Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mradi wa FISH4ACP walenga kuwainua wanawake wachakataji mkoani Kigoma, Tanzania

Wanawake wafanyabiashara wakiuza dagaa katika mwalo wa Katongo mkoani Kigoma , Tanzania
UN News
Wanawake wafanyabiashara wakiuza dagaa katika mwalo wa Katongo mkoani Kigoma , Tanzania

Mradi wa FISH4ACP walenga kuwainua wanawake wachakataji mkoani Kigoma, Tanzania

Wanawake

Katika baadhi ya jamii wanawake hutafsiriwa kama kundi dhaifu lisilo  na mchango wowote katika maendeleo wakiamini anapaswa kufanya majukumu ya nyumbani pekee lakini ni ukweli usiopingika kuwa kundi hili lina mchango mkubwa katika kuinua uchumi wa familia na Taifa kupitia sekta mbalimbali.

Katika mkoa wa Kigoma, baadhi ya wanawake wamejikita kufanya kazi katika sekta ya uvuvi. Ziada Juma ni mchakataji katika Mwalo wa  Katonga na anaeleza sababu za kufanya kazi hii.

 “Kilichonisukuma haswa haswa ni maisha yalivyonibana ndiyo maana niliona katika kuhangaika huku na huku nikaingia kwenye hizi biashara za kuchakata hapa ziwani na kulingana na maisha magumu ndiyo maana niliingia kwenye hizo biashara,”Amesema Ziada.

Changamoto wanazokutana nazo ni zipi?

“ Hizi biashara zenyewe hazipatikani zinanunuliwa kwa shida, hakuna masoko ya kuuzia tunakaa barabarani hizo mara nyingi na mitaji kuwa midogo ndo changamoto tunazokutana nazo,”Ameeleza.

 Nimefanikiwa pia kuzungumza na Fatuma Ndasalama ambaye ni mfanyabiashara nikamuuliza kuna  umuhimu gani kwa  mwanamke kufanya kazi?

“Maanake unapokuwa unajishughulisha kwa mafano  kama sisi tuna watoto, mtoto anapokuwa amesoma amefaulu baba  yake anaweza kujikuta hana kitu baadaye wewe ukampiga nguvu mwanaume mimi nawashauri tu wanaowakataza wake zao wawape tu ruhusa waendelee kufanya biashara mwanaume anapokuwa amekwama mwanamke anamkwamua,”amefafanua Fatuma.

Mfanyabiashara mwanamke katika  mwalo wa Katongo, Kigoma Tanzania
UN News
Mfanyabiashara mwanamke katika mwalo wa Katongo, Kigoma Tanzania

Aboubakari Milembe naye ni mkazi wa Katonga anatuambia wanawake wana mchango gani katika maendeleo na ujumbe wake kwa kina baba.

“Mwanaume anapoenda kutafuta riziki kuna wakati  anakwama mwanamke katika kuhangaika kwake anafanikiwa kwahiyo inasaidia kifamilia kwa sababu kuna watu wenye familia kubwa, wenye familia za kawaida na familia za chini kwa hiyo naona hilo suala ni muhimu sana katika kutafuta riziki baina ya watu wawili mwanaume na mwanamke mimi nawasihi wawape ruhusa wenzao waende kutafuta riziki,”Amebainisha Aboubakari.

Kwa upande wake  Mratibu wa mradi wa FISH4ACP kupitia FAO, Hashim Muumin anahitimisha kwa kutuambia  namna shirika hilo linagusa wanawake kiuchumi.

“Katika mkakati huu umezingatia masuala ya jinsia hasa hasa kina mama katika uvuvi huu wa Ziwa Tanganyika kwa asilimia zaidi ya 90 ndiyo ambao ni wachakataji wakubwa ushiriki wao katika maamuzi, usimamizi katika mnyororo huu wa thamani wa uvuvi wa  Ziwa Tanganyika umeonekana mdogo  sana kwahiyo mradi huu umelingalia suala hilo na utaenda kulishughulikia kuhakikisha kwamba katika eneo hilo kunaimarika,”Ameeleza Hashim.

Maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani mwaka 2022 yanafanyika chini ya kauli mbiu isemayo "Kizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu"