Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UN yatoa wito wa pande husika katika mvutano mkubwa wa Ukraine kujizuia  

Askari aliyevaa mavazi ya kujificha amesimama kwenye kituo cha ukaguzi kwenye barabara ya vumbi katika eneo la vijijini, lenye miti.
© UNICEF/Christopher Morris Mwanajeshi akilinda kituo cha mwisho cha ukaguzi cha serikali huko Bakhmutka, mkoa wa Donetsk, Ukraine. (Maktaba)

UN yatoa wito wa pande husika katika mvutano mkubwa wa Ukraine kujizuia  

Amani na Usalama

Wakati wa mkutano wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa hii leo Alhamisi unaohusu mgogoro wa Ukraine, Mkuu wa Idara ya Umoja wa Mataifa inayohusika na masuala ya siasa na ujenzi wa amani, Rosemary DiCarlo ametoa wito kwa pande husika kujizuia katika mazingira ya mvutano mkali. 

"Taharuki ndani na karibu na Ukraine ni mkubwa kuliko wakati wowote tangu 2014. Uvumi na shutuma kuhusu uwezekano wa mzozo wa kijeshi zimejaa. Chochote mtu anachofikiria juu ya matarajio ya makabiliano kama haya, ukweli ni kwamba hali ya sasa ni hatari sana." Amesema Rosemary DiCarlo, Msaidizi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Masuala ya Kisiasa, katika mkutano kwanjia ya video kwa wanachama wa Ushauri. 

Bi DiCarlo amekumbushia kuwa masuala yanayochochea mzozo wa sasa ni "tata na ya zamani" na yanahusisha mzozo wa miaka minane mashariki mwa Ukraine na masuala mapana zaidi yanayohusiana na usanifu au mundo wa usalama wa Ulaya. 

"Masuala haya yanaweza na yanapaswa kutatuliwa kupitia diplomasia na matumizi kamili ya mifumo na mifumo mingi ya kikanda iliyopo. Tunaunga mkono juhudi zote hizi, ikiwa ni pamoja na kupitia ofisi nzuri za Katibu Mkuu.” Amesema Bi DiCarlo. 

Makubaliano ya Minsk 

Hata hivyo, Bi DiCarlo ameeleza kujutia kwake kwamba kulikuwa na "maendeleo kidogo, ikiwa yapo, katika utekelezaji wa vifungu mbali mbali vya mikataba ya Minsk". 

Kwa mujibu wa Bi. DiCarlo, makubaliano ya Minsk yanasalia kuwa mfumo pekee ulioidhinishwa na Baraza la Usalama, katika azimio lake nambari 2202, la suluhu la mzozo wa mashariki mwa Ukraine kwa mazungumzo na kwa amani. 

Bi DiCarlo akizungumzia hali ilivyo amesema, "katika suala hili, tunazingatia ripoti za wasiwasi za ukiukaji mpya wa usitishaji mapigano saa chache zilizopita. Hali haipaswi kuruhusiwa kuwa mbaya zaidi. Tunatoa wito kwa pande zote kujizuia kwa wakati huu. Pia tunatoa wito kwa pande zote zinazohusika kujiepusha na hatua zozote za upande mmoja ambazo zinaweza kwenda kinyume na makubaliano ya Minsk, au kudhoofisha utekelezaji wake na kusababisha mvutano mpya, hasa kuhusiana na maeneo fulani ya Luhansk na Donetsk.” 

Jumatatu, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres alielezea wasiwasi wake kuhusu hatari ya mzozo wa kijeshi nchini Ukraine na kutoa wito wa kuimarishwa kwa juhudi za kidiplomasia. "Hakuna mbadala wa diplomasia," alisema. 

Tangu Novemba, Urusi imekusanya maelfu ya wanajeshi kwenye mipaka ya mashariki mwa Ukraine na hivyo kuzua wasiwasi katika nchi za Magharibi, ambazo zinahofia operesheni mpya ya kijeshi dhidi ya Ukraine, baada ya kunyakuliwa kwa Crimea mwaka 2014, sambamba na mzozo ambao umekuwa ukiendelea kwa muda wa miaka minane katika mashariki ya Ukraine. 

Marekani inasema Urusi inaweza kushambulia Ukraine "wakati wowote" lakini Urusi inakanusha nia yoyote ya kichokozi kuelekea Ukraine.