Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Fanya mambo haya 15 uache kutupa chakula

Utupaji wa chakula kama unavyodhihirishwa hapa kwenye soko moja nchini Uganda. Hii ni changamoto siyo tu kwa wauzaji wa vyakula bali pia wakulima.
© FAO/Sumy Sadurni
Utupaji wa chakula kama unavyodhihirishwa hapa kwenye soko moja nchini Uganda. Hii ni changamoto siyo tu kwa wauzaji wa vyakula bali pia wakulima.

Fanya mambo haya 15 uache kutupa chakula

Masuala ya UM

Kupunguza upotevu na utupaji wa chakula ni muhimu katika dunia ambayo mamilioni ya watu wanalala njaa kila siku, limesema shirika la chakula na kilimo la Umoja wa Mataifa FAO.  

Shirika hilo limesisitiza “Tunapopunguza utupaji chakula, tunaheshimu kuwa chakula hakipatikani kirahisi kwa mamilioni ya watu ambao wanalala njaa kila uchao. Ni juu yetu kubadili tabia zetu ili kufanya upotevu wa chakula kutokuwa ndio mfumo wa maisha maisha.” 

FAO imeainisha hatua rahisi ambazo kila mmoja anaweza kuchukua ili kukithamini na kukienzi chakula: 

1. Tumia lishe bora na endelevu 

Maisha yanaenda kwa kasi na kuandaa chakula chenye lishe inaweza kuwa changamoto, lakini milo yenye afya si lazima itumie muda mrefu kuandaliwa. Mtandao umejaa mapishi ya haraka yenye afya ambayo unaweza kushiriki na familia yako na marafiki zako. 

2. Nunua tu kile unachohitaji 

Panga chakula chako. Fanya orodha ya ununuzi na uizingatie, na epuka ununuzi wa kukurupuka. Sio tu utapoteza chakula kidogo, bali pia utaokoa pesa yako! 

3. Chagua matunda na mboga zenye muonekano mbaya 

Usihukumu chakula kwa muonekano kwake. Matunda na mboga zenye umbo la kushangaza au zilizopondwa mara nyingi hutupiliwa mbali kwa sababu hazifikii viwango vya kupendezesha macho. Usijali kwni ladha ni ileile. Tumia matunda yaliyokomaa kwa kutengeneza urojo, juisi na kuyala jinsi yalivyo. 

Mlo wa dola 1.20 New York, unagharimu mkazi wa Sudan Kusini dola 349.
UN News/Daniel Dickinson
Mlo wa dola 1.20 New York, unagharimu mkazi wa Sudan Kusini dola 349.

4. Hifadhi chakula kwa busara 

Sogeza bidhaa za zamani mbele ya kabati yako au jokofu na mpya weka nyuma. Tumia vyombo visivyoingiza hewa kuweka chakula wazi kwenye jokofu na hakikisha vikasha vimefungwa ili kuzuia wadudu kuingia. 

5. Kuelewa uwekaji wa chakula hadi lini 

Kuna tofauti kubwa kati ya tarehe "bora kabla ya " na "matumizi ifikapo ". Wakati mwingine chakula bado ni salama kula baada ya tarehe isemayo "bora kabla ya", lakini ni tarehe isemayo "matumizi ifikapo" ambayo inakuambia wakati gaani ni mwisho wa kutumia au sio salama tena kula.  

Angalia maandishi yanayoelezea kuhusu chakula hivyo kwa ajili ya  ya chakula vitu au viungo visivyofaa kwa afya kama vile mafuta na vihifadhi na epuka vyakula vilivyoengezwa sukari au chumvi. 

6. Anza kidogo 

Chukua sehemu ndogo nyumbani au shiriki sehemu kubwa kwenye mikahawa. 

7.Penda mabaki yako 

Endapo hutoweza kula kila kitu, kihifadhi kilichosalia kwenye jokofu kwa ajili ya baadaye au tumia mabaki hayo kuandaa mlo mwingine. 

8. Geuza mabaki ya chakula kuwa mbolea 

Badala ya kutupa mabaki ya chakula chako, yatumie kama mbolea. Kwa njia hii unarudisha virutubishi kwenye mchanga na kupunguza kiwango cha uzalishaji wako wa hewa ukaa. 

9. Heshimu chakula 

Chakula kinatuunganisha wote. Ungana tena na chakula kwa kujua mchakato wa kukiandaa. Soma juu ya uzalishaji wa chakula na uwajue wakulima wako. 

10. Saidia wakulima wa eneo lako 

Kwa kununua mazao ya ndani, unasaidia wakulima wa familia na wafanyabiashara ndogo ndogo katika jamii yako. Unasaidia pia kupambana na uchafuzi wa mazingira kwa kupunguza umbali wa kusafirisha chakula kwa malori na magari mengine. 

11. Kula samaki kwa wingi 

Kula zaidi aina mbalimbali za Samaki kama vile mackerel au sill, badala ya zile zilizo katika hatari ya kuvuliwa kupita kiasi, kama papa au jodari. Nunua samaki waliovuliwa au kufugwa kwa njia endelevu, kama samaki waliowekwa alama ya kujali mazingira au waliothibitishwa. 

12. Tumia maji kidogo 

Hatuwezi kuzalisha chakula bila maji. Ingawa ni muhimu kwamba wakulima watumie maji kidogo kukuza chakula, kupunguza taka ya chakula pia kunaokoa rasilimali zote za maji zilizoingia katika kuzalisha chakula.  

Punguza matumizi yako ya maji kwa njia zingine pia kama kukarabati mabomba yanayovuja au kufunga mabomba ya maji wakati unasafisha meno yako! 

13. Tunza udongo na maji 

Taka zingine za nyumbani zina hatari na hazipaswi kutupwa kwenye pipa la taka za kawaida. Vitu kama betri, rangi, simu za rununu, dawa, kemikali, mbolea, matairi, makasha ya wino, n.k zinaweza kuingia kwenye mchanga na mfumo wa usambazaji wa maji, na kuharibu rasilimali za asili zinazozalisha chakula chetu. 

14. Kula zaidi jamii ya kunde na mboga 

Mara moja kwa wiki, jaribu kula chakula cha jamii ya kunde au nafaka za kale kama vile quinoa. 

15. Gawia wenzako chakula

Changia na wengine chakula ambacho kingepotea bure. Kwa mfano, apu zinaweza kuwaunganisha majirani wao kwa wao na wafanyabiashara wa ndani ili chakula cha ziada kiweze kugawanywa, na sio kutupwa.