Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mtangazaji nchini Tanzania aliyezushiwa kufa na Corona awashauri watu wapate chanjo 

Mwandishi habari Gloria Michael ambaye aliugua COVID-19 na kwa bahati nzuri kupona sasa anachagiza watu wachanjwe.
Gloria Michael.
Mwandishi habari Gloria Michael ambaye aliugua COVID-19 na kwa bahati nzuri kupona sasa anachagiza watu wachanjwe.

Mtangazaji nchini Tanzania aliyezushiwa kufa na Corona awashauri watu wapate chanjo 

Afya
  • Aliugua Corona April 2020
  • Wizara ya Afya ilimpa ushauri wa kisaikolojia
  • Alipata chanjo ya Covid-19 siku ya kwanza zoezi la utoaji chanjo lilipoanza nchini Tanzania

Ugonjwa wa COVID-19 umeathiri watu wengi kwa njia mbali mbali iwe kutokana na wao binafsi kuugua au familia au rafiki wa karibu. Hali ni kama hiyo kwa mwandishi wa habari wa shirika la utangazaji Tanzania, TBC Gloria Michael kwa mara ya kwanza tangu azushiwe kufariki dunia kwa ugonjwa wa Corona amezungumza na Leah Mushi kusimulia masaibu yake yaliyomkumba na kuwashauri wananchi wote kuacha kusita na kwenda kupata chanjo.

Gloria anaanza simulizi yake kabla ya kukutana na maswahibu hayo.

“April tarehe 5, 2020 nilikuwa na homa kali sana, nikaenda hospitali, muuguzi alivyonipima na kukuta nina nyuzi joto 40 katika kipimo cha selsiyasi, aliniuliza iwapo nimesafiri ndani ya siku 14 nami nilimjibu ndio kwani nilikuwa nimetoka mkoani Arusha kwenye msiba. Muuguzi alivyosikia hivyo alishtuka sana na alinipa barakoa na kunitaka nikae pembeni nisubiri sikufahamu kwanini lakini akili ikaanza kuniambia hapa kuna tatizo. “ 

Baada ya vipimo alirudi kuendelea na matibabu nyumbani akisema, “Nilirejea nyumbani, hali yangu haikuwa nzuri, nilikuwa na homa kali naumwa viungo naumwa sana kichwa, lakini nikapeleka ruhusa kwa muajiri wangu niliyopewa hospitali na nikarejea nyumbani kupumzika” 

Siku chache baadaye alipata ripoti ya vifo miongoni mwa wale anaowafahamu na uvumi ukaenea kuwa naye amefariki dunia!  “Nilivyoamka asubuhi nilikuta ujumbe mwingi sana na simu imepigwa sana usiku kucha, na hapo hapo mume wangu akaanza kupokea simu za watu wakimuuliza iwapo taarifa zinazosambaa mitandaoni kuwa nimekufa ni za kweli. Nilifungua simu yangu na kukuta picha za ujumbe wa  watu wamenitumia jinsi taarifa zinavyosambaa zilisema nililazwa katika hospitali ya Mloganzila na nimefariki dunia kwa ugonjwa wa Corona, sio hisia njema sana” 

Gloria alipatiwa msaada wa kisaikolojia, Naishukuru sana wizara kwani nilipatiwa ushauri wa kisaikolojia mzuri sana, kwakweli sijawahi kupata huduma nzuri kama kipindi kile, nadhani na wenyewe walikuwa na wasiwasi kwamba mbona tuna idadi ya vifo vyote nchini na hiki changu hawakitambui? Nawashukuru sana sana kwakweli nimehudumiwa vizuri mpaka nilipopona.” 

Chanjo ya COVID-19

Na vipi kuhusu chanjo wakati huu ambapo tayari serikali ya Tanzania imeridhia chanjo ya COVID-19 kutolewa kwa wananchi? “Siku Rais wetu Samia Suluhu Hassan alivyosema anaunda jopo kumshauri kuhusu chanjo nilifurahi sana, na nikaweka nia siku chanjo ikija nchini lazima nitahakikisha naipata, na kweli nimeipata, nimechoma siku ya kwanza kabisa aliyochoma rais Ikulu. chanjo.” 

Gloria anamalizia kwakutoa ushauri, “Nikweli chanjo ni hiari lakini ikiwa hujaugua ugonjwa huu ndio unaona sawa lakini ukiugua kama mimi nilivyougua utaona ni namna gani ni muhimu kuipata, na kw akuwa chanjo ni bure mimi naomba nikushauri uende ukapate chanjo”