Wakati wa kutokomeza silaha za maangamizi za nyuklia ni sasa:Guterres
Wakati wa kutokomeza silaha za maangamizi za nyuklia ni sasa:Guterres
"Sasa ni wakati wa kuondoa silaha za nyuklia kutoka kwenye ulimwengu huu, na kuanzisha enzi mpya ya mazungumzo, uaminifu na amani", amesema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres Jumapili, katika ujumbe wake wa kuadhimisha siku ya kimataifa ya Kukomesha silaha za nyuklia.
Bwana Guterres amebainisha kuwa kushughulikia tishio la silaha za nyuklia “imekuwa msingi wa kazi ya Umoja wa Mataifa tangu kuanzishwa kwake, lilipopitishwa azimio la kwanza la Baraza Kuu kuhusu silaha hizo mwaka 1946 likitaka "kuondolewa silaha zote za atomiki na silaha zingine zote zinazoweza kusababisha maangamizi makuu kote duniani."
Lakini, mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa amesema kwamba, ingawa idadi ya silaha za nyuklia zimekuwa zikipungua kwa miongo kadhaa, zingine 14,000 zimehifadhiwa kote ulimwenguni, na kuifanya dunia kukabiliwa na hatari kubwa zaidi ya nyuklia kwa karibu miongo minne "Nchi zinaendelea kuimarisha vituo vya silaha za nyuklia, na tunaona ishara zenye kutia wasiwasi za mashindano mapya ya silaha. Ubinadamu bado unaendelea kuwa karibu na silaha za maangamizi ya nyuklia suala ambalo halikubaliki.”
Mkataba wa kupinga nyuklia uko njiapanda
Siku ya Alhamisi, juma hili mkuu wa Umoja wa Mataifa alitoa wito kwa tnchi zote zinazoshikilia teknolojia ya nyuklia kutia saini mkataba wa kina wa kupiga marufuku matumizi ya nyuklia (CTBT), ambao ulipitishwa mwaka 1996, na umesainiwa na nchi 185.
Ili mkataba wa CTBT uanze kutumika, lazima utiwe saini na kuridhiwa na nchi 44 zilizo na teknolojia ya nyuklia, ambazo nane bado hazijaridhia mkataba huo, China, Misri, India, Iran, Israel, Jamhuri ya Kidemokrasia ya watu wa Korea , Pakistan na Marekani."Tumebaki katika hali hii ya sintofahamu kwa muda mrefu," amesema Katibu Mkuu.
Ishara za matumaini
Bwana Guterres hata hivyo anaona uamuzi wa Urusi na Marekani kuongeza muda mpya wa kuanza mkakati wa kupunguza silaha na kushiriki mazungumzo, kama ishara ya matumaini.
Ameongeza kuwa mkataba wa kuzuia silaha za nyuklia, ambao ulianza kutumika mnamo Januari, pia ni hatua ya kukaribisha.
Wajibu wa kuendeleza hatua hizi, amesema Katibu Mkuu, uko mikononi mwa nchi wanachama.
Alifafanua kua mkutano wa wa kkataba wa Kutokuzagaa kwa silaha za nyuklia, uliopangwa kufanyika mnamo Januari 2022, kama ni fursa ya nchi zote kuchukua hatua kwa kivitendo kuzuia matumizi na kuondoa silaha hizo za nyuklia.
Amehimiza kuwa "Sasa ni wakati wa kuondoa wingu hili moja kwa moja, kuondoa silaha za nyuklia kutoka katika ulimwengu wetu", amehimiza Bwana Guterres, na kuongeza kuwa " Piani zama za kuanzisha enzi mpya ya mazungumzo, uaminifu na amani kwa watu wote".