Michelle Bachelet aanza ziara ya wiki moja Burkina Faso na Niger:OHCHR
Michelle Bachelet aanza ziara ya wiki moja Burkina Faso na Niger:OHCHR
Kamishina Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa mataifa Michelle Bachelet leo ameaza ziara ya siku saba ya kikazi barani Afrika akizuru nchi za Burkina Faso na Niger, kwa mwaliko maalum wan chi hizo.
Katika ziara hiyto itakayomalizika Desemba 4, Bi. Bachelet anaanzia Burkina Faso leo hadi Desemba Mosi.
Na wakati wa ziara hiyo atakutana na Rais Roch Marc Christian Kaboré, Waziri mkuu Christophe Joseph Marie Dabiré na viongozi wengine mbalimbali wa ngazi ya juu.
Pia anatarajiwa kukutana na Rais wa Bunge la taifa na tume ya haki za binadamu ya nchi hiyo, Commission Nationale des Droits Humains.
Nchini Niger ziara yake itaanza tarehe Mosi Desemba hadi tarehe 4 Desemba ambako pia atakutana na Rais Mohamed Bazoum, Waziri mkuu Ouhoumoudou Mahamadou na maafisa wengine wa ngazi ya juu.
Nchini humo pia atakutana na Rais wa bunge la taifa na tume ya taifa ya haki za binadamu, Commission Nationale des Droits Humains.
Wakati wa ziara hiyo katika nchi hizo mbili Bachelet atafanya mazungumzo pia na wanaharakati na watetezi wa haki za binadamu , viongozi wa kijamii na viongozi wa dini, waathirika wa ukiukwaji wa haki za binadamu na vitendo vya ukatili, watu waliotawanywa kutokana na vita na athari za mabadiliko ya tabianchi, mashirika ya asasi za kiraia yanayofanya kazi kutetyea haki za kiraia, kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni.
Mbali ya hao atakutana na kuzungumza pia na maafisa wa ngazi za juu wa kikosi cha pamoja cha Sahel G5.
Mwisho wa ziara yake katika kila nchi atakuwa na mkutano na waandishi wa Habari.