Hali inayoendelea kuzorota Lebanon inatia hofu:Guterres
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameelezea wasiwasi wake mkubwa kuhusu hali ya kiuchumi na kijamii inayoendelea kuzorota kwa haraka nchini Lebanon.
Kupitia taarifa iliyotolewa leo na msemaji wake mjini New York Marekani Guterres amesema “Watu wa Lebanon wanahangaika kila uchao kutokana na mfumoko wa bei, upungufu mkubwa wa mafuta, umeme, madawa n ahata fursa za kupata maji safi.”
Taarifa hiyo inasema Katibu Mkuu ametoa wito kwa viongozi wote wa kisia nchini Lebanon kuanzisha mara moja serikali inayofanyakazi ya umoja wa kitaifa ambayo itawaweza kuwapunguzia madhila mara moja watu wa taifa hilo, kuleta haki na uwajibikaji kwa watu wa Lebanon.
Pia amesema serikali hiyo inapaswa kuwa ya kuleta mabadiliko ya maana ili kurejesha fursa za watu kupata mahitaji ya msingi, kurejesha utulivu, kuchagiza maendeleo endelevu na kuhamasisha matumaini na mustakbali bora kwa wote.