Mashirika 7 ya Umoja wa Mataifa yaungana kusaidia wafanyabiashara Somaliland
Katika kukabiliana na uharibifu uliosababishwa na moto katika soko huko Hargeisa, Somaliland nchini Somalia, Umoja wa Mataifa umetuma timu ya wataalam wa kiufundi kufanya kazi na serikali ili kutathmini uharibifu na kusaidia ujenzi wa soko jipya.
Video iliypotengenezwa na UNSOM imeonesha moshi ukifuka na maeneo mengine moto ukiendelea ukiteketeza masalia ya eneo la soko la Waheen huko Hargeisa, Somaliland nchini Somalia.
Mohamed Abdullahi Muhamoud alikuwa akifanya biashara katikasoko hili anasema " Biashara yangu ilikuwa ikilisha familia yangu yote… biashara hii ilidumisha wanafamilia wengi ambao maisha yao yalitegemea moja kwa moja. Leo, kama unavyoona, limeharibiwa kabisa. "
Kilio hicho ni kama cha Zainab Hassan Warsame ambaye anashika majivu yaliyoteketeza duka lake la nguo.
“Duka langu lilikuwa limejaa nguo. Nilikuwa nauza aina zote za nguo. Lilikuwa duka kubwa la nguo. Nilikuwa nikiwalisha wazazi wangu wazee, watoto wangu, pamoja na watoto wa binti zangu - kwa jumla maisha ya watu kumi yalitegemea biashara yangu. Nilikuwa mlezi pekee wa familia yangu na walitegemea duka hili, lakini halipo tena.”
Katika uwanja wa ndege wa Somaliland ndege iliyobeba wataalamu kutoka mashirika 7 ya Umoja wa Mataifa wanawasili na kutembelea maeneo ya soko lililoungua pamoja na kufanya mazungumzo na makundi mbalimbali ya wafanyabiashara na serikali ili kuona ni namna gani Umoja wa Mataifa utawasaidia.
Jacqueline Saline Olweya ni naibu mwakilishi mkaazi wa shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo UNDP nchini Somalia baada ya kutembelea maeneo kadhaa na kuzungumza na wananchi ameseme.
“Nakumbuka nilizungumza na mmoja wa wanawake na kumuuliza kuhusu athari ya tukio hili kwake na akataja mambo mawili muhimu. Moja ni pigo analopaswa kubeba ni kubwa kwa sababu ya uharibifu wa mahali alipokuwa akiuza bidhaa zake, na alisimulia hili na athari ambayo inaweza kuwa nayo kwa afya zao wanapofanya kazi. Jambo la pili alilozungumza ni hitaji la mtaji, kuweza kujaza tena duka lake lililo teketea. Na alikuwa anazungumza kuhusu rasilimali chache sana anazopata kila mwaka lakini sasa zimeharibiwa, hana tena kitu, hivyo ziara yetu ya kuzungumza na watu imetusaidia kuwa na taswira ya ubinadamu kwenye janga hilo.”
Timu hiyo imeeleza baada tu ya kukamilika kwa tathmini wataweza kubaini ni rasilimali kiasi gani zinahitajika ili kukidhi mahitaji ya haraka, na ni rasilimali kiasi gani zinaweza kuelekezwa kwenye mahitaji ya muda mfupi na muda mrefu.
Wataalamu hao wa Umoja wa Mataifa wanaofanya tathmini ya janga hilo wanatoka katika Shirika la wa Mpango wa Maendeleo (UNDP), UN-Habitat, Shirika la Chakula na Kilimo (FAO), Shirika la Kazi Duniani (ILO), UN Women, Shirika la Afya Duniani (WHO), Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), Shirika la Uhamiaji (IOM), Ofisi ya Kamishna wa Haki za Kibinadamu (OHCHR) na Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa usaidizi nchini Somalia (UNSOM).