Baada ya miaka 10 ya madhila ya vita famililia Syria ziko hoi:Grandi
Kamishna mkuu wa shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR Filippo Grandi amerejea kutoka nchini Syria na kutoa ombi jipya la kuongeza misaada ya kibinadamu, wakati mchakato wa rasimu ya katiba mpya ya Syria ukianza wiki hii.
Kamishna huyo ambaye amehitimisha ziara ya siku mbili katika taifa hilo lililoghubikwa na vita alipata fursa ya kulutana na familia kadhaa ambazo zimerudi nyumbani baada ya miaka mingi ya kuishi kama wakimbizi wa ndani au wakimbizi katika nchi zingine.
Filippo Grandi leo ametoa ombi jipya la kuongezwa kwa misaada ya kibinadamu nchini humo.
Akiwa ziarani Syria alizuru katika mji wa Talbiseh huko Homs, ambapo alizungumza na Abeer, mama wa watoto saba. Familia yake imehama makazi yao mara mbili katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
Uchovu na kusambaratishwa kwa nyumba
Kamishna Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa amesema kwamba "baada ya miaka 10 ya mateso, familia nchini Syria zimechoka" na akasisitiza kuwa ameshuhudia "nguvu na dhamira waliyonayo watu hao katika kujenga maisha yao".
Grandi ameongeza kuwa UNHCR na washirika wake husaidia familia kukarabati madirisha na milango katika nyumba ambazo ambazo zimeharibiwa na vita, lakini watu hawa bado wanahitaji maji na umeme.
Mkuu wa UNHCR pia amesema shule na hospitali zinahitaji kurudi kufanyakazi na kwamba ni muhimu kwa Wasyria kupata riziki.
Sehemu kubwa ya kazi ya shirika hilo la Umoja wa Mataifa ni kutafuta suluhisho kwa wakimbizi na wakimbizi wa ndani ambao wanarudi katika miji yao nchini Syria na kuwasaidia kutotegemea sana misaada ya kibinadamu.
Zaidi ya Wasyria milioni 13 wameachwa bila makao baada ya miaka 10 ya vita na 350,000 wamepoteza maisha.
Takriban wengine milioni 6.7 wamehama makazi yao huku watu wengine milioni 5.5 ni wakimbizi katika nchi tano za jirani.
Uwajibikaji wa serikali
Lakini Siyria na mataifa jirani wanakabiliwa na shida ya uchumi, iliyochochewa na athari za Covid-19, kushuka kwa thamani ya sarafu za ndani na mfumuko wa bei. UNHCR inaelezea kuwa kutokana na hali hii, watu waliotawanywa na wakimbizi wanalazimika kufanya maamuzi magumu".
Wakati wa ziara yake nchini Syria, Bwana. Grandi alikutana pia na waziri wa mambo ya nje Hussein Makhlouf na kuzungumza juu ya kurudi kwa familia za wakimbizi.
Kamishna mkuu amekumbusha kuwa watu hawa ni raia wa Syria na "serikali ina jukumu la kuhakikisha usalama wao."
Katiba Mpya
Wiki hii pia unaanza mchakato wa kuunda katiba mpya ya Syria.
Huko mjini Geneva Uswisi, mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa kwa nchi hiyo, Geir Pedersen, ameelezea kwamba amekutana na wawakilishi wa serikali na upinzani, ambao wanaunda kamati ya katiba ya Syria, na wote walikubaliana kuanza mchakato wa mageuzi ya katiba.
Wote wamekusanyika mjini Geneva kwa duru ya sita ya mazungumzo katika kipindi cha miaka miwili.
Hakuna maendeleo yaliyopatikana katika mkutano uliopita, uliofanyika mwezi Januari, lakini kulingana na mjumbe wa Umoja wa Mataifa, pande hizo zilithibitisha kuwa wakati huu, wako tayari kuanza kuandika katiba mpya.