Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Taliban ni lazima muheshimu haki za binadamu Afghanistan hazina mjadala:HRC

Kamishina Mkuu wa Haki za binadamu Michelle Bachelet akizungumza kwenye kikao maalum kuhusu Afghanstan kwenye Baraza la Haki za Binadamu
UNOG
Kamishina Mkuu wa Haki za binadamu Michelle Bachelet akizungumza kwenye kikao maalum kuhusu Afghanstan kwenye Baraza la Haki za Binadamu

Taliban ni lazima muheshimu haki za binadamu Afghanistan hazina mjadala:HRC

Haki za binadamu

Baraza la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa leo limetoa wito kwa kundi la Taliban linalishika hatamu hivi sasa nchini Afghanistan kuheshiimu haki za binadamu, sheria za kimataifa na kutozima matumaini ya raia wan chi hiyo.

Katika kikao chake cha 31 kilichofanyika leo mjini Geneba Uswis Baraza la Haki za binadamu limesema lina hofu kufuatia ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu nchini Afghanistan.  

Katika taarifa yake kwenye kikao hicha Kamishina mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Michelle Bachelet amesistiza kwamba “Sheria za kimataifa za haki za binadamu hazina mjadala, na kwa watu kufurahia haki za binadamu haijalishi nani anayeshika hatamu au ndiye mwenye mamlaka. Vijana nchini Aghanistan wamekuwa na matumaini ya mustakbali bora na kutaka kuwa huru, kufanya maamuzi yao lakini pia akienzi utamaduni na dini zao , hivyo haipaswi kuzima matumaini hayo sasa.” 

Ameongeza kuwa mtazamo huo umekuwepo kwa muda mrefu na itakuwa vigumu kufuta sasa kwa kuwa tu anayeshikilia usukani ni mtu au kundi lingine. 

 

WFP ikitoa msaada wa fedha kwa familia zilizoathirika na machafuko Afghanistan
© WFP/Massoud Hossaini
WFP ikitoa msaada wa fedha kwa familia zilizoathirika na machafuko Afghanistan

Kwa mantiki hiyo Bi. Bachellet amesema “Nawasihi sana Taliban wazingatie kanuni za utawala unaosikiliza na kuzingatia haki za binadamu, na wafanye kazi ili kuanzisha tena mshikamano wa kijamii na maridhiano pamoja na kuheshimu haki za wote ambao wameteseka katika miongo ya mizozo. Mstari wa hatari usiopaswa kuvukwa itakuwa ndio kipimo chao Taliban hususan watakavyowatendea wanawake na wasichana, na kuheshimu haki zao za uhuru, uhuru wa kutembea, elimu, kujieleza na ajira, zikiongozwa na kanuni za kimataifa za haki za binadamu. Hasa, kuhakikisha upatikanaji wa elimu bora ya sekondari kwa wasichana itakuwa kiashiria muhimu cha utekelezaji wa haki za binadamu.” 

Kikao hicho pia kimepitisha mswada wa azimio linatotoa wito wa kheshimu haki za binadamu za watu wote, umezitaka pande zote katika mzozo kuheshimu wajibu wao chini ya sheria za kimataifa za kibinadamu, kusitisha uhasama mara moja na kujizuia na machafuko zaidi, limeitaka jumuiya ya kimataifa kuendelea kujihusisha na Afghanistan hasa katika hali ya kisiasa, kibinadamu, haki za binadamu na maendeleo, pia limeityaka jumuiya ya kimataifa wakiwemo wahisani kutoa msaada unaohitajika kwa raia wa Afghanistan na jamii zinazowahitaji na limetoa ombi kwa Kamisha mkuu kuwasilisha ripoti ya kinachoendelea Afghanistan ikiwemo uwajibikaji kwa wanaokiuka haki za binadamu.