Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wahamiaji wafariki jangwani kwa kiu:IOM

Uhamishwaji wa wahamiaji wa nchi ya tatu ambao walikuwa wamekwama katika kituo cha mapokezi Misrata, Libya. (Maktaba)
IOM
Uhamishwaji wa wahamiaji wa nchi ya tatu ambao walikuwa wamekwama katika kituo cha mapokezi Misrata, Libya. (Maktaba)

Wahamiaji wafariki jangwani kwa kiu:IOM

Wahamiaji na Wakimbizi

Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji IOM limesikitishwa na vifo vya wahamiaji wasiopungua 20 vilivyotokea katika jangwa la nchi ya Libya na kutoa wito  kwa mataifa ya Libya na Chad kuchukua hatua kali ili kulinda wahamiaji kwenye mpaka wa nchi hizo.

Taarifa ya IOM kutoka Geneva nchini Uswisi inasema shirika la huduma ya afya ya dharura la Libya mnamo tarehe 28 mwezi Juni walioripoti kukuta miili ya watu 18 wanao aminika kuwa raia wa Chad na miili ya watu wawili raia wa Libya karibu na mpaka wa Libya na Chad ambao wanaaminika vifo vyao vimesababishwa na kiu wakiwa jangwani.

Mkuu wa IOM nchini Libya Federico Soda amesema “Vifo vya watu 20 katika jangwa la Libya utumike kama wito mwingine wa kuamsha jumuiya nzima ya kimataifa na ukumbusho kwamba tuko mbali sana kufikia lengo la 'kutomwacha mtu nyuma', la malengo ya maendeleo endelevu a Umoja wa Mataifa kufikia mwaka 2030.”

Amekumbusha kuwa hasara dunia inayopata kupitia vifo vinavyotokea katika “Bahari ya Mediterania na katika majangwa ya kusini mwa Libya hazikubaliki na zinaweza kuepukika.”

Jangwa la Sahara ni kati ya njia hatari na mbaya zaidi za uhamiaji ulimwenguni

Kulingana na takwimu zilizotolewa na “mradi wa kusaka wahamiaji waliopotea” unaoendeshwa na IOM, zaidi ya vifo 2,000 vya wahamiaji vimerekodiwa tangu 2014 katika Jangwa la Sahara pekee, lakini wataalam wanaamini kuwa idadi inaweza kuwa ni kubwa zaidi.

Boti ilizama pwani ya Libya ikiripotiwa kubeba zaidi ya watu 120 na kati yao ni 47 tu walinusurika kifo.
IOM/Hussein Ben Mosa
Boti ilizama pwani ya Libya ikiripotiwa kubeba zaidi ya watu 120 na kati yao ni 47 tu walinusurika kifo.

Wahamiaji walindwe

Kwa upande wake Anne Kathrin ambaye ni Mkuu wa IOM nchini Chad amesema tangu kuimarishwa kwa uchimbaji wa dhahabu kaskazini mwa nchi ya Chad mwaka 2012, eneo la mpaka wa Chad na Libya limeshuhudia ongezeko kubwa la matukio yanayohusiana na wahamiaji kutelekezwa na wafanyabiashara na wasafirishaji, au wasafirishaji kupotea.

Anne amekazia kauli ya Mkuu wa IOM Libya kwakueleza kuwa “Majanga haya lazima yachukuliwe kuwa ni wito wa hatu kuchukuliwa ili kutoa angali viwango vidogo vya ulinzi kwa wahamiaji, kuwezesha shughuli za utafutaji na uokoaji, kuimarisha usimamizi wa mipaka wa kibinadamu, na kutoa msaada unaohitajika haraka katika eneo hili la mbali sana.”

Mwezi juni 20222, mapigano kati ya wachimba madini wa dhahabu katika mji wa Kouri Bougoudi, karibu na mpaka na Libya, yalisababisha mamia ya watu kupoteza maisha na takriban wafanyakazi 10,000 wa migodini kaskazini mwa Chad kukimbia makazi yao.

“Kwa kukosekana kwa njia salama za uhamiaji, wahamiaji hutumia barabara hatari, huangukia mikononi mwa wafanyabiashara, au kupotea jangwani -na mara nyingi matokeo mabaya.”

Zaidi ya wahamiaji 45,000 walirekodiwa katika Vituo vya Ufuatiliaji vya wahamiaji vya  Faya, Zouarké na Ounianga Kébir Kaskazini mwa Chad kati ya Januari na Machi 2022. Miongoni mwa wahamiaji waliohojiwa na IOM katika kipindi hicho, asilimia 32 walielekea Libya licha ya kukosekana kwa masharti ya kimsingi ya kuhakikisha usalama na ulinzi wao.

IOM inasisitiza wito wake wa ulinzi wa wahamiaji na haki zao kupitia juhudi za kujitolea za utafutaji na uokoaji, na uchunguzi na mashtaka ya wasafirishaji na wasafirishaji haramu wanaotumia fursa ya kukata tamaa na mazingira magumu ya watu.