
Marekani yatoa msaada wa taulo za kike kusaidia elimu kwa wasichana Dadaab:UNHCR
Mano Hamdam mwenye umri wa miaka 20 anakumbuka machache sana kuhusu maisha aliyokuwa akiishi huko Kismayo nchini Somalia.
Baba yake alifariki dunia mwaka 2006 na familia ilikabiliwa na changamoto kubwa ya fedha huku mama yake akijaribu kupata rizki kwa kila njia.
Kifo cha baba yake ambaye alikuwa ndio tegemeo kuu la familia pamoja na ukosefu wa usalama nchini Somalia viliilazimisha familia hiyo ya watu wanane kufungasha virago na kukimbilia nchi Jirani ya Kenya mwaka 2006.
Akikua, Mano na dada zake wanne hawakuwa na uwezo wa kununua au kupata taulo za kike na hawakuwa na jinsi bali kutafuta njia mbadala. “Tulirarua nguo zetu vipande vipande na kuvitumia kama taulo za kike.

Kama hatukuwa na smut aliyetusitiri na taulo za kike basi kutumia vipande tulivyochana chana vya nguo zetu ndio ilikuwa suluhu.”
Ukosefu wa taulo za kike kwa wasichana kambini Dadaab mara nyingi husababisha wasichana wa shule kukosa khudhuria masomo kila mwezi wanapokuwa hedhini.
Nino Omar mwenye umri wa miaka 19, anasoma darasa moja na Mano aliye na ndoto ya kuwa profesa wa masuala ya tiba.
Nino anasema taulo za kike wanazopewa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR na wadau wengine hazitoshi. “Kutokana na ukosefu wa nafasi za kazi, familia haziwezi kumudu kununua taulo za kike, Kwa wasichana wengi hata hawana uhaka na kile wanachopaswa kufanya wakati wakiwa kwenye siku zao,” anaongeza.

Kwa mujibu wa Martha Kow-Donkor, afisa wa UNHCR kwenye kambi ya Dadaa, tamaduni na dini pia huwa kizuizi kwa elimu kuhusu afya ya wasichana kwa kuwa elimu kama hiyo haitolewi nyumbani. “Wasichana hutegema marafiki kupata habari ambayo inaweza kuwa imepotoshwa. Kwa hivyo kuna hitaji la elimu ya hali ya juu ya afya na ngono kwa wasicna hawa n ani elimu iliyo sahihi shuleni”

Changamoto hizi zinazowakumba wanafunzi wasichana hazidhuru tu matokeo yao shuleni lakini pia huwapokonya heshima, kujithamini na kujiamini kwao.
Hofu yao kubwa ni kujichafua hali ambayo husababisha kejeli kutoka kwa wanafunzi wa kiume shuleni.
“Kuepuka hili, wasichana huchagua kukosa masomo wakati wa hedhi.
Baadhi ya wasichana huchagua kulala darasani, na baadhi huomba ruhusa kwenda msalani mara kwa mara na kupoteza muda muhimu wa masomo,” anasema afisa huyo wa UNHCR.
Mwezi Agosti mwaka huu 2021 shirika la UNHCR kwenye kambi ya Dadaab lilipokea msaada wa taulo za kike 100,000 ili ziweze kusambazwa kwa wasichana wakimbizi katika shule zote za msingi na upili katika kambi ya Dadaab.
Kutokana na usaidizi huo kutoka kwa wafadhili kama vile serikali ya Marekani ambayo mara kwa mara imetoa bidhaa hizo, sasa wasichana wengi wameanza kuhudhuria masomo kikamilifu.
Mano aliye na matumaini kila wakati, ana ndoto ya kuwa daktari na kuishi na kurejea familia yake nchini Somalia.
“Mara nitakapokamilisha masomo yangu, ninataka kurejea Somalia na kuwaelimisha wasichana kuhusu usafi na ikiwezekena nitengeneze taulo za kike kwa wasichana wote nchini Somalia,” anasema Mano.
TAGS: UNHCR, Dadaab, Somalia, wasichana, taulo za kike, elimu