WHO iko tayari kusaidia DPRK kupambana na mlipuko wa COVID-19
WHO iko tayari kusaidia DPRK kupambana na mlipuko wa COVID-19
Shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani WHO limesema leo kwamba limejitolea kuisaidia Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Korea (DPRK), kukabiliana na janga la COVID-19, baada ya maambukizi yake ya kwanza kutangazwa kwenye vyombo vya habari nchini humo.
Likijibu swali kutoka kwa UN News, shirika la WHO limesema limewasiliana na mamlaka nchini DPRK lakini bado halijapokea ripoti rasmi kutoka kwa wizara ya afya ya nchi hiyo.
Edwin Salvador, mwakilishi wa WHO nchini DPRK ambayo pia inajulikana kama Korea Kaskazini, amesema kuwa shirika hilo limeiunga mkono nchi hiyo katika kuandaa mpango wake wa kitaifa wa kukabiliana na COVID-19.
Vyombo vya habari vya serikali vimesema lahaja ya Omicron imegunduliwa katika mji mkuu, Pyongyang.
Mshikamano na taifa hilo
Kwa kushirikiana na washirika wake ikiwa ni pamoja na shirikam la Umoja wa Mataiofa la kuhudumia watoto UNICEF) na GAVI, muungano wa chanjo duniani, WHO imeunga mkono Korea Kaskazini katika kuandaa mpango wa kupeleka chanjo ya COVID-19.
Mpango huo ulikaguliwa na kuidhinishwa na wadau mbalimbali wa kikanda, na kuruhusu taifa hilo lililojitenga kupokea chanjo za COVID-19 kupitia mpango wa usambazaji wa chanjo unaoongozwa na Umoja wa Mataifa wa COVAX.
WHO imesema inaendelea kufanya kazi na mamlaka ya kitaifa ya DPRK kwa kuwapa taarifa muhimu kuhusu chanjo za COVID-19 zinazopatikana kupitia COVAX.