Mauaji ya mwandishi wa Habari Pakistan, UNESCO yataka uchunguzi ufanyike
Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni UNESCO limelataka uchunguzi ufanyike kuhusu mauaji ya mwandishi wa Habari Ishtiaq Sodharo yaliyotokea huko Khairpur, mkoa wa Sindh nchini Pakistan Julai Mosi, 2022
Taarifa ya shirika hilo iliyotolewa leo huko Paris Ufaransa imemnukuu Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO Audrey Azoulay akisema “Nalaani mauaji ya Ishtiaq Sodharo. Waandishi wa habari wana jukumu muhimu la kuhabarisha jamii na haki yao ya kufanya hivyo lazima ilindwe. Ninatoa wito kwa mamlaka kutumia juhudi zote kuchunguza sababu za mauaji ya Ishtiaq Sodharo na kuwafikisha mahakamani wahusika wa mauaji yake”.
Marehemu Sodharo alikuwa akifanya kazi katika kampuni ya kila wiki ya Sindhi Chinag, alipigwa risasi nje ya nyumba yake na kufariki akiwa hospitali kutokana na majeraha aliyopata wakati wa shambulio hilo.
Miongoni mwa shughuli za UNESCO ni kukuza usalama wa waandishi wa habari kupitia uhamasishaji wa kimataifa, kuwajengea uwezo na kwa kuratibu utekelezaji wa Mpango wa Utekelezaji wa Umoja wa Mataifa kuhusu Usalama wa Wanahabari na Suala la Kutokujali.