”    

Tangu kutambuliwa kwao, angalau wanajamii 5,000 wa jamii ya Washona wametuma maombi na kupokea vitambulisho vya Kenya huku wanajumuiya 1,649 wa jamii ya Washona, ambao walikuwa hawana utaifa wakiwa tayari wamekabidhiwa vyeti vya uraia.  

Kijana mmoja aliyezaliwa mwaka 1990, Chinyanga aanasema vitambulisho hivyo ni nyenzo muhimu kwa urithi wao kwa sababu watoto wao watajua walikotoka kwa sababu watakuwa wamebeba jina lao la asili la Zimbabwe.  

Washona wameishi bega kwa bega na wenyeji, na wanazungumza Kishona chao kwa ufasaha na lugha za kienyeji, ikiwa ni pamoja na Kiswahili. Wanasema hawakuwahi kukumbana na chuki na wakazi wa eneo hilo na wameoana na Wakenya ambao wamejiunga na imani yao.  

Kuna zaidi ya Washona 5,000 waliosambaa katika wakazi wote wa Kenya huko Kiambu, Meru, Embu, Laikipia, Kericho, Narok, Kajiado, Mombasa na Malindi.